Sunday, November 11, 2018

KIKAO CHA MAANDALIZI YA UNUNUZI KOROSHO


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, amekutana na Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, baadhi ya watendaji wa Serikali na Wakurugenzi wa mabenki na CBT jijini Dodoma Novemba 10.2018, kujadili maandalizi ya ununuzi wa korosho. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAISLAMU WANAWAKE WASHAURIWA KUANZISHA VIWANDA

Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Mwanza Alhaji Sheikh Hassan Musa Kabeke akizungumza na viongozi wa Jumuiya ya WAnawake wa Kiislamu Tanzania (JUWAKITA) kutoka wilaya za mkoa wa Mwanza, wakati wa hafla ya kuwatambulisha Mwenyekiti na katibu mteule wa jumuiya hiyo jana, Amina Ali Masenza na Dotto Mangu.
………………….................

NA BALTAZAR MASHAKA, MWANZA

WANAWAKE wa dini ya Kiislamu mkoani Mwanza wameaswa kuanzisha viwanda vidogo na vikundi vya ujasiriamali vitakavyotoa ajira na kuwasaidia  kujikomboa na umaskini wa kipato wakiwemo Watanzania wengine.

Rai hiyo ilitolewa jana na Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Mwanza, Alhaji Sheikh Hassan Musa Kabeke wakati akimtangaza mwenyekiti na katibu mteule wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislamu Tanzania (JUWAKITA) mkoani hapa.

Alisema akinamama wakianzisha viwanda vidogo watapata fursa ya kujikwamua na umaskini wa kipato lakini pia wakiwa na viwanda hivyo vitawasaidia na watanzania wengine maskini kupata ajira na hakutakuwa na ubaya wakishirikiana na wasio waislamu kujenga na kuanzisha viwanda.

Sheikh Kabeke alisema sera ya viwanda inalenga kuwafanya Watanzania kufikia uchumi wa kipato cha uchumi, hivyo haiwezekani wakafungiana wenyewe kwa wenyewe katika boksi na kuhoji, kuna ubaya gani kwa wanawake wa kiislamu kuanzisha viwanda.

 “Viwanda vidogo vya akina mama wakiwa navyo vitawasaidia na wengine masikini kujikomboa kiuchumi maana wapo watakaopata ajira hata kama ni vya kusindika nyanya,mananasi, mbogamboga na mazao mengine na hakuna ubaya kushirikiana na wasio waislamu,”

“Tunataka tuondokane nakubaguana huyu si mwislamu, huyu mkristo. Mbona damu tunayoongezwa hatuhoji , tunaishi kwenye nyumba na kusoma kwenye shule zisizo za waislamu.Hivyo kila mmoja wetu aimbe wimbo wa viwanda kuunga mkono serikali ya viwanda,”alisema Sheikh Kabeke.

Pia aliwashauri, kwa kuwa serikali imeondoa riba kwenye mikopo hiyo ya wanawake, vijana na walemavu, ni muda muafaka wa kuunda vikundi vya ujasiriamali na kuvisajili ili kuchangamkia fursa za mikopo ya fedha hizo zinazotolewa kwenye halmashauri za majiji,wilaya na miji.

Kaimu sheikh wa mkoa alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais John Magufuli kwa kutmiza miaka mitatu Ikulu kuwa uongozi wake ni makini kwa jinsi anavyosimamia rasilimali za nchi ili ziwanufaishe wanyonge na kupinga ufisadi.

“ Rais Magufuli ni kiongozi wa mfano, tunampongeza kwa umakini na ujasiri pamoja na serikali yake.Amesimamia kwa umakini na umahiri wa hali ya juu rasilimali zilizokuwa zinaporwa na wajanja wachache,hana ubaguzi na BAKWATA katupatia msikiti na anawajali wananchi wanyonge,”alisema.

Aidha, alieleza kuwa waislamu wanahitaji maendeleo ya elimu dini,kisera na kiuchumi wakiwemo watu wazima na watoto lakini walikatishwa tama na baadhi ya watu waliwachangisha na fedha hizo hazikufanya kazi iliyokusudiwa hima iliwanufaisha wao kwa kujimilikisha miradi.

“Tunahitaji maendeleo, viongozi wachangie dini yao na kila baada ya miezi mitatu tutakutana kufanya tathmini ya kilichopatikana na kuamua kifanye kazi gani maana huko nyuma waislamu walikatishwa tama na wajanja kujinufaisha na michango yao,” kaimu sheikh huyo wa mkoa.

Kuhusu vitendo vya ushoga alidai vimetokana an kumomonyoka kwa maadili na utandawazi mambo yaliyotufikisha kwenye dhambi hiyo ingawa wapo watu wanaofanya vitendo hivyo kwa kulazimisha na umaskini wa kipato na kiakili.

Hivyo ili kuondokana na hali hiyo viongozi wa dini waliopo serikalini waungane na washirikiane kutatua kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili waislamu ikiwa ni pamoja na kuwasaidia watoto wa kiislamu kupata elimu bora ya dini.

‘MO’ DEWJI AKUTANA NA UONGOZI MPYA SIMBA.


 Bilionea Mohammed ‘Mo’ Dewji (kulia) akiwa na Mdhamini wa klabu ya Simba SC, Ramesh Patel (kushoto) kwenye kikao cha jana Novemba 10, 2018.
......................................

MFANYABIASHARA Bilionea, Mohammed ‘Mo’ Dewji amekutana na Bodi ya Wakurugenzi ya klabu hiyo iliyochaguliwa katika uchaguzi Mkuu wa klabu uliofanyika Novemba 5 mjini Dar es Salaam.

Kikao hicho kilihusisha viongozi waliomaliza muda wao, chini ya kaimu Rais Salum Abdallah ‘Try Again’ na Mdhamini wa klabu, Ramesh Patel. 
Mo Dewji alitambulishwa rasmi Bodi ya Ukurugenzi ya Simba chini ya Mwenyekiti, Swedy Nkwabi na Wajumbe Hussein Kitta Mlinga, Dk. Zawadi Ally Kadunda, Suleiman Haroub Said, Mwina Mohammed Kaduguda na Asha Ramadhani Baraka.

Mo Dewji, Mbunge wa zamani wa Singida Mjini, kukubali kununua asilimia 49 za hisa za klabu ya Simba SC kulingana na maelekezo ya Serikali badala ya asilimia 51 alizotaka yeye awali katika mkutano Desemba 3, mwaka jana, ambao uliazimia kumfanya mwanahisa mkuu wa klabu katika mfumo mpya wa uendeshwaji.

Mo pekee aliweka dau la Sh Bilioni 20 kuomba asilimia 50 ya hisa, baada ya klabu kutangaza kuuza asilimia 50 ya hisa zake kwa Sh. Bilioni 20 miezi miwili iliyopita, ingawa baadaye Serikali ikaagiza klabu hiyo isiuze zaidi ya asilimia 49 kwa mtu mmoja.

Wanachama 1320 walihudhuria mkutano huo wa Desemba 3, mwaka jana kutoka Dar es Salaam na mikoa jirani na kwa furaha ya ushindi huo, Mo Dewji alitoa ahadi 10 za kuleta mabadiliko makubwa, ikiwemo ujenzi wa Uwanja wa mazoezi wa nyasi za asili na nyasi bandia pamoja na hosteli ya kisasa ya wachezaji.

Na uchaguzi wa Jumapili iliyopita Simba SC ulifanyika baada ya uongozi uliopita ulioingia madarakani juni 30, mwaka 2014 chini ya Rais, Evans Elieza Aveva, Makamu wa Rais, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ na Wajumbe Iddi Kajuna, Said Tully, Collins Frisch, Ally Suru na Jasmine Badour kumaliza muda wake.

Lakini Aveva na Kaburu hawakufanikiwa kumalizia muda wao madarakani, kufuatia kuwekwa rumande katika gereza la Keko tangu Juni 29, mwaka jana kwa tuhuma za kughushi nyaraka, kesi ambayo bado inaendelea katika Mahakama ya Kisutu mjini Dar es Salaam.

Na Julai 1, mwaka jana, Kamati ya Utendaji iliwateua ‘Try Again’ na Iddi Kajuna kukaimu nafasi za Aveva na Kaburu na hao ndiyo waliosimamia mchakato mzima wa mabadiliko ya klabu kuelekea uchaguzi huo.

Nkwabi ambaye amekidhi matakwa ya Katiba mpya ya Simba SC kuwa na elimu ya Shahada sasa ataongoza Bodi ya Wakurugenzi itakayokuwa na Wajumbe wanane chini yake huku akiwa na mamlaka ya kuteua Wajumbe wengine wanne, kati yao mmoja lazima awe mwanamke ili kukamilisha Bodi ya Ukurugenzi ya watu wanane.

Aidha, Mo Dewji anakutana na Bodi ya Ukurugenzi ya klabu siku moja tu baada ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kutaja ratiba ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2018- 2019, Simba ikipangiwa kuanza na Mbabane Swallows Swaziland katika Raundi ya Awali ya mchujo.

Na Wekundu wa Msimbazi, wakifanikiwa kuvuka mtihani huo, watakwenda hatua ya mwisho ya mchujo kuwania kuingia hatua ya makundi ya michuano hiyo, ambako watamenyana na mshindi kati ya Uniao Desportiva Do Songo ya Msumbiji na Nkana FC ya Zambia, anayochezea beki wake wa zamani, Mtanzania, Hassan Kessy aliyewahi kucheza na Yanga pia.
 Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba SC na viongozi waliomaliza muda wao katika kikao cha leo