Saturday, June 3, 2017

WAZIRI MKUU AAGIZA KILOSA WAILIPE GAIRO DENI LAO

GAI1
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Bi. Seriel Mchembe mara baada ya kuwasili wilayani humo (Juni 3, 2017) kwa ziara ya kikazi ya siku moja. Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Stephen Kebwe. (Picha na OWM).
GAI2
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa Jimbo la Gairo, Bw. Ahmed Shabiby mara baada ya kuwasili wilayani humo (Juni 3, 2017) kwa ziara ya kikazi ya siku moja. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Stephen Kebwe nawa pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Bi. Seriel Mchembe (Picha na OWM).
GAI3
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Cliford Tandari mara baada ya kuwasili wilayani humo (Juni 3, 2017) kwa ziara ya kikazi ya siku moja. Wa pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Mvomero. (Picha na OWM).
 GAI6
Viongozi na watumishi wa Wilaya ya Gairo wakimsikiliza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (hayupo pichani) katika mkutano aliouitisha mjini Gairo Juni 3, 2017. (Picha na OWM).
 GAI7
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na viongozi na watumishi wa Wilaya ya Gairo (hawapo pichani) katika mkutano aliouitisha mjini Gairo Juni 3, 2017 (Picha na OWM).
 ..........................


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemwagiza Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Clifford Tandari aitishe kikao na uongozi wa Halmashauri ya Kilosa na kupata kauli yao ni lini watalipa zaidi ya sh. milioni 210 wanazodaiwa na Halmashauri ya Gairo.

“Katibu Tawala itisha kikao cha Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Halmashauri, waseme ni lini watazileta fedha hizo ambazo zilitumwa kwao wakati Halmashauri ya Wilaya ya Gairo ikiwa haijafungua akaunti zake,” alisema.

Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Juni 3, 2017) wakati akizungumza na viongozi wa mkoa wa Morogoro, wilaya ya Gairo na watumishi wa Halmashauri ya Gairo mara baada ya kupokea taarifa ya mkoa na wilaya katika kikao kilichofanyika Gairo mjini
“Kilosa ni lazima wazilipe hizo fedha. Katibu Tawala simamia zoezi hilo na kama watachelewa, uzikate moja kwa moja kwenye fedha yao wanayoletwa kutoka Ofisi ya Rais (TAMISEMI). Nataka nipewe taarifa ya maamuzi hayo kabla Juni haijaisha,” alisema.

Mapema akitoa taarifa ya wilaya hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Bi. Siriel Mchembe alisema wanaidai Halmashauri ya Kilosa sh. 233,228,679 ambazo ziliingizwa huko wakati wilaya hiyo  inaanzishwa na hawakuwa wamefungua akaunti ya wilaya.

“Fedha hizi zilikuwa zinapitia Kilosa wakati wilaya ya Gairo imeanzishwa kwa kuwa kipindi hicho wilaya ya Gairo ilikuwa bado haijafungua akaunti. Fedha hizi zinajumuisha ruzuku ya uendeshaji, mapato ya ndani na miradi ya maendeleo,” alisema.

Alisema Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) iliagiza wilaya ya Kilosa ilipe deni hilo kabla ya Juni 2016 lakini hadi sasa wameshalipa sh. milioni 20 tu ambapo sh. milioni 10 zililipwa Desemba 2015 na nyingine milioni 10 zililipwa Mei 2017.

Akisisitiza kuhusu makusanyo ya mapato, Waziri Mkuu amewakumbusha watumishi hao kuwa Serikali imekwishatoa agizo la kutumia mashine za kielektroniki kukusanya mapato ifikapo Julai mosi.

“Makusanyo ya mapato ya ndani ni eneo muhimu sana. Tumeshaagiza, mwisho wa kutumia mifumo ya kawaida ni Juni 30. Kuanzia Julai mosi, kila eneo ni lazima litumie mashine za kielektroniki,” alisema Waziri Mkuu.
Alihoji ni kwa nini Halmashauri ya Gairo ililenga kukusanya sh.milioni 889.5 lakini kufikia Aprili mwaka huu, makusanyo halisi yalikuwa ni sh. milioni 356.2 sawa na asilimia 40.

Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Mamlaka ya Mapato (TRA) ya wilaya hiyo ambao hadi kufikia Aprili, 2017 wameweza kukusanya sh. milioni 601.5 ikilinganishwa na makadirio yao ya kukusanya sh. milioni 471 kwa mwaka. 

Waziri Mkuu aliwapongeza kwa sababu wamevuka lengo kwa asilimia 127.6.
Waziri Mkuu ambaye yuko kwenye ziara ya siku ya wilaya hiyo, asubuhi alipanda mti kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ikiwa maadhimisho ya siku ya upandaji miti hapa nchini.

Pia alikagua mradi wa maji wa kijiji cha Chakwale, na mradi wa visima 10 ambayo imekuwa na mgogoro kwa muda mrefu. Pia atazungumza na wananchi wa Gairo mjini kwenye mkutano wa hadhara.

ANNA MGHWIRA WA (ACT) WAZALENDO APATA UKUU WA MKOA WA KILIMANJARO.

index

Friday, June 2, 2017

MAJALIWA ASHIRIKI SALA YA IJUMAA KWENYE MSIKITI WA GADDAF MJINI DODOMA

ZIL1
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Sheikh Nurdin Kishik ambaye ni Mhadhiri wa Kimataifa wa Dini ya Kiislaam, (kulia) na ujumbe wake, ofisini kwake bungeni mjini Dodoma  Juni  2, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 ZIL2
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza baada ya kushiriki katika sala ya Ijumaa kwenye Msikiti wa  Al- Gadaf mjini Dodoma Juni 2, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
..........................

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Watanzania waendelee kuliombea Taifa ili liendelee kudumu katika hali ya amani na utulivu.

Alisema suala la kudumisha amani na utulivu ni jukumu la kila mmoja, hivyo kila mwananchi kwa imani yake ahakikishe anashiriki kutunza hali hiyo.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Juni 2, 2017) baada ya kumaliza kuswali sala ya Ijumaa katika Msikiti wa Al-Gadaf, mjini Dodoma.

Alisema ni vema kila mwananchi akajivunia hali ya amani na utulivu iliyoko nchini kwa kuwa ndiyo inayowezesha kufanyika kwa shughuli mbalimbali za kimaendeleo. “Tuendelee kudumisha amani, tufanye ibada kila mtu kwa imani yake. Serikali inaheshimu dini zote kwa sababu ndizo zinazojenga amani na mshikamano,” alisema.

Pia amewataka wazazi wahakikishe wanawalea watoto wao katika mazingira ya kidini ili wanapokuwa watu wazima waje kuwa raia wema. “Tuendelee kuhamasisha watoto wetu wasikilize mahubiri ya dini; ni jukumu letu sisi kama wazazi kuwahimiza wahudhurie mahubiri ya viongozi wa dini ili waweze kujijenga vyema kimaadili na kiimani pia.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewakumbusha Waislamu wahakikishe wanautumia vizuri mwezi mtukufu wa Ramadhan kwa kuzidisha ibada na kusaidia watu wenye mahitaji. “Leo ni Ijumaa ya kwanza katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani, nawaomba tutumie vizuri mwezi huu ili tupate baraka,” alisema.

Ibada hiyo ya sala ya Ijumaa iliongozwa na Sheikh Nurdin Kishki ambaye ni Imamu wa Msikiti wa Vetenari, wilayani Temeke, jijini Dar es Salaam.

Sheikh Kishki katika hotuba yake, aliwasisitiza Waislamu waendelee kufanya mambo mema yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu ikiwemo kuwatunza wazazi wao, kumswalia Mtume Mohammed (S.A.W) na kufunga katika mwezi mtukufu wa Ramadhan.

RAIS DKT. MAGUFULI AWATAKA POLISI KUTUMIA WELEDI KUKOMESHA UHALIFU

6JPN1

MAGAZETI YA LEO JUNI O2, 2017.