Saturday, March 30, 2024

TUISOME KWA WINGI QURAN TUKUFU-DK.MWINYI



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi amewahimiza Waumini wa Dini ya kiislamu kuendelea kuisoma kwa wingi Quran Tukufu katika kipindi hiki cha Mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Rais Dk.Mwinyi amesema hayo katika fainali za kwanza za Mashindano  ya kuhifadhi Quran  Tukufu  Afrika Mashariki yanayosimamiwa na Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar ikiwemo washiriki tisa kutoka nchi za Afrika Mashariki katika Uwanja wa  New Amaan  Complex, Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe 30 Machi 2024.

Aidha Rais Dk.Mwinyi ameiomba Ofisi ya Mufti  Mkuu wa Zanzibar kuzidisha juhudi za malezi ya vijana na kuwaongoza katika maadili na tabia njema ili wawe raia wema na wenye hofu ya Mungu.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuunga mkono mashindano hayo  kufanyika kila mwaka.

Kwa upande mwingine Rais Dk.Mwinyi amezipongeza Taasisi za Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kuandaa mashindano  hayo makubwa ambayo yanaitangaza Zanzibar.

Mshindi wa kwanza wa Mashindano hayo ni Mahmoud Kassim Nassor wa  Zanzibar aliyepata shilingi milioni  30 mshindi wa  pili Abdourahamane Papa Said  kutoka Comoro shilingi milioni 20 ,  na mshindi wa tatu Abdulrahman Mussa   kutoka Kenya shilingi milioni 10.














Saturday, March 16, 2024

MSIMAMIZI WA UCHAGUZI BAGAMOYO, AWAAPISHA MAKARANI WA UCHAGUZI MDOGO KATA YA FUKAYOSI.


 

Msimamizi wa uchaguzi jimbo la Bagamoyo Shauri Selenda, amewataka makarani waongozaji katika uchaguzi mdogo wa kata ya Fukayosi Halmashauri ya Bagamoyo, kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mafunzo watakayopewa.


Selenda ameyasema hayo alipokuwa akifungua mafunzo kwa Makarani waongozaji wa uchaguzi mdogo kata ya Fukayosi Haashauri ya Bagamoyo ambapo alisema makarani wanapaswa kuzingatia kanuni na sheria za uchaguzi katika kutekeleza majukumu yao kama watakavyoelekezwa katika mafunzo hayo.


Alisema kazi ya ukarani wa uchaguzi inahitaji uvumilivyu, subira na busara katika utendaji wake kwani kazi hiyo inawakutanisha na watu tofauti ambao wanahitaji kusikilizwa, kuelekezwa na kuongozwa juu ya kile wanachopaswa kufanya katika kutekeleza haki yao ya kikatiba ya kuchagua viongozi.


Makarani hao walikula kiapo cha kutekeleza majukumu hayo tayari kwaajili ya uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika Machi 20, 2024.


Kiti cha udiwani kata ya Fukayosi kimebaki wazi baada ya aliyekuwa Diwani wa kata hiyo kufariki dunia kwa maradhi ya shinikizo la damu mnamo mwezi Novemba mwaka 2023.


Akizungumza kwa niaba ya Makarani wenzake, Athumani Hassan Fundi, amesema watahakikisha wanazingatia kile wanachofundishwa ili kutekeleza majukumu yao kwa weledi

Alisema nia wameipokea kazi hiyo kwa moyo mmoja na wapo tayari kufuata maelekezo kwa mujibu wa sheria za uchaguzi ili kufanikisha kazi hiyo muhimu.





Monday, February 19, 2024

MILIONI 800 KUWASAIDIA WAHANGA WA MAFURIKO MULEBA.

 


Na Alodia Babara

 Bukoba,

Walengwa wapatao 482 walioathirika na mafuriko pamoja na upepo mkali  katika wilaya za Muleba na Manispaa ya Bukoba mwaka jana wanatarajia kupata msaada wa kibinadamu wenye malengo mbalimbali utakaoghalimu zaidi ya sh. milioni 800 kutoka taasisi zisizo za kiserikali.

Msaada  huo ambao unatolewa na Kanisa la Kiinjili la Kirutheli Tanzania KKKT Dayosisi ya Kaskazini Magharibi kwa ufadhili wa taasisis inayojihusisha na shughuli za kibinadamu kwa watu wenye majanga nchini Tanzania (TCRS) na taasisi ya Actalliance Tanzania Forum utakuwa wa mwaka mmoja utawezesha kutimiza malengo sita ambayo ni msaada wa chakula, uboreshaji wa makazi, msaada wa kisaikrojia, huduma za maji, elimu na Afya na usafi wa mazingira.

Akizindua mradi huo Februari 19, mwaka huu mkuu wa mkoa wa Kagera Fatuma Mwassa alisisitiza mambo matatu ikiwemo  matumizi ya fedha za walengwa, usimamizi mzuri pamoja na  elimu ya maafa kwa walengwa.

 Mwassa alieleza kuwa, anazo taarifa kuwa mradi huo utahusisha maswala ya fedha, akaelekeza maafisa wanaohusika na maafa upande wa Serikali kama maafisa maendeleo ya jamii, watendaji wa kata, madiwani na viongozi hadi ngazi ya wilaya kushirikiana na uongozi wa kanisa la Kiinjili la Kirutheli Tanzania dayosisi ya Kaskazini Mgharibi katika uhakiki wa walengwa ambao ni harisia ili mradi usije kunufaisha ambao siyo walengwa.

“Viongozi kuanzia ngazi ya kitongoji hadi wilaya ni lazima kushiriki kikamilifu wakati wa uhakiki na kutoa huduma kwa walengwa wanaostahili na ndiyo maana nyinyi viongozi mmehudhuria uzinduzi huu” amesema Mwassa.

Amesisitiza hilo baada ya kukumbana na changamoto wakati wa kugawa chakula kwa waathirika hao kilicholetwa na kamati ya maafa kutoka ofisi ya Waziri mkuu kwani ziliingizwa siasa na likaibuka vuguvugu wakitaka watu wote wapewe msaada huo na watu waliokuwa kwenye kata zilizokumbwa na maafa wakajitokeza wakidai wote wana shida.

Amesema tathimini ilishafanyika wenye uhitaji walishatambuliwa na kuwa viongozi wasiende kuzua la kuzua kwa kulazimisha wengine kuingia kwenye hiyo risti, kaya ambazo zitahusika baada ya uchunguzi ni 482 inajullikana na ndiyo bajeti iliyopo.

“Nitumie nafasi hii kusisitiza kuwa fedha zitakazotolewa zitumike kwa matumizi yaliyokusudiwa zisiwe chanzo cha ndoa kuvunjika na kusababisha ukatili wa kijinsia katika familia za walengwa” amesema Mwassa

Aidha aliongeza kuwa, mradi ujikite sana kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kujifunza namna ya kukabiliana na maafa, mfano wananchi waelimishwe kutojenga sehemu hatarishi zinazoweza kuhatarisha maisha yao na familia zao serikali inaposema maeneo haya hayafai kujengwa makazi basi watu wote wakubaliane na waache maeneo hayo.

Kwa  upande wake Mkurugenzi wa taasisi inayojihusisha na shughuli za kibinadamu kwa watu wenye majanga nchini Tanzania TCRS Samwel Mlay amesema kuwa, mradi utakuwa wa mwaka mmoja ulianza kutekelezwa Desemba mwaka jana na utakamilika Desemba mwaka huuu, utawezesha kutimiza malengo sita ambayo ni msaada wa chakula, uboreshaji wa makazi, msaada wa kisaikrojia, huduma za maji, elimu na afya na usafi wa mazingira.

Mlay amesema, mradi utaghalimu zaidi ya shl milioni 800 walengwa wapatao 482 walioathirika na mafuriko pamoja na upepo mkali  katika wilaya za Muleba na Manispaa ya Bukoba mwaka jana watanufaika na mradi huo ambapo katika wilaya ya Muleba ni kata mbili za Kashalunga na Kalambi na Manispaa ya Bukoba ni kata nne za Rwamishenyi, Hamugembe, Bilele na Kashai  zinatarajia kupata msaada wa kibinadamu katika nyanja mbalimbali kutoka katika  taasisi zisizo za kiserikali

Diwani wa kata ya Kashai Ramadhan Kambuga amesema kuwa, kutolewa kwa misaada hiyo kutasaidia kupunguza maumivu kwa wananchi waliokumbwa na mafuriko na upepo mkali.

 

Amesema wananchi waliokumbwa na athari za mafuriko na upepo walishatambuliwa hivyo hawatakwenda kinyume na wale waliotambuliwa kikubwa viongozi wa Serikali walishawatembelea na kuwabaini na mahitaji ya kila mmoja, hawataongeza wala kupunguza mlengwa kila mmoja alishawekwa kwenye utaratibu hivyo uadilifu, busara na hekima vitaendelea kutumika.

Hata hivyo mafuriko hayo kwa wilaya ya Muleba yalitokea Octoba 15, mwaka jana na kwa manispaa ya Bukoba yalitokea Oktoba 18, mwaka jana.