Monday, October 9, 2017

ABDUL SHARIFU ZAHORO, MWENYEKITI MPYA WA CCM BAGAMOYO.

Mwenyekiti Mpya wa CCM Wialaya ya Bagamoyo, alhaj Abdul Sharif Zahoro akiwa amepokelewa kata ya Kisutu, Mjini Bagamoyo.
 ............................................

MWENYEKITI mpya wa chama cha mapinduzi (CCM) wilayani Bagamoyo ,alhaj Abdulsharif Zahoro ,amesema atahakikisha anasimamia mali na vitega uchumi vya chama ili kiweze kujitegemea na kuondokana na hali ya kuwa ombaomba.


Aidha amedhamiria kwa dhati kukipigania chama kivitendo ,kufuatilia utekelezaji wa ilani kwenye ,mashina,matawi,kata na halmashauri ili kuweka njia nyepesi ya ushindi katika chaguzi za serikali za mitaa 2019 na uchaguzi mkuu 2020 .

Pamoja na hayo ,alhaj Abdulsharif ,amewataka wenyeviti wa vitongoji,madiwani na wabunge wilayani humo ,kutumia dhamana na nafasi walizochaguliwa kutekeleza ahadi walizozitoa  kwa wananchi kabla ya kusubiria kukaribia kwa uchaguzi .

Aliyasema hayo ,wakati alipo pokelewa na wanachama wilayani Bagamoyo,kata ya Kisutu ,ambapo ndipo alipozaliwa na kukomaa kisiasa ,baada ya kuchaguliwa nafasi hiyo kwa kupata kura 711.

Abdulsharif aliomba ushirikiano kwa wanachama ,viongozi kuanzia ngazi za chini na ambao kura hazikutosha kumuunga mkono ili kuimarisha chama kiweze kusonga mbele .

Mwenyekiti huyo ,alieleza CCM wilayani humo ina mali zake hivyo ni jukumu lake kufuatilia mapato na kuinua zile ambazo zinaonekana zinayumba kimapato .

Alhaj Abdulsharif alisema kuwa,haiwezekani vibanda vya biashara ambavyo vipo chini ya chama wilaya vikalipa fedha kwa kutumia njia zisizo kwenye maandishi ,suala ambalo atahakikisha analifuatilia ili kuongeza mapato na chama kiweze kujiendesha .

“Chama hiki kina vitega uchumi vingi ,na hizi hizi zinaweza kutuvusha kwenye hii hali ya kutembeza kibakuli kuombaomba ,tunapaswa kupigania vitega uchumi vyetu tujikomboe “

“Mie sijaja kufuata fedha ndani ya chama ,ninachotaka chama kijikwamue kiuchumi na tusimamie kwa umoja wetu ilani kwa lengo la kuendelea kushika dola ” alifafanua alhaj Abdulsharif .

Hata hivyo ,alisema kila mmoja atabeba mzigo wake kwani ambae atabainika kufanya ubadhilifu kwenye mali za chama hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake .

Alhaj Abdulsharif alizitaka,halmashauri zitekeleze ilani kwa kuboresha huduma za kijamii .

“Nitafuatilia ,tusimamie ilani na wataalamu ,kwani kuna mambo yapo sawa na mengine hayajakaa vizuri sana ,tuwekane sawa ,tutatue kero za wananchi kwa maslahi ya Bagamoyo,Chalinze na taifa kijumla” alisema.

Alisema asilimia ya fedha za kundi la vijana na wanawake ni lazima yatolewe kwa walengwa waweze kujiinua kimaisha .

Alieleza ,kujenga chama sio jambo la mchezo ,waungane kwa umoja wana Chalinze na Bagamoyo kufanya mabadiliko ya kimaendeleo ili kuziba upenyo kwa vyama pinzani .

Abdulsharif alibainisha kuwa ,siasa ni makundi ,ni demokrasia ,lakini uchaguzi ukiisha makundi yote yanapaswa kuwa pamoja kushikamana na kuondoa tofauti zao .

Aliwashukuru wanachama wote wa CCM ,wajumbe wa mkutano mkuu wa chama waliomchagua na ambao hawakumchagua na kusema hana kinyongo na mtu kilicho mbele ni kufanya kazi .

Katika uchaguzi uliofanyika kumchagua mwenyekiti mpya wa CCM wilayani hapo ,Abdulsharif alishinda kwa kupata kura 711 dhidi ya kura 383 za Alma’s Masukuzi huku Tariq Kifuru akipata kura 185 .

Nafasi ya Katibu Mwenezi ilikwenda kwa John Francis maarufu kama Bolizozo aliyepata kura 112 akimshinda Hassan Sharifu aliyepata kura 4

 


Saturday, October 7, 2017

VIDEO RAIS AFANYA MABADILIKO BARAZA LA MAWAZIRI




RAIS MAGUFULI AFANYA MABADILIKO BARAZA LA MAWAZIRI.



Wizara zilizogawanywa ni Wizara ya nishati na madini ambayo ilikuwa wizara moja na sasa zitakuwa wizara mbili ambazo ni Wizara ya Nishati inayojitegemea ambayo itakuwa na naibu waziri na naibu wazriri na wizara ya Madini ambayo pia itakuwa na waziri na naibu waziri.

Wizara nyingine iliyogawanywa ni Wizara ya Kilimo, Mifugo, na Uvuvi ambazo sasa zitakuwa wizara mbili, wizara ya kilimo itakayojitegemea ambayo itakuwa na waziri na naibu waziri na wizara ya Mifugo na uvuvi ambayo pia itakuwa na waziri na naibu waziri wake.

Aidha, mabadiliko mengine yamefanyika kwenye wizara ya Viwanda, Biashara na uwekezaji ambayo sasa itakuwa na naibu waziri wakati hapo awali ilikuwa haina naibu waziri huku wizara ya TAMISEMI itakuwa na manaibu waziri wawili badala ya yule mmoja wa awali.

Katika mabadiliko hayo Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imeongezewa naibu waziri ambapo sasa itakuwa na manaibu waziri wawili ambao mmoja atashughulikia mawasiliano na uchukuzi na mwingine atashughulikia ujenzi.

Kutokana na mabadiliko hayo wizara zimeongezeka kutoka 19 hadi 21 na manaibu waziri wameongezeka kutoka 16 na hadi 21, na kufanya idadi ya nafasi za mawaziri zilizoongezwa ni mbili na nafasi za manaibu waziri zilizoongezeka ni tano.

Rais Dkt. John magufuli amewataja mawaziri walioingia kwenye Baraza jipya la mawaziri kuwa ni:-

 1.Waziri wa Ofisi ya Rais Menejmenti ya utumishi wa uma na tawala bora, ni George Huruma Mkuchika

2.Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ni Selemani Saidi Jafo.
manaibu waziri ni Josephat Sikamba Kandege na George Kakunda.

3.Waziri wa Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira, ni Januari yusufu Makamba naibu waziri ni Kangi Lugola.

4.Waziri wa  Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, ni Jenista Johakim Muhagama, Naibu Waziri kazi, vijana na ajira ni Antoni Piter Mavunde.naibu waziri walemavu ni  Stela Alex Ikupa.

5.Waziri wa kiilimo  ni DKT. Injinia  Charles Chizeba, Naibu waziri ni  Dkt. Mere Machachu Mwanjelwa.

6. Waziri wa Mifugo na Uvuvi  ni Luhaga Mpina, Naibu waziri ni Abdallah Hamisi Ulega.

7. Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ni Prof. Makame Mnyaa Mbalawa, Naibu Waziri ni 7.injinia Etashanta Justus Nditie na Eliasi John Kwandikwa. 

8. Waziri wa Fedha na mipango ni Dkt. Philipo Mpango, naibu waziri ni Dkt. Ashantu Kijaju.

9. Waziri wa  Nishati ni Dkt. Medadi Matogolo Kalemani, Naibu waziri ni Subira Hamisi Mgalu.

10. Waziri wa Madini ni Angela Kairuki naibu waziri ni Haruni S. Nyongo.

11.Waziri wa Katiba na Sheria ni Paramagamba Kabudi.

12. Waziri wa mambo ya nje, ushirikiano wa Afrika mashariki kikanda na kimataifa Dkt. Agustino Mahiga, naibu waziri  Dkt. Suzani Kolimba.

13. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa ni Dkt. Husein Mwinyi
14. Waziri wa mambo ya ndani ni Mwigulu Lameki Nchemba naibu Waziri Hamadi Yusufu Masauni.

15. Waziri wa Maliasili na utalii ni Dkt. Hamisi Andrea Kigwangwala naibu waziri ni Ngailonga Josephati Hasunga.

16. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ni Wiliamu Lukuvi naibu waziri Engelina Sylvester Mabula .

17. Waziri wa Viwanda, Biashara na uwekezaji ni Charles Paul Mwijage naibu waziri injinia Stela Manyanya.

18. Waziri wa Elimu na mafunzo ya Ufundi ni Joyce Ndalichako Naibu waziri ni Wiliamu Ole nasha.

19. Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto ni Ummy Mwalimu naibu wake ni 19Faustin Ndungulile.

20. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ni Dkt. Harson George Mwakyembe, naibu wake ni 20Juliana Daniel Shonza.

21. Waziri wa Maji na Umwagiliaji, I sack Aloece Kamwelwe naibu wake ni Juma Hamidu Awesu.

Aidha, Rais Dkt. Magufuli amefanya mabadiliko kwa katibu wa Bunge na kumteua Dkt. Stephen Kagaigai.

Rais Dkt. John Magufuli alisema wateule wote waliotajwa wataapishwa jumatatu Tarehe 09 Oktoba 2017.saa tatu Asubuhi.    

Friday, October 6, 2017

RC NDIKILO AWASIMAMISHA KAZI WATUMISHI WAWILI WA KAMPUNI INAYOJENGA RELI YA STANDARD GAUGE

SAM_6008
Mwakilishi wa kampuni ya Yapi Merkezi ya nchini Uturuki ,inayojenga mradi wa reli ya Standard Gauge kutoka Dar es Salaam- Morogoro,Mhandisi Mert Oz ,(aliyesimama katikatika )akimuonyesha maelezo yaliyomo kwenye karatasi,mkuu wa mkoa wa Pwani ,Mhandisi Evarist Ndikilo(wa kwanza kushoto) wakati alipokwenda kutembelea mradi huo huko Soga wilaya ya Kibaha.
Picha na Mwamvua Mwinyi
......................

Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha

MKUU wa Mkoa wa Pwani ,mhandisi Evarist Ndikilo amewasimamisha kazi watumishi wawili wa kampuni ya ujenzi ya Yapi Merkezi ya nchini Uturuki inayojenga reli ya Standard Gauge kutoka Dar es Salaam- Morogoro kwa tuhuma za rushwa ya ajira.

Aidha ameagiza watumishi hao wasimamishwe kupisha uchunguzi huku akitoa siku saba kwa vyombo vya dola kufuatilia suala hilo.

Mkuu huyo wa mkoa ,aliyasema hayo wakati alipotembelea ujenzi wa mradi huo kwenye kijiji cha Soga wilayani Kibaha .

Mhandisi Ndikilo,alieleza kuwa endapo ikibainika wamehusika na vitendo hivyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aliwataja watumishi hao ambao walikuwa wakilalamikiwa na wananchi waliokuwa wakienda kuomba kazi kuwa walikuwa wakiomba rushwa ni pamoja na Nelson ambae ametambulika kwa jina moja ofisa mwajiri (HR) kwenye kampuni hiyo .

Mwingine ni Torong’ong’o ambaye ni dereva wa moja ya viongozi wa kampuni hiyo ambao hawakuhudhuria hata kwenye mkutano huo.

Awali mhandisi Ndikilo alipokelewa kwa mabango na watu waliokuwa nje ya kampuni hiyo wakilalamika kunyimwa ajira upande wa madereva na waendeshaji wa mitambo wakidai kuwa ajira zinatolewa kwa njia ya rushwa.
“Tunanyimwa ajira hasa tunaotoka maeneo ya Kibaha na mkoa wa Pwani kwa ujumla na wanaoajiriwa ni watu wa nje ya mkoa”walisema.

Mhandisi Ndikilo,alielezea kwamba alikuwa pia akipelekewa malalamiko ofisini kwake ambapo baadhi ya madereva waliandika majina yao na kuambatanisha vyeti vyao na uzoefu wao wa kazi lakini hawakupata ajira.

“Malalamiko yamekuwa ni mengi sana na wanaolalamika wanasema wamenyimwa ajira wengi ni wa hapa Kibaha na mkoa wa Pwani ambao walipaswa kunufaika na mradi huu kwani kila eneo lenye mradi lazima wahusika wa eneo wapewe kipaumbele “
“Inadaiwa walioajiriwa hata 100 hawafiki katia ya 390 ya walioajiriwa,” alisema Ndikilo.

“Tumeambiwa kuna baadhi wanaajiriwa kusikojulikana wakija hapa wanaingizwa moja kwa moja na kati ya wafanyakazi 390 wengi wanatoka nje ya mkoa huku wa hapa wakiambulia kula vumbi tu wakishinda hapa nje bila ya mafanikio,” alisema mhandisi Ndikilo.

Akizungumzia suala hilo Diwani wa Kata ya Soga Ramadhan Chezeni alisema taarifa kuwa wapo  watu wameajiriwa kwa kufuata sifa si la kweli.
Alieleza kuna vijana wengi wanasifa zinazostahili lakini wanasumbuliwa bila ya kupata ajira.

Kwa upande wake   Meneja mradi huo uliochini ya Reli Assets Holding Company (RAHCO) ,mhandisi Maizo Mgedzi alisema suala la rushwa halifahamu .

Alisema anachojua wanaoajiriwa wote ni wenye sifa na vigezo ,na wanatoka nchini bila ya kujali eneo analotoka.

Mgedzi alisema kuwa watahakikisha wanalifuatilia suala hilo ili kupisha uchunguzi lengo likiwa ni kuhakikisha hakuna malalamiko kwa wananchi wanaozunguka eneo la mradi huo.

Naye mwakilishi wa kampuni ya Yapi Merkezi  Mhandisi Mert Oz alisema,endapo watabaini wapo walioingizwa kwenye ajira kinyume cha utaratibu,hawatasita kuwaondoa.

Oz alisema , wanafuata taratibu za ajira na wanategemea kuletewa wafanyakazi kwa utaratibu wa nchi na kufuata sheria za ajira.
 SAM_5973

MKUU wa Mkoa wa Pwani ,Mhandisi Evarist Ndikilo akipokelewa kwa mabango na baadhi ya watu ,wakati alipokwenda mradi wa reli ya Standard Gauge kutoka Dar es Salaam- Morogoro inayojengwa na kampuni ya ujenzi ya Yapi Merkezi ya nchini Uturuki ,huko Soga wilayani Kibaha.

MAGAZETI YA LEO TAREHE 06 OKTOBA 2017.