Saturday, May 26, 2018

KAIMU DC KIBAHA, MAJID MWANGA, ATAKA VIJANA JKT KULINDA AFYA ZAO.


Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo akikagua gwaride la vijana wa kujitolea Operesheni Merelani waliopata mafunzo ya awali ya kijeshi sherehe hizo zilifanyika uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha katika Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
 
Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali ya kijeshi kwa vijana wa kujitolea Operesheni Merelani uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha katika Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
.............................................
Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha Alhaj Majid Mwanga amewataka vijana wanaomaliza mafunzo ya JKT kutunza afya zao ili waweze kushiriki katika shughuli za kujenga Taifa kikamilifu.

Majidi aliyasema hayo wakati wa kufunga  mafunzo ya awali ya kijeshi kwa vijana wa kujitolea operesheni Mererani yaliyofanyika katika kikosi cha jeshi 832 KJ-RUVU JKT.

Alisema kazi ya jeshi ni kazi inayohitai utayari, ari na afya njema hivyo askari ili aweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo anatakiwa awe na afya iliyo imarika.

Aliongeza kuwa katika U tatu walizojifunza yaani Uadilifu, Uzalendo na Uaminifu wasisahau kuwa ni lazima kuwa na afya nzuri itakayomfanya askari kuwa mchangamfu na mwenye nguvu wa kupambana na mazingira ya aina yoyote.

Alisema kutokana na umri wa vijana hao, vipo vishawishi vingi katika jamii vinavyoweza kupelekea kufanya mambo yatakayosababisha kudhoofika kwa afya zao hivyo ni lazima wachukue tahadhari.

Alifafanua kuwa hali ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI nchini hasa katika wilaya za Kibaha na Bagamoyo inatisha hivyo vijana wa JKT wanapaswa kulitambua hilo na kujua namna ya kukabiliana na hali hiyo ili kujilinda na maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

Katika hatua nyingine aliwataka kuishi maisha ya kiaskari kwa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu kama walivyoapa na kuongeza kuwa kiapo ni kifungo.

Alisema haitarajiwi askari aliyepata mafunzo na kula kiapo cha utii afanye vitendo vinavyokwenda kinyume na kiapo chake kwani yeye anapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii.

Kwa upande wake Mkuu JKT nchini Meja Jenarali Martini Busungu katika hutuba iliyosomwa kwa niaba yake na Kaimu Mkuu wa utawala JKT Makao Makuu, Kanali Hawa Kodi aliwataka vijana hao waliopata mafunzo ya JKT kuwa mfano wa kuigwa katika jamii na ipatikane tofauti kati yao na wale ambao hawakupata mafunzo hayo.

Alisema mafunzo hayo yatumike vizuri katika jamii na wala yasiwe kwaajili ya kuwapiga raia wema na badala yake wawe ndio walinzi wa raia na kuhakikisha wanapinga kwa namna yoyote vitendo vya kihalifu.

Aliongeza kwa kuwataka vijana hao kushirikiana na mamlaka zinazohusika ili kuwafichua waovu, wasaliti na wale wote wasioitakia mema nchi ya Tanzania.

Aidha, alisema katika kipindi hiki ambacho maadili ya kitanzania yameporomoka kwa kuiga tamaduni za watu wa kigeni, Jeshi la Kujenga Taifa lina mchango mkubwa katika kuhakikisha vijana wanakuwa katika maadili mema ya kitanzania ili kulinda heshima ya nchi yetu katika uso wa dunia.
Alisema tamaduni za kigeni nyingi zina athari kubwa katika ustawi wa maadili ya vijana hapa nchini hivyo ni wajibu wa watanzania wote kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Jeshi la Kujenga Taifa katika malezzi ya vijana ili kupata wazalendo wa nchi yetu.

Awali akisoma taarifa ya vijana hao, Mkuu wa Kikosi cha jeshi cha 832 KJ-RUVU JKT, Kanali Charles Mbuge alisema vijana hao wamejifunza mambo mbalimbali ya kijeshi ikiwa ni pamoja na uvumilivu, nidhamu, na kujituma wanapopewa majukumu.

Aliongeza kuwa katika mafunzo hayo waliweza kujifunza ufugaji wa aina mbalimbali, uandaaji wa bustani za mbogamboga pamoja na kuibua vipai vya sanaa na Michezo na taaluma za aina mbalimbali..

Kanali Mbuge aliwataka vijana hao wakawe askari bora na wawe tayari kutumikia nchi yao ikiwa ni pamoja na kulinda rasilimali za nchi pindi watakapohitaika kufanya hivyo.

Aidha, alisema wakufunzi wa vijana hao wametimiza majukumu yao ya kuwajenga katika tabia njema na uzalendo na kwamba  kwa sasa wamebadilika tabia zao na kuongeza maarifa juu ya ufahamu wa mambo mbalimbali.

Wakisoma risala mbele ya mgeni rasmi, vijana hao wahitimu wa mafunzo ya awali ya kijeshi wa Operesheni Meralani, walisema katika kipindi chote cha mafunzo yao waliweza kupata taaluma ya stadi za maisha na stadi za kazi kwa kujifunza kwa nadharia na vitendo kazi za mikono na ujasiliamali ikiwemo ufugaji wa kuku, Bata, Samaki, na kilimo cha bustani za mbogamboga.

Walisema elimu hiyo waliyoipata itawasaidia kujikwamua kimaisha kwa kujiongezea kipato na kuondokana na umasikini.

Jumla ya vijana 1408 wamehitimu mafunzo yao ya awali ya kijeshi katika kikosi cha jeshi 832 KJ-Ruvu JKT, ambao miongoni mwao wavulana ni 960 na wasichana 448.
 
 Kaimu Mkuu wa utawala JKT Makao Makuu, Kanali Hawa Kodi akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali ya kijeshi kwa vijana wa kujitolea Operesheni Merelani uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha katika Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
 Mkuu wa Kikosi cha jeshi 832 KJ-RUVU JKT, Kanali Charles Mbuge akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali kwa vijana wa kujitolea Operesheni Merelani uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha katika Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
 Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo akipata utambulisho wa vikundi tayari kwa maonyesho mbalimbali ikiwemo gwaride la mwendo wa haraka na mwendo pole kupita mbele yake.
Picha juu ni gwaride la mwendo pole na picha chini ni gwaride la mwendo wa haraka Vijana wahitimu wa mafunzo ya awali ya kijeshi wakiongozwa na wakufunzi wao wakipita mbele ya mgeni rasmi, katika uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
Wakufunzi na maafisa wa ngazi mbalimbali wa jeshi wakishuhudia vijana wao katika kufunga mafunzo ya awali ya kijeshi yaliyofanyika
uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
 
Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo (kushoto) akizungumza jambo na  Mkuu wa Kikosi cha jeshi 832 KJ-RUVU JKT, Kanali Charles Mbuge (kulia).
 
Meza kuu, katikati ni Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, kushoto ni  Kaimu Mkuu wa utawala JKT Makao Makuu, Kanali Hawa Kodi ambae alimuwakilisha Mkuu wa JKT nchini Meja Jenarali Martini Busungu katika shughuli hiyo na kulia ni Mkuu wa Kikosi cha jeshi 832 KJ-RUVU JKT, Kanali Charles Mbuge.
Wageni waalikwa, wazazi wa vijana hao, ndugu jamaa na marafiki wakishuhudia sherehe hizo za kufunga mafunzo ya awali kwa vijana wa kujitolea Operesheni Merelani uwanja wa mabatini huko Mlandizi wilayani Kibaha katika Kikosi cha Jeshi 832 KJ-RUVU JKT.
  Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Alhaj Majid Mwanga, ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, akiangalia bwawa la samaki alipokuwa akikagua miradi mbalimbali ya ujasiliamali inayotekelezwa na kikosi cha jeshi cha 832 KJ- RUVU JKT. 

Picha juu na chini ni Vijana wahitimu wa mafunzo ya awali ya kijeshi katika Kikosi cha jeshi 832 KJ- RUVU JKT wakionyesha mazao wanayolima katika kikosi hicho ikiwa ni sehemu ya mafunzo waliyopatiwa.

Thursday, May 24, 2018

RC NDIKILO ATAKA WANANCHI WALINDE MISITU.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amewataka wananchi mkoani humo kuacha kuvamia maeneo hifadhi za misitu ili kuruhusu uoto wa asili kwa manufaa ya taifa.

Mhandisi Ndikilo ameyasema hayo alipokuwa katika ziara ya kukagua Hifadhi ya Msitu wa Zigua ambayo kwa muda mrefu ilikuwa imevamiwa.

Akizungumza mara baada ya kujionea hali ilivyo kwa sasa katika msitu huo Mkuu huyo wa Mkoa alisema baada ya kuwaondoa wavamizi katika hifadhi za misitu za mkoa wa Pwani hali za misitu hiyo imerejea kama kawaida na kwamba sasa misitu hiyo imeanza kupendeza.

Alisema kufautia kurudi kwa hali ya kawaida katika Misitu hiyo Mkuu huyo wa Mkoa alisema wananchi mkoani humo wanapaswa kuwa walinzi wa misitu hiyo na kwamba waache kuvamia na kufanya shughuli za kibanadamu.

Aliitaja misitu hiyo iliyopo Mkoa wa Pwani kuwa ni Msitu wa Zigua, Msitu wa kazi mzumbwi, na Msitu wa Ruvu kusini

Akizungumzia umuhimu wa Msitu wa Zigua alisema msitu huo ni mapitio ya wanyama kutoka mbuga ya wanyama Saadani kuelekea Mikumi na  Mbuga Selou

Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa, Msitu huo ndio unaweza kuhifadhi mai ya mto wami ambayo hutumika kwa matumizi mbalimbali ya binadamu na wanyama katika hifadhi ya wami mbiki iliyopo wilayani Bagamoyo mkoa wa Pwani.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kanda ya mashariki Caroline Malundo alisema kwa sasa Msitu huo umerejea katika hali yake ya kawaida na kwamba hata wanyama waliokuwa wametoweka wameanza kurejea.

Alisema oparesheni ya kuwaondoa wavamizi katika msitu huo iliyofanywa kwa kushirikiana na kamati za ulinzi na usalama za wilaya tatu ambazo ni Handeni, Bagamoyo na Kilindi ilifanikiwa kwa kiasi kikubwa na kwamba mpaka sasa hakuna wavamizi ndani ya msitu huo.
 

Wednesday, May 23, 2018

WANAWAKE BAGAMOYO WAPEWA ELIMU YA UJASILIAMALI.


Wanawake wa Bagamoyo wamepewa elimu ya ujasiliamali ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Semina hiyo ambayo imeandaliwa na ... ililenga kuwajengea uwezo katika shughuli zao katika uzalishaji wa bidha mbalimbali.

Aidha, kinamama hao wametakiwa kuzalisha bidhaa zenye ubora ili kukabiliana na ushindani wa soko.

Muwezeshai wa semina hiyo alisema ni lazima kina mama waiamini kile wanachofanya kwani kuiamini ni njia moja wapo ya kufikia malengo.

Kwa upande wao wanawake hao wajasiliamali wilayani Bagamoyo wamesema wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika kuzalisha bidhaa zao na kudhindwa kufikia malengo wanayojiwekea.

Walisema miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na kukosa elimu ya ujasiliamali hali inayopelekea kinamama wengi kufanya kazi zao chini ya kiwango.

Waliongeza kwa kusema kuwa upatikanaji wa malighafi ni tatizo linalowakwamisha wengi kwakuwa malighafi zimekuwa zikiuzwa kwa bei ya juu au kukosekana kabisa na hatimae mjasiliamali anakata tamaa ya kuendelea na uzalishaji.

Kupitia semina hiyo kinamama hao wameiomba serikali kuwajengea mazingira mazuri wajasiliamali wanawake ili waweze kumudu kuzalisha bidhaa zao ambazo ndio msingi wa maisha yao na familia zao.

Awali akifungua semina hiyo, Katibu Tawala wa wilaya ya Bagamoyo Erica Yegela aliwataka kinamama kuwa kitu kimoja ili kufikia malengo wanayojiwekea

Alisema ni vyema wakawa kwenye vikundi ili kuweza kupata msaada ikiwemo mikopo ambayo itawasidia kuendesha shughulizao za ujasiliamli.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Uwezeshaji wanawake kiuchumi Bagamoyo Tedy Davis alisema tatizo linalowakwamisha wajasiliamli wananwake ni kukosa mitaji hali inayopelekea kushindwa kuzalisha bidhaa.

Alisema ipo mikakati mingi ya kuwawezesha wanawake Bagamoyo ili wajikwamue kiuchumi lakini utekelezaji wa mikakati mingi unahitaji fedha.
 
 
Washiriki wa  mafunzo hayo wakifuatilia kwa karibu.
 



Monday, May 21, 2018

WAZIRI MKUU AZINDUA MRADI WA UUNGANISHWAJI WA UMEME WA GRIDI YA TAIFA KWA MIKOA WA LINDI NA MTWARA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akifunua kitambaa kuashiria uzinduzi wa mradi wa uunganishwaji umeme wa Gridi ya Taifa kwa mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Mahumbika Mkoani Lindi leo Mei 21, 2018. Kushoto ni Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, na kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi. Mradi huo sasa umeondoa kero ya muda mrefu ya upatikanaji wa umeme ulio bora na wa uhakika kwenye mikoa hiyo ya Kusini.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,(katikati) na viongozi wengine wa serikali wakiwemo mawaziri akikata utepe kuashiria uzinduzi wa mradi wa kuunganishwa umeme wa Gridi ya Taifa kwa mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Mahumbika Mkoani Lindi leo Mei 21, 2018. 

WAZIRI Mkuu Mhe. Kassim Majaliwaamewahakiki shia watanzania wote kuwa Serikali itafikisha umeme kila kona nakila kijiji.

Waziri Mkuu aliyasema hayo mara baada yakuzindua mradi wa uunganishwaji wa umeme wa Gridi ya Taika kwa mikoa ya Lindi
na Mtwara kwenye hafla iliyofanyika Kituo cha kupoza na kusambaza umeme chaMahumbika mkoani Lindi leo Mei 21, 2018.

Hata hivyo aliwataka kuwa wavumilivu kwanimipango ya serikali ambahyo ni kuhakikisha umeme unafika sio tu maeneo yamijini bali pia kwenye vijiji vyote vya Tanzania.

“Kitendo kinachofanyika hapoa leo ni ushahjidiwa ahadi hiyo ya serikali na ninachowaomba Watanzania ni kuwa na subira kwaniserikali inatekeleza ahadi ilizotoa kuhakikisha watanzania wanapata umem wa uhakika
na wa bei nafuu.”

Akizungumzia  uzinduzi huo ambao sasa umetoa sukuhisho lauhaba wa umeme kwenye mkoa huo wa Lindi Waziri Mkuu alitoa maagizo kwenye
halmashauri zote mkoani humo kuhakikisha maeneo yote nyeti ya huduma za kijamii yanafikishiwa umeme ikiwemo shule na hospitali

“Hatutarajii kuwa na eneo lenye shida ya umeme, hapa ni umeme masaa 24, na tafsiri ya serikali kuwa hapa ni umeme wa uhakika na wa kutosha ndio hii ambayo leo hii tumezindua.” Alisema.

Alisema sera ya serikali ni ya uchumi wa viwanda,na kwamba, wale watu wanaotaka kuwekeza viwanda vya Korosho, Salfa na vifaa
mbalimbaki kwenye mkoa wa Lindi sasa ni wakati wao kwenda mkoani humo na kuwekeza kwani hivi sasa kuna umeme wa uhakika.

Aidha Waziri Mkuu aliwaasa wananchi kuwa
walinzi wa miundombinu ya umeme, na kuwataka wanapoona vitendo vya watu wakihujumu mkiundombinu basi taarifa za kuwashughulikia watu hao ni vema zikatolewa kwa vyombo husika ili kuchukua hatua. “Naomba vifaa vyote vinavyoletwa kwenye maeneo yenu, kwenye vijiji vyenu basi tuvilinde ili hatimaye tuweze kunufaika na uimarishwaji wa miundombinu ya umeme.” Aliasa Wazir Mkuu.

Kupitia Mradi wa umeme vijijini REA,
Serikali imepunguza kutoka Shilingi 380,000/= hadi shilingi 27,000/= tu.

Waziri Dkt. Kalemani, (katikati), akisindikizwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, (kulia) na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka.





SPIKA NDUGAI AKUTANA NA MHE. JAJI WARIOBA OFISINI KWAKE JIJINI DODOMA

Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai (kushoto) akimsikiliza Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba (kulia) alipomtembelea leo Ofisini kwake Jijini Dodoma.

Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Ackson (kushoto) akisalimiana na Waziri Mkuu Mstaafu. Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba (kulia) alipowatembelea jana katika Ofisi ya Bunge Jijini Dodoma. Katikati ni Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai


Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba (kulia) akisalimiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, kazi, Vijana, Ajira na Wenye ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (wa pili kushoto), wa pili kulia ni Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai na kushoto ni Naibu Spika wa  Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Ackson walipokutana leo katika Ofisi ya Bunge Jijini Dodoma.


Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai (kushoto) akiteta jambo na Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba (kulia) alipomtembelea leo Ofisini kwake Jijini Dodoma.

(PICHA NA DEONISIUS SIMBA – OFISI YA BUNGE

RAIS DKT. MAGUFULI AWAPONGEZA WABUNGE WA BUNGE LA AFRIKA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wanahabari mara baada ya kuwapongeza wabunge hao wa Tanzania waliochaguliwa kushika nafasi za juu katika Bunge la Afrika.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Wabunge, wa kwanza kushoto Stephen Masele ambaye amechaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Bunge la Afrika aliyeambatana na Mbunge mwingine Mboni Mhita (kulia) ambaye pia  amechaguliwa kuwa Rais wa Caucus ya vijana ya Bunge la Afrika katika uchaguzi uliofanyika Afrika ya Kusini wiki iliyopita.

Makamu wa Rais wa Bunge la Afrika Stephen Masele akizungumza na Wanahari Ikulu jijini Dar es Salaam. Kulia ni Rais wa Caucus ya vijana ya Bunge la Afrika Mboni Mhita


PICHA NA IKULU



DK.SHEIN AKUTANA NA BALOZI MPYA WA CANADA,CUBA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza  la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na mgeni wake Balozi Mpya   wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Canada pia akiiwakilisha Tanzania nchini Cuba Mhe.Alphayo Kidata  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kujitambulisha,

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza  la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na  mgeni wake Balozi  Mpya wa    Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Canada pia akiiwakilisha Tanzania nchini Cuba Mhe.Alphayo Kidata  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kujitambulisha,

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza  la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akiagana na  mgeni  wake Balozi   Mpya wa    Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Canada pia akiiwakilisha Tanzania nchini Cuba Mhe.Alphayo Kidata  baada ya mazungumzo yao alipofika kujitambulisha Ikulu Mjini Zanzibar leo

Picha na Ikulu



Sunday, May 20, 2018

SIMBA YAMKABIDHI RAIS MAGUFULI ZAWADI YA JEZI NAMBA 19

Uongozi wa klabu ya Simba kupitia kwa Kaimu Rais wake, Salim Abdallah ‘Try Again’ umemkabidhi zawadi ya jezi yenye namba 19 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli.

Abdallah amesema kuwa zawadi hiyo kwa Rais Magufuli ilipaswa kutolewa jana lakini kutokana na ufinyu wa ratiba namna ilivyokuwa ulishindwa kumpatia.

Simba wamemkabidhi jezi hiyo Rais Magufuli kupitia kwa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Harrison Mwakyembe, kufuatia kuwa mgeni rasmi katika mchezo wa jana kati ya Simba dhidi ya Kagera Sugar.

Magufuli alihudhuria mchezo huo wa ligi na kupata fursa ya kuwakabidhi Simba kombe la ligi walilotwaa msimu huu.

Simba wamempa jezi hiyo Waziri Mwakyembe amfikishie Magufuli wakati wa Mkutano wa Mabadiliko ya Katiba uliokuwa unafanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa JK Nyerere, jijini Dar es Salaam leo.

MIGOMBA MABINGWA SIRRO CUP 2018 KIBITI.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarest Ndikilo akimkabidhi kombe la ushindi nahodha wa timu ya Migomba Maulid Mtupa baada ya kuibuka mabingwa wa kombe la IGP Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) kwa kuichapa Mjawa  kwa penati 12 kwa 11 katika uwanja wa Samora Kibiti.
..........................
Na Jeshi la Polisi.


Timu ya Migomba kutoka Wilayani Rufiji mkoani Pwani wametawazwa kuwa mabingwa wa kombe la Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) baada ya kuichapa timu ya Mjawa ya Wilayani Kibiti kwa mikwaju ya penati 12-11 katika fainali iliyopigwa katika uwanja wa Samora Kibiti.

Mchezo huo ulikuwa mkali kwa dakika zote tisini ambapo kila timu ilijitahidi kutafuta nafasi lakini mpaka dakika tisini zinakamilika hakuna timu iliyoweza kuona nyavu za timu pinzani na hivyo kuamuriwa kupigwa kwa mikwaju hiyo iliyopelekea Migomba kuibuka mabingwa.

Kutokana na ushindi huo Migomba walikabidhiwa kombe, pesa taslimu shilingi milioni moja na seti moja ya jezi huku Mjawa wakipata fedha taslimu laki tano na seti moja ya jezi wakati mshindi wa tatu timu ya Mipeko alipata fedha taslimu laki tatu na seti moja ya jezi.

Akizungumza baada ya kuwakabidhi zawadi mabingwa hao, Mkuu wa Mkoa wa Pwani amemuomba IGP Simon Sirro kuendelea kuandaa kombe hilo kwa kuwa limesaidia kuinua vipaji vya vijana wa Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji na kuimarisha usalama kupitia michezo.

“Bila usalama tusingekuwepo leo hii hapa, hivyo nawaasa kuendelea kutoa taarifa za uhalifu ili zifanyiwe kazi kwa maana bila usalama hii burudani tusingeiona hapa na namuomba IGP mwakani tena afanye hivi hivi” Alisema Ndikilo.

Kwa Upande wake Mkuu wa Kitengo cha Michezo ndani ya Jeshi la Polisi Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Philip Kalangi alisema jumla ya timu 52 kutoka Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji zilishiriki michezo hiyo iliyobeba kauli mbiu ya Kibiti Salama, Jamii Salama ikiwa na lengo la kuwakutanisha wakazi wa maeneo hayo kupitia michezo na kupiga vita uhalifu.

Kalangi alisema Programu hiyo ya michezo inafanywa pia katika mikoa mbalimbali kupitia kwa Wakuu wa Polisi wa Mikoa na Wakuu wa Polisi wa Wilaya na ni endelevu ili kusaidia ushirikishwaji wa jamii katika mapambano dhidi ya uhalifu.
 
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Chatanda akimkabidhi seti jezi nahodha wa timu ya Mjawa Bakari Tuga kutoka Kibiti baada ya kushika nafasi ya pili katika kombe la IGP Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) iliyoikutanisha timu hiyo na Migomba kutoka Rufiji katika uwanja wa Samora Kibiti. Migomba walifanikiwa kutwaa ubingwa baada ya kuichapa Mjawa penati 12 kwa 11.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarest Ndikilo akisalimiana na Wachezaji wa timu ya Migomba kutoka Rufiji kabla ya kuanza kwa fainali ya kombe la IGP Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) iliyoikutanisha timu hiyo na Mjawa kutoka Kibiti katika uwanja wa Samora Kibiti. Migomba walifanikiwa kutwaa ubingwa baada ya kuichapa Mjawa penati 12 kwa 11.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarest Ndikilo akisalimiana na Wachezaji wa timu ya Mjawa kutoka Kibiti kabla ya kuanza kwa fainali ya kombe la IGP Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) iliyoikutanisha timu hiyo na Migomba kutoka Rufiji katika uwanja wa Samora Kibiti. Migomba walifanikiwa kutwaa ubingwa baada ya kuichapa Mjawa penati 12 kwa 11.

Picha zote na Jeshi la Polisi

MUFTI ZUBEIR ATAKA WAISLAMU WAITAFUTE ELIMU.

Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Aboubakari Zuberi amesema swala la elimu katika uislamu lina histoeia kubwa kutokana na umuhimu wake hivyo waislamu hawapaswi kujiweka mbali na elimu.

Sheikh Zubeir alitoa kauli hiyo mjini Kibaha Mkowa wa Pwani, wakakti wa kuzindua mafunzo ya uislamu kwa kinababa na kinamama yanayoendeshwa kila mwaka ifikapo mwezi wa Ramadhani.

Alisema kutokana na umuhimu wa Elimu Mtume Muhammad Swalallaahu Alayhi Wasallama aliteremshiwa Aya zinazomtaka msome ili aweze kutekeleza mambo mbalimbali kwa kutumia elimu ikiwemo ibada.

Alisema kuwa uislamu ni dini inayohitaji watu wasome na kuongeza kuwa haikubainishwa kitu gani cha kusoma na kwamba swala la kutafuta elimu halina mipaka ya kitu gani cha kusoma bali kinachozingatiwa ni elimu yenye manufaa na inayosomwa kwaajili ya Mwenyezimungu.

Akizungumzia mpango huo wa kutoa elimu kwa kina baba na kina mama Mkoani Pwani ulioanzishwa na kaimu sheikh wa Mkoa wa Pwani Sheikh Khamis Mtupa, Sheikh Zuberi alisema ni mpango mzuri unofaa kuigwa na masheikh wengine ili kueneza elimu kwa umma wa kiislamu.

Aliongeza kwa kusema kuwa Uislamu hautenganishwi na elimu na wala elimu haitenganishwi na uislamu hivyo waislamu wanapaswa kusoma masomo mbalimbali ikiwemo Maarifa ya uislamu, Uchumi, Ujasiliamali pamoja na kusoma umuhimu wa mahusiano mema baina ya mtu na mtu kama alivyoishi Mtume Muhammad Swalallaahu Alayhi Wasalam.

Aidha, sheikh zubeir aliwataka waandaaji wa masomo hayo kutilia uzito katika somo la amani kwani uislamu ndio dini inayopaswa kuongoza katika kulinda amani na sio kuivuruga amani.

Alisema kwa umuhimu wa somo la amani iko haja ya watoa mada kuandaa vipindi na kuvirusha kupitia vyombo vya habari ili somo la amani lienee miongoni mwa jamii.

Awali akisoma taarifa juu ya namna darsa hizo zinavyoendeshwa na aina ya masomo wanayosomesha Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Pwani Hamisi Mtupa alisema washiriki wa darsa hizo watasomeshwa masomo mbalimbali yatakayowajengea uwezo katika nayna tofauti tofauti.

Nae  Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo, katika hutuba iliyosomwa kwa niaba yake na Kaimu Mkuu wa wilaya ya Kibaha ambae pia ni Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, Majid Mwanga alisema mkoa wa Pwani katika kipindi hiki cha Mwezi wa Ramadhani vyakula vyote vinapatikana kwa wingi katika masoko ya mkoa huo kwa bei za kawaida.

Aidha, alimuhakikishia Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania kuwa,  mafuta ya kula na sukari vipo vya kutosha katika Mkoa huo na kwamba tayari ukaguzi umeshafanywa na Mkuu wa mkoa kuhakikisha vitu vyote vipo na vinapatikana bila ya usumbufu wowote.

Akizungumzia swala amani katika Mkoa wa Pwani Mhandisi Ndikilo alisema Mkoa huo kwa sasa hauna matukio ya uvunjifu wa amani huku kamati ya ulinzi na usalama inaendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo ikiwemo sehemu za kufanyia ibada.

Mpngo huo wa Mafunzo ya uislamu kwa kinababa na kinamama Mkoa wa Pwani yanayofanyika kila mwezi wa Ramadhai umetimiza miaka kumi sasa toka kuanzishwa kwake mwaka 2008 na Kaimu Sheikh wa Mkoa huo Alhaj Hamisi Mtupa.
  
Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Aboubakari Zuberi (kulia) akiwa na Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, Majid Mwanga (kushoto) ambae alimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo.

Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Pwani Hamisi Mtupa akisoma taarifa mpango wa darsa hizo mbele ya mgeni rasmi Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Aboubakari Zuberi.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo