Sunday, March 15, 2020

AJALI YA MOTO MOROGORO YAWAJERUHI WAANDISHI WA HABARI

Na Rashid Mtagaluka, Morogoro .

Waandishi wa Habari watatu kutoka vyombo habari tofauti mkoani Morogoro wamejeruhiwa na Moto wakati walipokuwa wakikusanya taarifa za ajali hiyo iliyotokea majira ya saa 8:30 mchana wa leo Machi 14,2020 mjini Morogoro. 


Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Morogoro Kamishina Msaidizi Mwandamizi Gudluck Zerote amesema, chanzo cha tukio hilo hakijafahamika, ingawa Kamanda Zerote alikiri huwenda mrundikano wa mitungi ya gas iliyowekwa kiholela kwenye mojawapo ya chumba kwenye nyumba hiyo ukachangia. 


Kwa mujibu wa Kamanda Zerote, waliojeruhiwa kwenye tukio hilo lililotokea mtaa wa Mzambarauni ulioko kata ya Mafisa ni Hassan Ninga wa Imaan Media, Omar Hussein wa Sahara Media na Salum Yusuf wa Abood Media ambao wamekimbizwa hospital ya Rufaa ya mkoa wa Morogoro. 


"Tumepokea taarifa ya Moto majira ya saa 8:39 mchna wa leo na ilipofika saa 8;45 tulishafika hapa na wakati tukizima moto upande huu kumbe kulikuwa na chumba kimoja kilikuwa kimehifadhiwa mitungi mitano mikubwa ya gas" ,alisema Zerote na kuongeza. 


"Lakini muda mfupi ndipo mitungi hiyo iliyokuwa imehifadhiwa bila kibali na mfanyabiashara ambaye hatujapata jina lake, ikaanza kulipuka mmoja baada ya mwingine, tukaamua kusubiri pembeni maana gas ikishawaka kiasi hicho huwezi kuzima kwa kutumia maji, hivyo tukasubiri ipowe". 


Aidha Kamanda Zerote ametoa wito kwa wananchi kutohifadhi gas zaidi ya ile ya matumizi yao ya kawaida Kama ilivyotokea kwenye nyumba hiyo iliyoharibika vibaya kutokana na watu kuvunja madirisha ili kujinusuru. 


Naye mwenyekiti wa mtaa huo wa Mzambarauni Mohammed Salum amesema tukio hilo licha ya kuwajeruhi waandishi wa Habari watatu, pia limeleta taharuki mtaani hapo kwa baadhi ya wakaazi kukimbia ovyo bila kuchukua tahadhari nankusababisha baadhi yao kuumia. 


Pia kiongozi huyo ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mtaani humo ameishauri Mamlaka husika kupiga marufuku biashara ya gas kufanyika kiholela bla kuzongatia sheria, kanuni na taratibu ili kuepusha madhara kwa jamii. 


Kwa upande wake diwani wa kata ya Mafisa kulikotokea tukionhilo Bwana Alli Rashid Kalungwana amesema pamoja na tukio hilo kusababisha maafa kwa tasnia ya habari, lakini hakukuwa na madhara zaidi kwa wananchi wa kata yake. 


Nao baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo wamesema iko haja kwa serikali na vyombo vyake vya dola kuongeza juhudi ya kutoa elimu ya matumizi sahihi ya nishati hii mbadala kwa lengo la kuwasaidia wananchi kufahamu jinsi ha kujikinga na ajali za Moto. 


Rajab Farijala Rajab ambaye ni miongoni mwa wananchi wa kata ya Mafisa Manispaa ya Morogoro ameiomba serikali kuangalia upya sheria inatoruhusu wafanyabiashara wa gas kuhifadhi mitungi mingi na mikubwa kwenye nyumba moja inayoishi watu, ili kuokoa nguvu kazi kubwa ya Taifa

MACHOKODO, MAKAMO MWENYEKITI COREFA AZIKWA BAGAMOYO.

 Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA), Hassan Hasanoo, (kushoto mwenye kapelo) akipokea jeneza liliobeba Mwili wa aliyekuwa Makamo Mwenyekiti wa Chama hicho, Marehemu Shabani Omari Kangale (Machokodo) aliyefariki ghafla kwa ugonjwa wa Pumu.
............................................


Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Shabani Omari Kangale (Macho kodo) amefariki dunia akiwa nyumbani kwake huko Bagamoyo usiku wa tarehe 13 Machi 2020.


Taarifa zilizotolewa na familia ya marehemu zilisema marehemu alikuwa akisumbuliwa na pumu na kwamba sababu ya kifo chake ni pumu iliyombana kwa kasi.


Akizungumza na BAGAMOYO KWANZA BLOG Mwenyekiti wa Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Hassan Hasanoo alisema kifo cha Kangale ni pigo kubwa kwa COREFA na wana michezo wote mkoa wa Pwani.


Alisema Kangale alikuwa sio ni Makamo Mwenyekiti bali alikuwa ni zaidi ya Makamo Mwenyekiti kwa umahiri wake katika uongozi, busara na moyo wa kujitolea katika mambo mbalimbali yanayohusu chama cha mpira Pwani.


Watu mbalimbali waliohudhuria katika mazishi hayo wamemzungumzia marehemu Kangale kuwa ni mtu mwenye kupenda ushirikiano katika mambo mbalimbali ya kijamii jambo ambalo litafanya aendelee kukumbukwa.


Aidha, viongozi waliowakilisha makundi yao wamesema Marehemu Shabani Kangale (Machokodo) ni mtu wa kipekee katika utendaji wake wa kazi na namna anavyoweza kushughulikia matatizo.


Mashjabiki wa mpira wa miguu Bagamoyo na Mkoa wa Pwani kwa ujumla wamesema Chama cha Mpira wa miguu mkoa wa Pwani kimepata pigo kwa kuondokewa na kiongozi mchapa kazi, mpenda watu, na mwepesi wa kushughulikia matatizo.


Marehemu Shabani Omari Kangale (Machokodo) amezaliwa mwaka 1957 na kupata elimu yake ya usimamizi wa fedha, katika chuo cha IFM mwaka 1980 na kwamba katika uhai wake alifanya kazi sehemu mbalimbali ikiwemo TAMCO KIBAHA, KIWANDA CHA URAFIKI, TIPA, SCANIA, KAGERA SUKARI, KJ MOTORS, NASSACO, STEEL CAST NA MUWA.


Aidha, marehemu Kangale alihamia Bagamoyo mwaka 2003 na kuendelea na biashara zake binafsi.


Akiwa Bagamoyo aliwahi kuwa mweka hazina wa Chama cha mpira wa Miguu wilaya ya Bagamoyo (BFA) mwaka 2008 mpaka 2012.


Alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wilaya ya Bagamoyo (BFA) Mwaka 2012 mpaka 2016.
Kuanzia 2016 alikuwa Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa miguu mkoa wa Pwani (COREFA) mpaka umauti unamkuta.


Marehemu ameacha wake wawili, watoto sita na wajukuu watano
Mwenyezimungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi Aamiyn.
Watu mbalimbali waliohudhuria mazishi ya aliykuwa Makamo Mwenyekiti wa Mpira wa miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Shabani Omari Kangale (Machokodo) wakiomba dua wakati wa mazishi yaliyofanyika nyumbani kwake Majengo Bagamoyo mjini hapo jana Machi 14, 2020.
 Swali ya jeneza iliyoswaliwa kwaajili ya marehemu Shabani Kangale (Machokodo) Nyumbani kwake Majengo mjini Bagamoyo Machi 14, 2020.
 
Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA), Hassan Hasanoo, (kushoto mwenye kapelo) akiwa kwenye msiba wa aliyekuwa Makamo Mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Pwani, Shabani Kangale, katikati ni Mwenyekiti wa Mamlaka ya mji mdogo wa Kisarawe, Ally Mkomwa.
 
 Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA), Hassan Hasanoo, (kulia) akiwa eneo la makaburi Mwanakalenge Bagamoyo mahali ambapo amezikwa Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Shabani Omari Kangale (Machokodo).
Wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Bagamoyo na nje ya Bagamoyo, wakisindikiza mwili wa marehemu Shabani Omari Kangale (Machokodo) kuelekea makaburi ya Mwanakalenge Bagamoyo mjini, Machi 14, 2020.