Saturday, September 24, 2016

WAZIRI MKUU AAGIZA MADAKTARI WANAOMILIKI MADUKA YA DAWA NJE YA HOSPITALI WACHUNGUZWE

fia4
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Bi. Mwanalingwe  Shani Juma  akiwa na  mwanane mchanga, Ngweshani  Khatibu  wakati alipotembelea wodi ya wazazi katika hospitali ya wilaya ya Mafia Septemba 24, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
.............................


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Dk Beatrice Byalugaba kufanya uchunguzi na kubaini madaktari wa hospitali ya wilaya ya Mafia wanaomiliki maduka ya dawa nje ya hospitali hiyo na kuwachukulia hatua.

Amesema ameshangazwa kukuta maduka ya dawa yanayomilikiwa na madaktari nje ya hospitali hiyo kwani tayari Serikali ilishaagiza kuondolewa kwa maduka ya madaktari karibu na hospitali wanazofanyia kazi.

Waziri mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Septemba 24, 2016) wakati alipotembelea hospitali ya wilaya ya Mafia katika siku ya pili ya ziara yake wilayani mafia.

Kuhusu tatizo la upungufu wa dawa hospitalini hapo amemuagiza Dk. Beatrice kufanya utafiti wa aina ya magonjwa yanayowasumbua wananchi wa wilaya hiyo ili wanapoagiza waagize dawa nyingi za kutibu magonjwa hayo.

Pia aliwataka watumishi wa hospitali hiyo wajitahidi kuwahudumia vizuri wagonjwa licha ya uchache wao. Lengo ni kuhakikisha wanapunguza malalamiko kutoka kwa wananchi.

Wakati huo huo Waziri Mkuu amewahamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ili waweze kuwa na uhakika wa kupatiwa matibabu bure kwa kipindi cha mwaka mzima.

Awali Mganga Mkuu wa wilaya hiyo Dk. Joseph Mziba alisema mwamko wa wananchi kujiunga na mfuko wa CHF ni mdogo jambo linalokwamisha upatikanaji wa huduma za afya wilayani Mafia. Jumla ya wananchi waliojiunga na CHF ni  watu 6,000 kati ya watu 50,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo Bw. Eric Mapunda ameiomba Serikali kutoa kibali kwa halmashauri kununua dawa ambazo zinakosekana MSD kwenye soko moja kwa moja bila ya kupitia utaratibu wa manunuzi.

“Kuna wakati tunakosa dawa MSD na kulazimika kununua kwa mawakala kwa kufuata taratibu ya manunuzi. Tunalazimika kununua boksi moja la ambapo boksi moja la panadol linauzwa sh. 20,000 na tukinunua moja kwa moja sokoni bila ya kufuata utaratibu huo boksi hilo hilo tunalipata kwa sh. 8,000,”alisema.

Baadhi ya wananchi waliokuwepo hospitalini hapo walieleza malalamiko yao kuhusu lugha chafu na dharau inayotolewa na baadhi ya madaktari na wauguzi.


WAZIRI MKUU ATEMBELEA KIWANDA CHA SAMAKI CHA TANIPESA MAFIA

fia3
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wa kwanza kulia, akitazama samaki aina ya pweza wakati alipotembelea kiwanda cha samaki cha TANIPESCA eneo la Kilindoni wilayani Mfia  Septemba 24, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
................................


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaagiza mkuu wa wilaya ya Mafia mkoani Pwani, Bw. Shaib Nnunduma pamoja na mkurugenzi wa halmashauri hiyo Bw. Eric Mapunda kuimarisha doria kwenye eneo la bahari ili kuzuia uvuvi haramu.

Amesema vitendo vya uvuvi haramu vinavyoendelea katika wilaya hiyo vinapaswa kudhibitiwa haraka kwa sababu vinasababisha halmashauri hiyo kukosa mapato na kushindwa kuboresha maendeleo ya wananchi.

Waziri mkuu ametoa agizo hilo kwa nyakati tofauti leo (Jumamosi, Septemba 24, 2016) wakati alipotembelea kiwanda cha samaki cha Tanpesca na alipowahutubia wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye kijiji cha Kirongwe wilaya ya Mafia.

Amesema uvuvi ndiyo shughuli kuu ya uchumi na chanzo muhimu cha mapato kwa wilaya ya Mafia na suala la uvuvi haramu linaathiri sana mapato ya halmashauri hivyo ni vema wakaimarisha doria ili kukomesha vitendo hivyo.

“Lazima jambo hili lidhibitiwe. Uvuvi wa kutumia mabomu unaharibu mazingira ya chini ya bahari hivyo samaki wanashindwa kuzaliana kwa wingi. Hakikisheni watu hao wanakamatwa na kuchukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kuteketeza zana wanazotumia,” amesema.

Naye Mkurugenzi wa kampuni ya Alphakrust inayomiliki kiwanda cha Tanpesca, Ganeshen Vedagiri amesema kampuni hiyo imeajiri watumishi 855 kati yake 445 ni wakazi wa wilaya ya Mafia huku wanawake wakiwa 250.

Amesema wanajumla ya mabwawa 76 ya kufugia samaki aina ya kamba na kwa sasa yanayotumika ni 30 na kila moja lina uwezo wa kuzalisha kilo 5,000 katika siku siku 150 na kufanikiwa kuvuna tani 300 kwa mwaka.

Mkurugenzi huyo amesema katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2016.2017 wanatarajia kupata wastani wa sh. bilioni 120 katika mauzo ya nje na sh. bilioni 62 kutoka katika mauzo ya ndani. Wanaltarajia kulipa kodi ya zaidi ya bilioni 15 kwa mwaka huu.

Kwa upande wake Mohamed Gomvu ambaye ni Diwani wa kata ya Kirongwe na Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mafia alisema maeneo yaliyoathirika zaidi na uvuvi haramu ni vijiji vya Ndagoni (Kiega), Kifinge, Chunguruma (Tumbuju) na kisiwa cha Nyororo.

Amesema jambo linalokwamisha ukamatwaji wa uvuvi haramu ni kutokana na watumishi kukosa uamini na kuvujisha siri kwa wavuvi hao hivyo wanashindwa kuwanasa kwenye mitego yao.

KINDAMBA, ATEULIWA KUWA KAIMU OFISA MTENDAJI MKUU WA TTCL

dsc_5652
Waziri Waziri Kindamba, ambae ameteuliwa na Rais Magufuli kuwa Kaimu Ofisa Mtendaji mkuu wa TTCL. 
 

MAGAZETI YA TANZANIA LEO TAREHE 24 SEPTEMBA 2016

wac