Saturday, December 21, 2024

WANAFUNZI KIDOGOZERO WAISHUKURU LION.

 







Na Omary Mngindo, Kidogozero.



WANAFUNZI wanaioishi katika mazingira hatarishi wakilelewa kwenye kituo cha Faraja, Kijiji cha Kidogozero Kata ya Vigwaza Chalinze wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani, wameishukuru Lion Club (Host) ya jijini Dar esa Salaam kwa kuwapatia misaada.


Shukrani hizo zimetolewa na wanafunzi Enjo Frank na Faraji Ramadhani baada ya kupokea vifaa vya shule na vyakula vyenye shilingi milioni 1.6, vikikabidhiwa na Rais Mahmood Rajvan, Mountazir Barwani na viongozi wenzao walipofika kijijini hapo kuwafariji watoto hao 41.


"Namshukuru Mwenyeezimungu kwani sikutegemea kupata msaada kama huu, utakaonisaidia katika masomo yangu wakati shule ikifunguliwa, mungu awasaidie na awaongezee pale mlipopunguza," alisema Enjo.


Nae Ramadhani alieleza kwamba kwa msaada huo wa begi, madaftari  pamoja na peni vimempatia chachu ya kuendelea na masomo, huku akiahidi kufanya vizuri zaidi katika elimu yake ya Sekondari.


Kwa upande wao wazazi Mohamed Ally aliishukuru Lion huku akiwahimiza wanafunzi kuongeza bidii katika kusoma, na kwamba zawadi hizo ziwe chachu ya kufanya vizuri zaidi kwenye masomo yao.


Evat Mapunda alielezea shukrani zake kwa uongozi huo kwa msaada mkubwa ambao wamewapatia watoto hao, na kuwa kijana wake amepoteza wazazi wote wawili hivyo yupo mikononi mwake hivyo msaada huo umekuwa faraja kubwa kwake.


"Kijana wangu hana baba hana mama mimi ndio anayenitegemea hivyo vifaa hivi vimenigomboa, muendelee na moyo huo wa kusaidia watoto kama hawa hasanteni sana," alimalizia Evat.


Katibu wa kikundi hicho Zena Mindu mbali ya kuwashukuru Lion, pia ameuomba uongozi huo kuendelea kukisaidia kikundi hicho kinacholea watoto hao hao, huku wakiwa hawana msaada wowote.


"Nawashukuru sana mlikuja Ruvu Darajani kukabidhi Matenki ya maji pamoja na vifaa vya shule, nami mlinikabidhi msaada, leo mmekuja hukuhuku Kidogozero ambako ndio tunakosihi na kutusaidia vifaa vya shule pamoja na vyakula, tunawashukuru sana," alisema Mindu.


Akizungumza kwa niaba ya Diwani Mussa Gama, Katibu wake Amos Mwakamale alitoa shukrani kwa Lion huku akiwataka wazazi waaoishi na watoto hao kuhakikisha shule ziapofunguliwa wote wanakwenda kusoma.


Mwenyekiti wa Kijiji Said Sango alimshukuru Barwani na viongozi wote, kwa kuendeleza kazi aliyoianza kijana wake Mouhsin Barwani aliyekuwa Diwani wa Kata hiyo miaka mitano iliyopita.


"Nimefurahi kuona mnaendelea kutusaidia Kata ya Vigwaza, tunaona kama bado tupo na Mohsin Barwani aliyekuwa diwani wetu miaka mitano iliyopita, hapa Kidogozero kuna tenki alilolitoa  shuleni mpaka leo linatumika, tunawashukuru sana," alisema Sango.


Akitoa neno kwa wanafunzi hao, Barwani aliwataka wanfunzi hao kukazania masomo, na kwamba taifa linawategemea katika kulitumikia miaka ijayo panapouhai, hivyo wakazanie elimu.


Tuesday, December 17, 2024

WAZIRI KIKWETE AHUDHURIA MASHINDANO YA QUR ANI KWA WENYE ULEMAVU.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye ulemavu, Ridhiwani Kikwete  ameshiriki mashindano ya Usomaji wa Quraan Takatifu kwa Wenye Ulemavu yaliyoandaliwa na Taasisi ya Riziki Lulida yaliyofanyika jijini Dodoma.


Katika mashindano hayo ambayo yalikutanisha Wenye Ulemavu kutoka makundi mbalimbali, Waziri Kikwete alitoa  salamu za serikali na kuwakumbusha kazi nzuri anayoifanya Mh. Samia Suluhu Hassan , Rais wa Jamhuri Ya Muungano ya Tanzania ikiwemo Mkakati wa kusimamia Haki na Ustawi wa Wenye Ualbino, Sera ya Usimamizi wa Teknolojia saidizi na mapitizo ya sera mbalimbali zinazosimamia maslahi ya Wenye Ulemavu ikiwemo sera ambazo haziendani na mazingira ya sasa. 


Aidha alisema Wizara kwa upande wao walieleza walipofikia katika kila maelekezo ya Mh. Rais, Ilani ya uchaguzi na miongozo mingi imetolewa. 

Wameendelea kumpongeza Muandaaji wa mashindano hayo Bi. Riziki Lulida, na taasisi yake na Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na washiriki na kwa upekee Mh. Rais kwa kuunga mkono jambo hilo kwa kuchangia Shilingi Milioni 15. kwa vijana washiriki 30 walioshiriki usomaji wa Qur ani tukufu.



Tuesday, December 3, 2024

WATU 7 WAFARIKI AJALI YA GARI KARAGWE.

 

Na Alodia Dominick,  Karagwe.


Watu saba wamepoteza maisha huku wengine tisa wakijeruhiwa katika ajali iliyohusisha magari matatu ya haice, kosta pamoja na Lori aina ya scania katika kizuizi cha barabarani kilichopo kijiji cha Kihanga kata ya Kihanga wilaya ya Karagwe mkoani Kagera na chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva.


Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kagera Blasius Chatanda amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema imetokea Desemba 03, 2024 saa 5:00 asubuhi  na kuhusisha lori aina ya scania yenye namba T621 AJQ lenye Tela namba T472 EAQ likiwa linatokea Kayanga wilaya ya Karagwe kwenda Kyaka lilipofika Kihanga katika kizuizi cha barabarani yalikuwepo magari mawili.


Ameongeza kuwa, moja lilikuwa kosta namba T367 ECP pamoja na toyota  haice yenye namba za usajili T973 DGD yakiwa yamesimama yanaendelea kukaguliwa na maafisa uhamiaji mita kama kumi kutoka kwenye kizuizi ndipo Scania iliyagonga kutokea nyuma na kusababisha ajali hiyo.


"Gari hilo limetokea Mbeya likiwa limebeba mchele kuupeleka Mtukula na baada ya kushusha mchele lilipata mzigo mwingine Karagwe wa kurudi nao Mbeya ambao ni parachichi, huyu dereva ni mgeni katika eneo hilo kwa uzembe na kutokuchukua tahadhari alikuja katika mwendo ambao ni mkali akaigonga toyota haice pamoja na kosta" amesema Chatanda.


Aidha, katika ajali hiyo vimetokea vifo saba wanawake wanne, mwanaume mmoja na watoto wawili huku majeruhi wakiwa tisa wanaume wanne na wanawake watano.


Amesema uzembe wa dereva umesababisha ajali kwani inaonekana alikuja katika mwende mkali lakini ajali haikusababishwa na kufeli breki kwani huko nyuma alikotoka alipita katika mlima wa Kishoju na kwenye kona hivyo ingekuwa breki ule mteremko asingeumaliza.


"Ni wazi kwamba tahadhari za alama barabarani hakuzichukua kwani barabara hiyo inazo alama za barabara na hata kabla ya kizuizi kuna alama pia" amesema Chatanda.


Mmoja wa mashuhuda Adamu Alon mtengeneza majokofu kutoka Kayanga amesema kuwa, ameitwa na mteja Kyaka wilaya ya Misenyi na kupanda Kosta ambayo imehusika kwenye ajali walivyofika Mgakorongo walikuta hilo lori likiwa limesimama dereva anaongea na askari wa usalama barabarani wakapita.


Amesema, wakati gari hilo limefika Kihanga katika kizuizi cha barabarani ndipo Scania hiyo imegonga gari lao likiwa linakaguliwa na maafisa uhamiaji yeye alikuwa amekaa kiti cha mbele na dereva huku akitakiwa kuonyesha kitambulisho na afisa uhamiaji ndipo amesikia kishindo kikubwa na gari alilokuwemo likahama na kwenda mbele.


Ameeleza kuwa, yeye na afisa uhamiaji wamedondoka chini baadaye alipopata fahamu alikuta scania waliyoipita Mgakorongo ndiyo iliwagonga.


Majeruhi wamelazwa katika hospitali ya wilaya ya Karagwe iliyopo Nyakanongo pamoja na miili ya marehemu imehifadhiwa katika hospitali hiyo.







Friday, November 29, 2024

VIONGOZI WATEULE WA VITONGOJI NA VIJIJI WAAPA BAGAMOYO.

 







Viongozi wa Vitongoji na Vijiji pamoja na Wajumbe wao walioshinda katika uchaguzi uliofanyika tarehe 27 Novemba 2024. Leo tarehe 29 Novemba 2024 wameapishwa rasmi kushika nyadhifa zao katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo. 

Akifungua kikao cha kuwaapisha Viongozi hao, Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Bagamoyo Bw Shauri Selenda aliwakaribisha na kuwashukuru kwa kuchaguliwa  na kuaminiwa na wananchi katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika tarehe 27 mwezi huu .

"Nichukue nafasi kwa niaba yangu mimi mwenyewe na kwa niaba ya Halmashsuri kwa kuteuliwa kuwa viongozi wa Serikali za Mitaa,  "Mchakato haukuwa rahisi lakini mmefanikiwa niwapongeze". Alisema Bw Shauri Selenda.

 Katika Uchaguzi huo ulifanyika tarehe 27 Novembe, 2024 vyama mbalimbali vya kisiasa vilishiriki kikamilifu katika uchaguzi huo kwenye vitongoji vyote   167 vya Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo. 

     Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Mhe.Shaibu Ndemanga aliwaasa wenyeviti  hao kushirikiana ili kuwahudumia wananchi kama walivyoapa katika viapo vyao.

CCM YASHINDA KWA ASILIMIA 98.82 LINDI

 

NA HADIJA OMARY, LINDI.


Msimamizi wa Uchaguzi Manispaa ya Lindi Mkoani Humo bwana Juma Mnwele Leo tarehe 29 November 2024 ametangaza matokeo ya Jumla ya uchaguzi wa Serikali za mitaa vijiji na vitongoji Katika Manispaa hiyo uliofanyika November 27 mwaka huu 2024


Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake msimamizi huyo wa uchaguzi Manispaa ya Lindi amesema Kati ya nafasi za uongozi 1954 zilizoshindaniwa na Vyama vya siasa chama cha mapinduzi kimeshinda nafasi 1931 sawa na asilimia 98.82, chama cha ACT wazalendo wameshinda nafasi 21 sawa na asilimia 1.07


Alitaja chama chama kingine ni chadema ambacho kilishinda nafasi 2 sawa na asilimia 0.1 kikifuatiwa na chama cha wananchi cuf ambacho kimeshinda nafasi 1 sawa na asilimia 0.05 huku chama cha CHAUMA, NCCR MAGEUZI na TLP vikikosa ushindi kabisa

Monday, November 25, 2024

RAIS SAMIA KUSHIRIKIANA NA THE ISLAMIC FOUNDATION KUANZISHA CHUO CHA UALIMU NA MAADILI.

 

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameridhia kushirikiana na Taasisi ya The Islamic Foundation kuanzisha Chuo cha Ualimu na Maadili katika eneo la Kitungwa wilayani Morogoro.


Rais Dkt. Samia ameyasema hayo leo tarehe 25 Novemba 2024 wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi katika Msikiti wa Al Ghaith uliopo maeneo ya Kilakala Flats/old Dar es Salaam Road mjini Morogoro unaomilikiwa na Taasisi ya The Islamic Foundation Chini ya Mwenyekiti wake Aref Nahdi


Aidha, Rais Dkt. Samia amesema katika kipindi hiki dunia imekumbwa na mmomonyoko wa maadili kuna haja kubwa ya kuongeza ujenzi wa Madrasa ili ziwe vituo vya kuwalea watoto kiimani na maadili.


Aliwahimiza wazazi kusimamia malezi bora ya watoto ili jamii iwe na kizazi chenye hofu ya Mungu, na maadili mema.


Akizungumzia mmomonyoko wa maadili, Mwenyekiti wa Taasisi ya The Islamic Foundation, Aref Nahdi, amesema jamii ya sasa imecha ushirikiano katika malezi jamno linalopelekea watoto kupoteza heshima katika jamii na kuharibikiwa kimaadili.


Alisema zamani ilikuwa mtoto akikosea anapewa onyo na mtu yeyote aliyemzidi umri na kwamba taarifa zikifika nyumba kwa mtoto huyo mzazi wa mtoto anaongeza kumpa adhabu ili iwe fundisho kwa mtoto huyo


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akifungua kitambaa kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi Msikiti wa Al Ghaith uliopo maeneo ya Kilakala Flats/old Dar es Salaam Road mjini Morogoro unaomilikiwa na Taasisi ya The Islamic Foundation Chini ya Mwenyekiti wake Aref Nahdi (kushoto)









Mwenyekiti wa Taasisi ya The Islamic Foundation, Aref Nahdi akizungumza na waandiaji wa habari katika tukio la uwekaji wa jiwe la msingi Msikiti wa Al Ghaith uliopo maeneo ya Kilakala Flats/old Dar es Salaam Road mjini Morogoro, ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 25 Novemba 2024.





Saturday, November 16, 2024

HEART TO HEART YASAIDIA MRADI WA MAJI ZAHANATI YA NAMUPA

 






NA HADIJA OMARY,   LINDI.


Hatua ya Taasisi ya heart to heart Foundation kwa ufadhili wa KOICA kuchimba kisima cha maji Katika Zahanati ya namupa iliyopo Katika Kata ya nyangao halmashauri ya Mtama Mkoani Lindi  inaelezwa kuwa ni msaada kwa wanawake wajawazito wanaokwenda kujifungua Katika Zahanati hiyo kutobeba maji kutoka majumbani kwao



Kwa mujibu wa taarifa ya Mganga Mfawidi wa Zahanati hiyo Dr. Paul Dominic alisema mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bi victoria Mwanziva Jana November 15, 2024 wakati wa makabidhiano ya kisima hicho ni kwamba kutokana na  tatizo hilo la  ukosefu wa maji  Katika Zahanati hiyo inawalazimu kina mama wanaofika kwa ajili ya kujifungua  kubeba maji kutoka majumbani 


" Katika kipindi ambacho kina mama walikuwa wanakuja kupatiwa huduma ya kujifungua Katika Zahanati yetu  walikuwa wanalazimika kubeba maji kutoka majumbani kwao na wengine wanabeba kutoka mtoni kwa ajili ya kuweza kusaidia kukabiliana na upungufu wa maji ulikuwepo na kuweza kukamilisha zoezi la mama kujifungua ambalo linahitaji maji mengi".


Hata hivyo Dkt Dominic alisema kuwa kapatikana kwa maji hayo pia kutaweza kusaidia kupunguza magonjwa yote yanayotokana na maji.


Nae Melina Simon Amesema tatizo hilo lilikuwa likiwafanya wamama wajawazito kutoka kijijini wakiwa na maji na pengina yasitosheleze mahitaji na kulazimika kurudi tena nyumbani kwa mara ya pili ili kufuata maji mengine ili kumalizia kupata huduma hiyo.


Mratibu wa Mradi kutoka heart to heart Foundation Innocent Deus Amesema Utekelezaji wa mradi huo ni moja ya kuunga mkono juhudi za serikali katika kuleta maendeleo kwenye jamii husika ambapo  kupitia Mradi huo wa miaka mitatu Taasisi hiyo inalenga kufikisha huduma ya maji Safi na salama Katika vituo vya Afya na Zahanati 15 ndani ya halmashauri hiyo ya Mtama .


Amesema Katika kijiji hicho cha Namupa ujenzi huo umehusisha huduma Kwenye Zahanati hiyo pamoja na kusogeza huduma hiyo kwa wananchi .


"Kingine tumeona kulikuwa na changamoto Katika chumba cha kujifungulia ambapo kwenye hicho chumba kulikuwa hakuna huduma ya maji hivyo Katika hii Zahanati ya namupa kwa sababu tumetaka iwe ya mfano tumeunganisha pia huduma hiyo kwenye hicho chumba cha kujifungulia".


Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bi victoria Mwanziva akimuwakilisha Mkuu wa mkoa huo amesema kama serikali ya wilaya  itaendelea kuthamini mchango unaotolewa na taasisi mbalimbali ikiwemo heart to heart katika kuunga mkono jitihada za serikali katika kutatua changamoto za wananchi ambapo aliwataka wananchi kulinda miundombinu hiyo ya maji ili idumu kwa muda mrefu.


"Mheshimiwa Rais Samia suluhu Hassan amewekeza Sana Katika sekta mbalimbali, amewekeza Katika sekta ya maji, Elimu,  sekta ya Afya lakini tunapowapata Wadau wetu kama hawa heart to heart Foundation wanakuja kuongezea nguvu Sisi hatuna budi  kuwashukuru Sana Sana" 


GHOROFA LAPOROMOKA KARIAKOO

 


Jengo la ghorofa Kariakoo mtaa wa Kongo na Mchikichi Jijini Dar es aalaam limeporomoka leo asubui Novemba 16, 2024. huku watu kadhaa wakiwa chini ya kifusi

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Albert Charamila amefika eneo la tukio na kuwataka walio hai ndani ya jengo hilo wawe watulivu ili kuona namna ya kuwaokoa 

Vikosi vya jeshi la ukoaji na zimamoto tayati vimewasili eneo la tukio, Vikosi vya jeshi la polisi vimefika eneo la tukio 

Juhudi za kuokoa watu zinaendelea kwa kushirikiana vikosi vya jeshi la uokoaji na zimamoto, jeshi la polisi na wananchi wote waliopo eneo la tukio wakitoa ushirikiano

Sunday, November 10, 2024

MUFTI NA SHEIK MKUU WA TANZANIA APONGEZA MRADI WA KUTAFSIRI QUR’AN TUKUFU NENO-KWA-NENO KWA LUGHA YA KISWAHILI

 


Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakary Zubeiry bin Ally, amempongeza Dkt. Shehnaz Shaikh kwa kazi yake ya kujitolea katika kuandaa tafsiri ya Qur’an neno-kwa-neno kwa lugha ya Kiswahili.
 
Katika mkutano uliofanyika leo ofisini kwake Kinondoni, Dar es Salaam, mara baada ya swala ya Ijumaa, Dkt. Abubakary aliutambua mradi huo kama rasilimali nzuri kwa Waislamu wanaozungumza Kiswahili, na kwamba utawasaidia kuelewa Qur’an kwa undani wa kipekee.
 
Dkt. Shaikh, mzaliwa wa Gujarat, India, na kwa sasa akiishi Dallas, Marekani, aliandamana na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislamu, Bi Shamim Khan, na Alhaj Albert Marwa, ambaye aliratibu ziara yake. 
 
Dkt. Abubakary alitoa shukrani zake kwa kujitolea kwa Dkt. Shaikh, akibainisha kwamba ingawa wengi wanaweza kuelewa maana pana ya Qur’an, ni wachache wanaoweza kuifahamu kwa kina neno kwa neno. 
 
Uelewa huu, alieleza, huleta muunganiko wa kiroho na uwazi zaidi wa mafundisho ya Qur’an, jambo ambalo tafsiri yake inaleta ufahamu mkubwaa zaidi kwa wasomaji wa Kiswahili.
 
Dkt. Abubakary alisisitiza umuhimu wa lugha sahihi katika kutafsiri Qur’an, akisema kuwa Kiswahili kinahitaji umakini mkubwa wakati wa kufikisha maandiko ya Kiarabu. 
 
Alionyesha imani kwamba wasomi wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro (MUM), ambao watasaidia kukamilisha tafsiri hiyo, wana ujuzi wa kutosha kwa kazi hii nyeti.
 
Mufti pia alielezea umuhimu wa tafsiri hii ya neno kwa neno katika dunia ya sasa inayounganishwa zaidi, kwani Waislamu wengi, hasa vijana na wale wanaoishi katika maeneo yasiyozungumza Kiarabu, hukutana na changamoto ya kufikia lugha asilia ya Kiarabu ya Qur’an. 
 
Alisema ingawa tafsiri za jumla huleta uelewa wa kawaida, mara nyingi hukosa muundo na maana halisi ya Qur’an. Hivyo Tafsiri ya Dkt. Shaikh, kwa kutoa ufafanuzi sahihi wa neno kwa neno, inakuwa ni zana muhimu ya kujifunza na kutafakari, ikiwaruhusu wasio na ujuzi wa Kiarabu cha zamani kuelewa kwa undani Maandiko Matakatifu.
 
Dkt. Abubakary alimshukuru Alhaj Marwa kwa kuratibu ziara ya Dkt. Shaikh na kumsifu kwa kujitolea kwake kuendeleza elimu ya Kiislamu. Alielezea mradi wa tafsiri ya Dkt. Shaikh kama mfano bora wa wajibu wa kusambaza ujumbe wa Mwenyezi Mungu.
 
Kwa upande wake, Dkt. Shaikh alieleza shukrani zake kwa Mufti kwa kubariki mradi huo. Akihitimisha ziara yake ya siku tano, alishiriki kuwa tafsiri yake imekubaliwa na kutumiwa katika nchi kadhaa duniani. 
 
Amesema mradi huo haubadilishi hata nukta moja ya Qur’anbali kila neno katika Kitabu hicho Kitukufu kinatafsiriwa neno kwa neno kama lilivyo na kulitafsiri kwa Kiswahili.
 
Tangu mwaka 2010, Dkt. Shaikh ametoa matoleo matatu ya tafsiri ya Qur’an kwa Kiingereza na Kiurdu, pamoja na vitabu vya watoto, vinavyopatikana kwenye Amazon. Pia hutoa rasilimali za bure mtandaoni, ikiwemo mihadhara ya YouTube na PDF zinazoweza kupakuliwa.
 
Akiwa katika chuo cha MUM Morogoro, Dkt. Shaikh alishuhudia kuundwa kwa timu ya wahadhiri kumi ambao wataendeleza mradi wake, wakiwezeshwa kwa zana za teknolojia na maelekezo. 
 
Juhudi hii mpya inafuata kazi yake ya miaka kumi ya kutafsiri, ambayo sasa inasimama kama rasilimali muhimu kwa Waislamu wanaozungumza Kiingereza na Kiurdu duniani kote.