Saturday, October 7, 2023
SERIKALI ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA KANISA KATOLIKI - DKT. MPANGO.
Friday, October 6, 2023
REA YATOA MWONGOZO UWEZESHAJI UJENZI VITUO VIDOGO VYA MAFUTA VIJIJINI
Mhandisi Miradi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Kelvin Tarimo, akiwaeleza Wajumbe wa Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Mkoa wa Ruvuma, dhamira ya Serikali kuanzisha mpango wa kuwezesha ujenzi wa vituo vidogo vya bidhaa za mafuta (Dizeli na Petroli) maeneo ya vijijini. Alikuwa akiwasilisha mada katika Baraza hilo Oktoba 5 mwaka huu kwa mwaliko wa Naibu Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Vijana Mkoa wa Ruvuma, Judith Kapinga.
...................................
Veronica Simba na Issa Sabuni – REA
Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imedhamiria kuanzisha mpango wa kuwezesha ujenzi wa vituo vipya vidogo vya gharama nafuu vya bidhaa za mafuta (Dizeli na Petroli) maeneo ya vijijini ili kuondosha njia zisizo salama za uhifadhi wa mafuta hayo.
Hayo yamesemwa na Mhandisi Miradi kutoka REA, Kelvin Tarimo wakati akitoa semina kwa Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Ruvuma, Oktoba 5 mwaka huu kwa mwaliko wa Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga.
Akizungumza na Wajumbe wa Baraza hilo, Mhandisi Tarimo alieleza mambo mbalimbali ikiwemo mwongozo wa ujenzi wa vituo hivyo kwa wale watakaokidhi vigezo na kupata mkopo wa kuvijenga.
Alisema kuwa pamoja na mambo mengine, Mwongozo huo unaainisha bayana vigezo kwa mwombaji wa mkopo ambavyo vimegawanyika katika makundi mawili; kiufundi na kifedha.
Mhandisi Tarimo alivitaja baadhi ya vigezo vya kiufundi kwa mwombaji kuwa ni pamoja na mtu binafsi au kikundi cha wajasiriamali kijijini kilichosajiliwa na Mamlaka husika au Serikali ya kijiji kuwa na kibali cha ujenzi kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA).
Kigezo kingine ni mwombaji kuwasilisha kwa REA barua ya maombi ya mkopo wa ujenzi wa kituo au vituo vipya tu na siyo vinavyohitaji ukarabati au vilivyoanza kujengwa.
Aidha, mwombaji atatakiwa kuwa na barua ya uthibitisho kutoka Halmashauri ya kijiji na Wilaya inayomruhusu kuendesha biashara ya kituo cha mafuta katika eneo aliloomba pamoja na kuwa na namba ya mlipa kodi (TIN Namba) kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Pia, alieleza kuwa mwombaji anatakiwa kuwa na uthibitisho wa umiliki wa ardhi (Hati Miliki ya ardhi au Hati za kimila au uthibitisho wa umiliki wa ardhi) kutoka kwa Halmashauri ya Kijiji au Wilaya.
Kingine ni kibali cha ujenzi kutoka Mamlaka husika pamoja na kujaza fomu ya kuonesha namna anavyokusudia kufanya biashara ya mafuta.
Akieleza zaidi, Mhandisi Tarimo alisema fedha hizo za Mradi zitakazotolewa kama mkopo, ni sehemu ya juhudi za Serikali zinazolenga kuzuia kuhifadhi mafuta ndani ya nyumba kwa kutumia mapipa na chupa za plastiki katika kuuza mafuta ya petroli na dizeli kwa watumiaji wadogo kama vile waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda katika maeneo ya vijijini.
“Hii ni kutokana na kukua na kuongezeka kwa matumizi ya bidhaa hizi katika shughuli za maendeleo maeneo ya vijijini,” alisema.
Kiasi cha mkopo ni shilingi milioni 75 na riba yake ni asilimia tano ilhali marejesho yake ni hadi kipindi cha miaka saba.
Mhandisi Tarimo ametoa hamasa kwa wananchi wote wenye nia kutembelea tovuti ya Wakala wa Nishati Vijijini ambayo ni www.rea.go.tz ili kusoma Mwongozo kamili wa utoaji na usimamizi wa mkopo wa uwezeshaji wa ujenzi na uendeshaji wa vituo vidogo vya bidhaa za mafuta (petroli na dizeli) vijijini.
WATENDAJI WIZARA YA MADINI WATAKIWA KUPANGA MIKAKATI KUONGEZA BAJETI YA WIZARA
Dar es Salaam
Katibu Mkuu Wizara ya Madini Kheri Mahimbali amewataka Watendaji wa Wizara na Taasisi kujipanga kimkakati kwa kubuni miradi yenye tija kwenye Sekta ya Madini itakayowezesha kuongeza Bajeti ya Wizara na kuhakikisha inakwenda sambamba na Vipaumbele vya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2023/24, Dira ya 2030 Madini ni Maisha na Utajiri pamoja na Vipaumbele vya Taifa.
Ametoa rai hiyo leo Oktoba 6, 2023, wakati wa kikao chake na baadhi ya Watendaji hao wa Wizara na Wakuu wa Taasisi za Wizara, ambacho pia kimehusisha watendaji wanaohusika na masuala ya Mipango, Fedha na Rasilimaliwatu kilicholenga kujadili na kujipanga kutekeleza maelekezo, vipaumbele vya Wizara, majukumu, mipango na program mbalimbali ambazo zilijadiliwa wakati wa vikao vya Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde alivyofanya na taasisi zote chini ya Wizara baada ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Waziri wa Madini kwa lengo la kufahamiana, kujengeana uelewa na kuweka mikakati ili kuongeza tija kwenye Sekta ya Madini
Aidha, katika kikao hicho, watendaji hao wamepata wasaa wa kufahamishwa kuhusu namna ya kuandaa mipango na miradi ya kisekta yenye tija kwa taifa kwa kuhakikisha inakwenda sambamba na vipaumbele vilivyopangwa na Wizara na vile vya kitaifa.
Akizungumza katika kikao hicho, Mchumi Mwandamizi kutoka Tume ya Taifa ya Mipango Khalid Shekimweli amesisitiza kuwa miradi na mipango inayopangwa na sekta ni vema ikazingatia maeneo makuu ya msingi ambayo ni pamoja na kuzingatia masuala yanayohusu huduma muhimu za kijamii, yanayokusudia kuondoa umaskini pamoja na kukuza uchumi.
Awali, Mkurugenzi wa Sera na Mipango Wizara ya Madini Bw. Augustino Olal ameeleza kuwa katika Mwaka wa Fedha wizara imepangiwa bajeti ya Shilingi Bilioni 89.3 ambayo imelenga kutekeleza vipaumbele Sita vya Wizara na kuvitaja kuwa ni pamoja na kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli, kuongeza Mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa; kuendeleza Madini Muhimu na Madini Mkakati; Kuwaendeleza na kusogezaHuduma za Ugani kwa Wachimbaji wadogo; kuhamasisha shughuli za Uongezaji thamani Madini na kuhamasisha uwekezaji na Biashara katika sekta ya Madini na Uanzishwaji wa Minada na Maoneshi ya Madini ya Vito.
Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri
Thursday, October 5, 2023
MAKAMU WA RAIS AZITAKA NGO's KUCHUNGA MAADILI NA TAMADUNI ZA KITANZANIA.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa mashirika yasiyo ya kiserikali nchini (NGO’s) kuwajibika kutunza na kulinda maadili kwa kuheshimu mila, desturi na tamaduni za kitanzania wakati wa utekelezaji wa programu mbalimbali.
Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifunga Jukwaa la Tatu la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) llililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete mkoani Dodoma. Aidha amewataka kuzingatia sheria za nchi na kufuata miongozo mbalimbali inayoratibu shughuli za mashirika hayo.
Makamu wa Rais ametoa rai kwa NGO’s kuhakikisha hazitumiki kuharibu maadili ya Tanzania kwa kutekeleza ajenda binafsi zisizofaa. Ametoa wito kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Ustawi na Maendeleo ya Jamii kufanya uchambuzi makini wa mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na kuishauri serikali ipasavyo juu mwenendo na ufanisi wa mashirika hayo.
Pia Makamu wa Rais amesema suala la mabadiliko ya tabianchi linapaswa kuchukuliwa kwa umuhimu mkubwa na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwani Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoathiriwa na mabadiliko ya tabianchi na hali ya hewa isiyotabirika.
Amesema serikali Serikali ingependa kuona ushiriki zaidi wa NGOs katika utoaji elimu na hamasa kuhusu uhifadhi wa mazingira, udhibiti wa majanga na maisha endelevu, utunzaji wa misitu na uoto wa asili na kuchangia katika utengenezaji au uboreshaji wa sera mbalimbali.
Aidha amesema mashirika hayo yana nafasi ya kubuni programu muhimu kama ukusanyaji na urejelezaji taka, biashara ya kaboni, uanzishwaji na utunzaji wa vitalu vya miti na usambazaji wa miche pamoja na usafi wa mazingira katika maeneo maalum.
Halikadhalika Makamu wa Rais amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ili Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yaweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi wa hali ya juu zaidi.
Ametaja miongoni mwa hatua ambazo Serikali imechukua katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza utambuzi wa mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, ni pamoja na kuandaliwa kwa Mwongozo wa Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Tanzania Bara (2020), Mfumo wa Kielektroniki wa Usajili na Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (2020), Kitabu cha Mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika Maendeleo ya Taifa (2020/2021/2022), pamoja na Mkakati wa Kitaifa wa Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (2022/23 – 2026/27).
Hatua nyingine ni uanzishwaji wa madawati ya uratibu wa mashirika yasiyo ya kiserikali katika Wizara za Kisekta na Mfumo wa Ramani ya Kidigitali ya Utambuzi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ambao imezinduliwa.
Kwa Upande wake Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Doroth Gwajima amesema NGO’s zimekuwa zikiunga mkono jitihada za serikali kupitia utekelezaji wa miradi na afua mbalimbali ikiwemo miradi ya afya, elimu, mazingira, kilimo , maji, utawala bora, nishati na uwezaji wa jamii.
Ameongeza kwamba utekelezaji wa miradi hiyo umechangia kuboresha utoaji huduma, kuzalisha ajira, kuongeza mapato ya serikali na ukuaji wa uchumi kwa ujumla. Dkt. Gwajima amesema Wizara itaendelea kuboresha mazingira wezeshi kwa NGO’s ili ziweze kuisadia jamii kwa kuzingatia mipango, mikakati na vipaumbele vya taifa.
Awali Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) Dkt. Liliani Badi ameiomba serikali kushughulikia changamoto mbalimbali zinazokabili Mashirika yasiyo ya kiserikali ikiwemo upatikanaji wa vibali kwaajili ya utekelezaji wamiradi na afua mbalimbali katika mikoa na halmashauri mbalimbali, vigezo vya upatikanaji wa misamaha ya kodi pamoja changamoto ya mashirika yasiyo ya kiserikali ya kimataifa kutozingatia utekelezaji wa takwa la kisheria la kuyajengea uwezo mashirika yasiyo ya kiserikali ya ndani ya nchi.
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
05 Oktoba 2023
Dodoma.
CHONGOLO: MAWAZIRI 3 KUHUSIKA FIDIA MRADI WA UMEME TABORA - KATAVI
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema atakutana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Nishati na Wizara ya Fedha, kwa ajili ya kutatua changamoto ya malipo ya fidia ya wananchi ambao ardhi yao imechukuliwa kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Ujenzi wa Msongo wa Umeme kutoka Tabora hadi Katavi.
Katibu Mkuu Ndugu Chongolo amesema hayo leo Oktoba 5, 2023, wakati akizungumza na wananchi wa Inyonga, wilayani Mlele, Mkoa wa Katavi, kuhusu mradi huo wa msongo wa umeme ambao utauwezesha mkoa huo sasa kuunganishwa katika gridi ya taifa, hivyo kumaliza kabisa changamoto ya nishati hiyo katika maeneo hayo.
“Nikirudi Dar es Salaam nitakaa na pande zote zinazohusiana na ulipaji fidia wakiwemo Wizara ya Nishati, Wizara ya Fedha na Wizara ya Ardhi pamoja na wadau wengine ili watuambie wanaendaje na nini kifanyike kusukuma suala la fidia ili walipwe haraka.
Ndugu Chongolo amewahikishia wananchi wa Mkoa wa Katavi kuwa katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020 - 2025, kuunganisha Mkoa wa Katavi kwenye gridi ya taifa, ni mojawapo ya vipaumbele vya muhimu kwa Serikali.
Chongolo ambaye yupo katika mkoa huo kwa ziara ya kuhamaisha uhai wa Chama, kukagua utekelezaji wa Ilani pamoja na kusikiliza changamoto za wananchi na kuzitafutia majawabu, amesema Serikali tayari imeshatenga fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo.
“Na huu mradi sio mradi tu bali ni mradi wenye lengo mahususi la kutafuta majawabu kwa wananchi wa Katavi lakini pia kuinua shughuli za uchumi wao na wakazi wa jirani kama Sikonge na maeneo mengine.
“Mmeeleza vizuri uwezo wa kituo hapa ni megawati 1.4 na mahitaji sasa hivi yaweza kuwa yamefika megawati mbili lakini ukipeleka Majimoto kuna viwanda zaidi ya 20 au 30 vya mpunga vile viwanda vyote vinahitaji umeme.
“Ukipiga hesabu utakuta Majimoto nao wanahitaji megawati mbili mpaka tatu, kwa hiyo zinahitajika karibia megawati tano kwa wilaya ya Mlele. Ukienda Mpanda shughuli zao zinaunganisha mpaka Kalema na kalema tuna bandari." Amesema.
Ameongeza ili kubadilisha kwenda kwenye uhalisia ni kutekeleza huo mradi huku akitumia nafasi hiyo kuzungumzia suala la fidia kwa watakaopitisha mradi huo.
“Nikirudi Dar es Salaam nitakaa na pande zote zinazohusiana na ulipaji fidia wakiwemo Wizara ya Nishati,Wizara ya Fedha na Wizara ya Ardhi pamoja na wadau wengine ili watuambie wanaendaje na nini kifanyike kusukuma suala la fidia ili walipwe haraka.
Ameongeza fidia ikishalipwa itabaki kusubiri ujenzi wa laini ya umeme na kushauri watekelezaji wa mradi huo kuanzia shughuli za za awali za utekelezaji wa mradi huo kwa kuandaa mazingira.
“Wakati huu ungekuwa wakati muafaka wa kuanza kujenga nguzo kwenye maeneo yale yenye majimaji ili wakati wa masika ujenzi usimame maeneo hayo.Tunaomba mradi huu uangaliwe kwa uzito wake.
“Tukifungua na kuleta umeme kwa wananchi wa Katavi naamini mchango wao katika kukuza uchumi wa nchi hii utakwenda juu kwani kwa sasa hata ujenzi wa viwanda vikiwemo vya kuchakata tumbaku na migodi ya madini, umesimama kwasababu ya changamoto ya umeme,” amesema Ndugu Chongolo.
RAIS SAMIA AMEIBEBA KWA DHATI AJENDA YA MATUMIZI NISHATI MBADALA – NAIBU WAZIRI KAPINGA
Lilian Lundo, Veronica Simba na Zuena Msuya - Songea
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameibeba kwa dhati ajenda ya matumizi ya nishati mbadala kutokana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi.
Mhe. Kapinga amesema hayo leo Oktoba 5, 2023 wakati wa Baraza Maalum la Jumuiya ya Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Ruvuma, sanjari na ugawaji wa majiko/mitungi ya gesi yaliyotolewa na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
“Ninyi nyote mnafahamu ajenda ya Mhe. Rais kuhusiana na umuhimu wa nishati mbadala, tunafahamu changamoto ya mabadiliko ya tabianchi na changamoto za mazingira kwa ujumla. Hii ni ajenda ambayo Mhe. Rais ameibeba kwa dhati kabisa kuhakikisha tunaanza mchakato wa kuelimisha Watanzania ili kuondokana na nishati ambazo sio rafiki kwa mazingira, na kutumia zilizo rafiki kwa mazingira,” amesema Mhe. Kapinga.
Naibu Waziri Kapinga ambaye pia ni Mbunge wa Vijana Mkoa wa Ruvuma amewataka vijana kushirikiana na wanawake, wazee na makundi mengine katika kuhakikisha wanapunguza changamoto za kimazingira kwa matumizi ya nishati mbadala.
“Wengi wanadhani ajenda hii ya nishati mbadala ni kwa ajili ya akina mama tu, lakini wote tunafahamu nguvu na mchango wa vijana kwenye masuala ya mabadiliko chanya. Kwa hiyo ajenda hii ni lazima twende nayo pamoja wanawake, vijana, wazee na kila kundi kwenye jamii. Ndiyo maana nikaona busara kushirikisha Baraza la Mkoa kwa sababu ninyi ndio viongozi kwenye Wilaya zenu,” amesema Mhe. Kapinga.
Akifafanua, amesema kuwa ajenda ya matumizi ya nishati mbadala ni ya Serikali ya Awamu ya Sita na inatakiwa kuungwa mkono na wananchi wote ili kuweza kuboresha mazingira na kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi yanayoendelea hivi sasa duniani kote.
Kapinga amesema ni wakati wa vijana kusaidia katika anjenda mbalimbali zenye manufaa ya taifa na kwamba ajenda ya nishati mbadala ikibebwa na vijana inaweza kwenda kwa kasi katika kusaidia kupunguza changamoto za uharibifu wa mazingira unaofanywa na jamii.
Aidha, ameongeza kuwa wakati huu ambapo REA wanaendelea kutoa elimu ya matumizi ya nishati mbadala, Mhe. Rais ametoa mitungi ya gesi kwa Wabunge wote ili iende kwenye maeneo yote, na majimbo yote ili kuhamasisha umuhimu wa nishati mbadala.
Awali, akiwasilisha Mada kuhusu nishati safi ya kupikia, Mhandisi Kelvin Tarimo kutoka REA amesema Wakala hiyo inaendeshwa kwa Mipango Mikuu mitatu ambayo ni Mpango wa Sera ya Taifa wa Upelekaji Nishati Vijijini (Rural Energy Master Plan), Mpango wa usambazaji wa huduma ya umeme vijijini (Rural Electrification Master Plan) pamoja na Mpango wa Nishati safi za kupikia.
Kuhusu Mpango wa nishati safi ya kupikia, Mhandisi Tarimo amesema umelenga kuhamasisha matumizi ya nishati iliyo salama kwa mtumiaji na kwa mazingira, ubora, upatikanaji wake, gharama nafuu, rafiki kwa mazingira na iliyo endelevu.
Akizungumzia aina za nishati za kupikia na kiwango cha matumizi yake kwa hapa nchini, Mhandisi Tarimo amebainisha kuwa kuni inaongoza kwa asilimia 63. 5 ikifuatiwa na mkaa asilimia 26.2, gesi oevu asilimia 5.1, umeme asilimia 3 na asilimia 2.2 vyanzo vinginevyo.
Amesema, kutokana na matumizi makubwa ya mkaa na kuni, imechangia uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana na ukataji miti. Pia, amesema athari nyingine ni za kiafya kwa watumiaji wa nishati hizo ambapo vifo zaidi ya 33,000 hutokea kwa mwaka kutokana na kuvuta hewa ya ukaa. Vilevile, kiuchumi amesema matumizi ya nishati zisizo salama yanachelewesha maendeleo ya shughuli za kiuchumi.
Kufuatia hali hiyo, amesema Serikali imeweka mikakati ya makusudi katika kuelimisha na kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala hivyo akatoa wito kwa wananchi wanaopata elimu hiyo kuifikisha kwa wengine.
Amewasihi wananchi kubadili mitazamo hasi dhidi ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwemo imani kwa baadhi ya watu kwamba chakula huwa kitamu zaidi kikipikwa kwa kutumia mkaa au kuni kuliko kikipikwa katika jiko la gesi au umeme.
Mhandisi Tarimo ametoa wito kwa wananchi kuunga mkono kampeni ya Mheshimiwa Rais kuhusu matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia.
Naibu Waziri Kapinga yuko katika ziara ya kazi mkoani Ruvuma kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati pamoja na kuzungumza na wananchi.
NCHI ZA AFRIKA ZATAKIWA KUSHIRIKIANA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO ZA ONGEZEKO LA IDADI YA WATU


































































