Sunday, January 19, 2020

TANI 60 ZA KOROSHO GHAFI ZAKOSA WANUNUZI LINDI.

Mwenyekiti wa chama kikuu cha ushirika cha Lindi Mwambao Mohamed Duka akifungua kikao cha mnada wa Korosho uliofanyika katika chama cha msingi Kiwalala AMCOS Halmashauri ya Mtama, PICHA NA HADIJA HASSAN.
..................................................


Na HADIJA HASSAN, LINDI.

ZAIDI ya Tani 60 za korosho ghafi kutoka chama kikuu cha ushirika cha Lindi Mwambao kinachojumuisha Wakulima wa Wilaya za Mtama, Kilwa na Manispaa ya Lindi Mkoani humo zilizopelekwa kwenye Mnada wa 10 wa chama hicho zimekosa wanunuzi.

Korosho hizo zilizokosa wanunuzi ni Korosho daraja la kwanza tani 4 na kg 318 na daraja la pili tani 6 na kg 74 kutoka ghala la Buko Lindi na Tani 50 daraja la pili kuoka ghala la Nangurukuru Kilwa.

Kwa mujibu wa Afisa ushirika wa Mkoa wa Lindi Richard Zengo alisema kuwa katika mnada wa 10 uliofanyika jana Januari 18, 2020 katika Chama cha Msingi cha Ushirika Kiwalala AMCOS halmashauri ya Mtama jumla ya tani 1057 na kg 761 zilifikishwa mnadani huku mnunuzi mmoja tu ndie aliyeomba kununua korosho hizo.

Zengo alisema katika mnada huo korosho Tani 150 na kg 827 Daraja la kwanza kutoka ghala la Mtama na Tani 378 na kg 827 za Ghala la Nangurukuru ziliuzwa kwa bei ya Shilingi 2015 na huku Daraja la pili tani 38 na kg 198 kutoka Ghala la mtama na tani 429 na kg 993 kwa bei ya shilingi 1560.

Awali Akiwasalimu wananchi wa Kilwalala Diwani wa kata hiyo kabla ya kutangazwa kwa bei hizo za korosho alitumia fursa hiyo kuwashauri wananchi hao kuridhia kuuza korosho hizo kwa bei iliyoko sokoni.


"Kwa kuwa mnunuzi aliyetufikia ni mmoja na bei tumezisikia Sisi hatuna namna niwasihi wakulima wenzangu kuipokea bei hii wajanja wanasema pesa haikataliwi hivyo katika mjadala wetu wote tukumbuke kuwa sisi ndio tuliopewa dhamana ya kuuza ama kuto kuuza korosho hizi hivyo sio vibaya kwa Kuzingatia hali ya maisha ya sasa sisi tukaitikia hiyo bei iliyopo kuuza korosho zetu" aliwasihi wananchi hao.

Hata hivyo ushauri wa Diwani huyo uliungwa mkono na wakulima waliohudhuria katika mnada huo kwa pamoja kuridhia kuuza korosho hizo kwa bei zilizopo sokoni.

Akifunga kikao hicho cha Mnada wa korosho Mwenekiti wa chama hicho Mohamed Duka aliwapongeza wakulima hao kwa maamuzi ya busara ya kuridhia kuuza korosho zao kwa bei iliyopo Sokoni.


MWENYEKITI WA KIJIJI ATUHUMIWA KUUZA ARDHI CHALINZE.

 Mwenyekiti wa kiji cha Tukamisasa, Kata ya Ubena Amani Msasu akijitetea kwenye Mkutano wa hadhara kuhusu tuhuma za yeye kuuza ardhi ekari 400, pembeni yake kushoto ni Afisa Tarafa, Tarafa ya Chalinze, Thomas Molel.
...............................................

Na Omary Mngindo, Chalinze

WAKAZI wa Kijiji cha Tukamisasa Kata ya Ubena Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoa wa Pwani, wanamtuhumu Mwenyekiti wao Amani Msasu wakidai ameuza ardhi ekari 400.

Katika Mkutano Maalumu ulio ombwa na wananchi kwa lengo la kutoa tamko la kumkataa Mwenyekiti huyo, chini ya Afisa Tarafa, Tarafa ya Chalinze, Thomas Molel, wakazi hao walisema kuwa wakimtuhumu Msasu kuwa ameuza ardhi hiyo mali ya kijiji.

Shujaa Theophil wa kwanza kuzungumza ambapo alisema Msasu kabla ya nafasi hiyo alikuwa anauza ardhi, na kuwa alipochaguliwa akishirikiana na watu hao wamefanya mpango wa kuwauzia taasisi ya VICOBA ya Dar es Salaam ekari 400 mali ya wanakijiji.

"Hatuna imani na Mwenyekiti, ana mpango wa kuuza ardhi yetu eka 400 kwa kikundi cha VICOBA kinachotokea Dar es Salaam, mara mbili tumevamiwa na magari yakiwa na wanachama wamevalia sare wakisema wamekuja kuangalia ardhi yao," alisema Theophil.

Mkazi Fatuma Matitu alisema kuwa tuhuma hizo kwa Mwenyekiti hazina ukweli, na kwamba zinalenga kumchafua, huku akisema kuwa hiyo ardhi inayodaiwa imeuzwa iko salama.

Machaku Bunga aliuambia mkutano huo kuwa Msasu anapotoshwa na baadhi ya wakazi wanaomzunguka wakijihusisha na uuzwaji wa ardhi kijiiini hapo, na kwamba alishawahi kumwita kwa lengo la kutaka kumtaadhalisha juu ya hilo.

"Nilimuita Msasu kwa lengo la kutaka kumtaadharisha kuhusiana na watu waliomzunguuka ambao wanajulikana sana hapa kijijini kwa uuzaji wa ardhi za wananchi, lakini alinipuuza," alisema Machaku.


Nae mkazi Godian Mazoezi alisema kuwa wanakijiji hawana imani na Mwenyekiti huyo, kwani ameonesha hatokuwa na msaada kwa wananchi, na hiyo inatokana na dhamira yake ya kutaka kuuza ardhi hiyo mali ya wana-Tukamisasa.

Akitoa utetezi mbele ya Afisa Tarafa na mamia ya wananchi waliohudhuria mkutano huo, Msasu alisema kwamba yeye amewahi kuuza ekari 30 za ardhi kijijini hapo ambazo ni mali ya wanafamilia na si kwamba ameuza ekari 400 mali ya kijiji kama inavyodaiwa.

"Hata mimi kuna siku nikiwa hapa kijijini nimewaona wanachama wa SACCOS kutoka Dar es Salaam wakiungana na baadhi yao wakazi wa hapa Tukamisasa wakitaka waoneshwe ardhi ambayo wanadai kuinunua, nilishangazwa na hilo," alisema Msasu.

Akihitimisha mkutano huo, Afisa Tarafa, Tarafa ya Chalinze, Thomas Molel alianza kutoa elimu ya ardhi huku akisema kijiji kina mamlaka ya kuuza mwisho ekari 50 tu, na kwamba zaidi ya hapo wenye mamlaka ya kuidhinisha malipo ni ngazi ya wilaya.

"Kama ardhi ni mali ya familia lazima kuwepo na muhtasari wa wanafamilia wakikubaliana juu ya uuzwaji huo, kisha unafikishwa kwenye mkutano mkuu wa kijiji kwa kuridhia uuzwaji huo," alimalizia Molel.
  
Mkazi wa kijiji chicho cha Tukamisasa, Shujaa Theophil akizungumza katika mkutano huo. PICHA ZOTE NA OMARY MNGINDO.


Friday, January 17, 2020

UBORESHAJI DAFTARI LA WAPIGA KURA LINDI WAELEKEA UKINGONI

NA HADIJA HASSAN, LINDI.

Wakati zoezi la uandikishaji wa dafatari la kudumu la wapiga kura likiwa linaelekea mwishoni katika mikoa ya Lindi na Mtwara, baadhi ya wananchi wa wilaya ya Kilwa mkoani Lindi wameelezea changamoto mbali mbali zinazolikabili zoezi hilo ikiwemo ya usumbufu wa baadhi ya mashine za BVR.

Wakizungmza na Bagamoyo kwanza Blog baadhi ya wananchi wa kilwa masoko, somanga, na Kinjumbi waliofika katika vituo vya kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura wameeleza kuwapo na changamoto za baadhi ya mashine ambazo huwalazimu kusubiri kwa muda.

Nae Mohamed Linena Mkazi wa Kilwa Masoko alisema kuwa baada ya kufika katika kituo cha kujiandikisha wapiga Kura alilazimika kusubiri kwa masaa kadhaa katika kituo hicho kuendelea na zoezi hilo kutokana na mashine hizo kusumbua mpaka pale fundi wa (BVR) alipofika na kufanya marekebisho katika mashine hizo.

Nae mwandikishaji mkuu wa kituo cha ofisi ya Serikali ya Kijiji Somanga Kusini kata ya Somanga alisema kuwa licha ya ya changamoto hizo, zoezi hilo limeenda vizuri kwa siku zote isipokuwa siku ya nne ndio kulitokea changamoto kwenye mashine hiyo ya BVR hali iliyowalazimu kusimamisha kwa muda zoezi la uandikishaji.

Nae mwandikishaji Msaidizi wa kituo hicho cha Somanga kusini, Yusra Mtulya –alisema kuwa Inapotokea changamoto kama hiyo ya hitilafu ya mashine kwa muda mrefu huwalazimu wananchi wanaokwenda kujiandikisha kuwapeleka katika kituo cha jirani ili waweze kujiandikisha.

Kwa upande wake IT wa BVR Operate ambae alikataa kutaja Jina lake aliieleza Bagamoyo kwanza Blog kuwa maranyingi hitilafu zinazojitokeza katika mashine hizo za BVR zinatokana na kuhamishwa hamishwa kwa mashine hali inayopelekea baadhi ya waya kuchomoka au kukatika hiyo inatoka na aina ya usafiri unaotumika na hasa kwa hali ya bara bara ilivyo.

Nae Ofisa Uchaguzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa Ally Ligalawike alisema changamoto hiyo ya kusumbua kwa mashine za BVR unatokana na Jografia ya maeneo husika kwani yapo maeneo ambayo hayana umeme kabisa hali inayowalazimu wasimamizi wa maeneo hayo kuisafirisha mashine hiyo hadi maeneo jirani ambako umeme unapatikana ili waweze kuichaji kwa ajili ya matumizi ya siku inayofuata

" kutokana na hali ya Bara bara hasa katika kipindi hiki cha masika maeneo mengi magari yanashindwa kufika hiyo ulazimika kutumia usafiri wa baiskeli au pikipiki ili kutafuta umeme wa kuchaji mashine hizo kwa ajili ya matumizi ya siku inayofuata"

Alisema hali hiyo inafanya mashine zilete hitirafu mara kwa mara kwa baadhi ya maeneo yenye changamoto hiyo.

Hata hivyo Ligalawike aliesema kuwa ili kukabiliana na changamoto hiyo Halmashauri imetoa magari sita ambayo yatatumika kwa dharula katika tarafa sita za Halmashauri hiyo kwa kushirikiana na mafundi (BVR Operate) kutoka tume ya Taifa ya Uchaguzi NEC.

Kuhusu hali ya zoezi inavyokwenda alisema zoezi linaendelea vizuri kwani mpaka sasa tayari wameshaandikisha zaidi ya asilimia 70 ya lengo walilojiwekea kuandikisha wapiga Kura wa Wilaya hiyo.

Zoezi la uandikishaji katika dafrati la kudumu la wapiga kura katika mikoa ya Lindi na Mtwara lilianza januari 12 mwaka huu wa 2020, ambapo linategemewa kufikia tamati januari 18 likiwa na lengo la kuandikisha wananchi waliofikisha umri wa kupiga kura, kuboresha taarifa za baadhi ya waliowahi kujiandikisha pamoja na kurekebisha taarifa za wasio na sifa ikiwamo waliofariki.

MWAKITINYA AWAPA SOMO UVCCM DODOMA

Na Omary Mngindo, Dodoma

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (MNEC-CCM) kundi la vijana Mussa Mwakitinya, amewataka vijana kuyasemea mazuri yanayotekelezwa na serikali ya awamu ya tano, chini ya Rais John Magufuli.

Aidha MNEC huyo amewakumbusha wanafunzi hao wanaosoma katika Chuo Kikuu cha Tanzania kilichopo Manispaa ya Dodoma, kutumia vyema masomo yao katika nyanja ya siasa ya Ujamaa, inayolenga kudumisha umoja, upendo na mshikamano katika nchi.

Mwakitinya ametoa kauli hiyo hivi karibuni akiwa mgeni rasmi kwenye Mkutano Mkuu wa Matawi mawili ya UVCCM, uliofanyika ndani ya Kata ya Ntyuka mbele ya Mwenyekiti Patrick Mathias, Katibu Aidan Kajivo na viongozi mbalimbali wa tawi la CBSL.

Mwakitinya alianza kwa salamu za Mwenyekiti wa CCM Taifa John Magufuli na Mwenyekiti wa UVCCM Kheri James, pia akipongeza kazi nzuri zinazotekelezwa na serikali, sanjali na Jumuiya hiyo kupata eneo la kujenga ofisi lililopo kata ya Ntyuka.

“Ndani ya chama na Serikali kuna macho yanakuangalia wakati mwenyewe usijue, niwakumbushe wana-CCM wenzangu tudumishe Umoja na mshikamano wetu katika kuelekea uchaguzi Mkuu, kwa kuhakikisha tunafuata misingi ya chama," alisema.

Aliongeza kuwa chama kinawahitaji watu wenye hulka kama za Dkt John Magufulli, na kwamba wawapime watu wanaokuja kuomba kura kwa kuangalia kama wanaendana na tabia ya Rais huyo.

"Tusiwape nafasi watu wanaopinga maendeleo na vibaraka wao katika kuelekea uchaguzi mkuu, vipo vyama vimepoteza mwelekeo, vinafanya siasa panapokuwepo na matukio, kutokee msiba, ajali, mafuriko na majanga mbalimbali, twendeni tukawapige mchana kweupee," alisema NEC huyo.


Aidha Mjumbe huyo wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kuwakilisha Vijana, ameviasa vyama vya siasa na baadhi ya wanasiasa, kuacha kuyapeleka masuala ya nchi kwa watu wa nje ya nchi, ambao hawahusiki na chochote cha nchi hii.

Kwa upande wake Katibu wa tawi la UDOM Mwinyi Halid alisema kuwa wao ni askari walio mstari wa mbele katika kukilinda Chama cha Mapinduzi (CCM0), pia wakiwa wasomi kazi yao ni kushauri na kupongeza panapofanyika mageuzi ya kiutendaji, yanayoleta athari chanya katika maisha ya watu.