Thursday, April 11, 2019

RAIS MAGUFULI AZUNGUMZA NA WANANCHI WA MAFINGA AKIWA NJIANI KUELEKEA MKOANI IRINGA

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wananchi wa Mafinga mara baada ya kuwasili wakati akitokea Makambako mkoani Njombe. 

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. John Pombe Magufuli akimsikiliza kijana Baraka Mwakipesile (Anko Magu) wa Mafinga ambaye anaigiza sauti ya Rais Dkt. Magufuli mara baada ya kupewa nafasi ya kuzungumza.

 Umati wa Wananchi wa Mafinga  wakimsikiliza  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli wakati alipokuwa akizungumza nao.

 Baraka Mwakipesile (Anko Magu) Kijana anayeigiza sauti ya Rais Dkt. Magufuli akipiga makofi wakati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa akihutubia. Picha na IKULU.

WATUMISHI BAGAMOYO WATAKIWA KUZINGATIA MAADILI YA UTUMISHI

Image may contain: 2 people, people sitting
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Fatuma Latu, amefanya kikao kazi maalumu na Watumishi wa Halmashauri kuwaelekeza na kuwakumbusha maagizo mbalimbali ya Serikali katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.


Watumishi hao wapatao 250 wa makao makuu na watendaji wa Kata waliohudhuria mkutano huo walikumbushwa juu ya uadilifu katika utumishi wa Umma, weledi, kufuata utaratibu wakati wa kutekeleza majukumu yao, kuzingatia lishe na usafi wa kila mtumishi binafsi, mada zilizowasilishwa kwa Watumishi hao na Mkurugenzi mtendaji akisaidiana na Wakuu wa Idara wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo


Akizungumza na Watumishi hao Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Fatuma Latu amewasisitiza Watumishi hao kuzingatia utunzaji wa Afya zao kwa kula vizuri, kwani mtumishi anayekula vizuri na mwenye Afya njema na uwezo mkubwa zaidi wa kusikiliza, kuyaelewa na kuyafanyia kazi maagizo mbalimbali ya Serikali.


"Serikali inafanya kazi kwa vipaumbele, na katika masuala ya Watumishi, inasisitiza Watumishi wa Umma kuhakikisha wanazingatia masuala ya lishe, kwa kula mlo kamili kila siku ili kuimarisha Afya zao na kujiongezea uwezo wa kufanya kazi kwa bidii na weledi kwani Chakula kina uwezo wa kumpa mtu nguvu, Afya na wakati mwingine Chakula ni dawa"

"Nawasihi sana hakikisheni mnatenga muda wa kula chakula mnapokuwa katika kutimiza majukumu yenu ya kila siku, mishahara mnayopokea, muitumie pia kwa ajili ya kupata chakula bora ninyi na familia zenu, sio mnatumia mshahara wote kukopa katika taasisi mbalimbali za fedha na kusahau kabisa kama kuna umuhimu wa kujihakikishia kupata mlo wa kila siku kupitia mshahara huo huo" Alisema Bi. Fatuma Latu


Watumishi walioshiriki kikao hicho pia walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuwasilisha kero wanazokumbana nazo wakati wakitimiza majukumu yao ya kila siku ambapo baadhi yao walizungumzia kero ya kutopandishwa madaraja kwa muda mrefu, malipo ya stahili mbalimbali na changamoto ya upungufu wa watumishi, na mambo hayo yote yalitolewa ufafanuzi wa kina na Mkurugenzi Mtendaji pamoja na Wakuu wa Idara.


Mkurugenzi Mtendaji ameanzisha utaratibu wa kukutana na Watumishi wa Halmashauri mara moja kwa Mwezi, kwa ajili ya kuwapa maelekezo mbalimbali ya Serikali na kusikiliza kero za watumishi hao, lengo likiwa ni kuongeza ufanisi katika utendaji kazi za Halmashauri.




Image may contain: 6 people, people sitting and indoor
Image may contain: 11 people, people smiling, people sitting
 Sehemu ya Watumishi wa Halmashauri ya Bagamoyo wakiwa kwenye kikao kazi kilichoitishwa na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Fatuma Omari Latu.

WATOTO 58,048 KUPEWA TIBA KINGA CHALINZE

Image may contain: 3 people, people standing and indoor
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Chalinze Wilayani Bagamoyo Bi Amina Kiwanuka amezindua rasmi zoezi la utoaji tiba kinga ya kichocho na minyoo tumbo kwa watoto 58,048 wenye miaka 5-14 walioandikishwa shule na wasioandikishwa,uzinduzi huo umefanyika leo katika shule ya msingi Lugoba kiwilaya.


Katika hotuba yake ya uzinduzi wa zoezi la utoaji tiba kinga ya kichocho na minyoo tumbo,Mkurugenzi Kiwanuka amewaasa wanafunzi na walimu kuwa walimu kwa jamii kwa kutoa Elimu ya matumizi ya maji safi na salama ili kujiepusha na kichocho na minyoo tumbo na kuwataka wanafunzi waache kuoga kwenye madimbwi ya Maji ambayo kimsingi huwa ndio chanzo cha Magonjwa kama kichocho.

 
Kwa mujibu wa Mratibu Wa Magonjwa yaliyokuwa hayakupewi kipaumbele, Dkt Waziri Mkuwili alifafanua kuwa zoezi hili linafanyika siku ya leo katika shule zote katika Halmashauri ya Chalinze kwa kuwapa tiba kinga ya kichocho na minyoo tumbo jumla ya watoto 58,048 wenye umri wa miaka 5-14 katika halmashauri ya Chalinze.


Aliendelea kufafanua kuwa zoezi hili ni zoezi la kitaifa ambalo linafanyika kitaifa kwa misingi ya kupambana na Magonjwa ambayo hayakupewa kipaumbele na hatimaye kuathiri Afya za watoto katika jamii.


Hata hivyo Dkt Mkuwili alifafanua kuhusu ubora wa dawa hizo na kuwataka wananchi wasisite kuwaleta watoto wao katika vituo vya kutolea dawa na kuongezea kuwa dawa hizi hazina madhara kwa watoto kinachotakiwa ni kuhakikisha watoto wamekula chakula ndiyo waweze kumeza dawa hizo.


Naye Mganga Mkuu Wa Wilaya Dkt Rahim Hangai aliwataka wananchi wa Chalinze kuwaleta watoto katika vituo vya dawa kwani leo ni siku rasmi kwa ajili ya zoezi la kunywesha dawa watoto wote katika Halmashauri ya Chalinze wenye umri wa miaka 5-14