Monday, June 3, 2024

WADAU WA USHIRIKA WATOA MSAADA HOSPITALI YA WILAYA YA RUANGWA 

 





Na Mwandishi wetu, Lindi.

Kuelekea siku ya jukwaa la ushirika linalotarajiwa kufanyika hapo kesho juni 04, 2024 wadau wa ushirika Mkoa wa Lindi wamekabidhi misaada mbalimbali ya kibinaadamu kwa wagonjwa waliolazwa katika hospitali ya Wilaya ya Ruangwa pamoja na kupanda miti hospitalini hapo



Misaada hiyo iliyokabidhiwa ni pamoja na sabuni za unga pamoja na sukari ambavyo vimegawiwa kwa akina Mama waliojifungua katika hospitali hiyo


Akizungumza na Waandishi wa Habari, Bi. Cesilia Socitenes amesema kuwa huduma zilizofanyika katika Hospitali ni moja ya utekelezaji wa misingi Saba ya ushirika ambapo msingi wa saba unaelekeza kuijali jamii.


Ameongeza kuwa katika utekelezaji wa msingi huo wa Saba, wanachama wa Vyama vya Ushirika watachangia damu ili kuokoa maisha ya wagonjwa wengi ambao matibabu yao yanauhitaji wa damu.


Kwa upande wake, Ndg. Richard Zengo, Mrajisi Msaidizi anayesimamia Sehemu ya Vyama Visivyo vya Kifedha kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika amesema kuwa moja ya malengo makuu ya Jukwaa la Ushirika ni kuhimiza utekelezaji wa msingi wa saba wa Ushirika ambao ni kujali jamii.


Zengo amesisitiza kuwa shughuli zote zinazofanyika ni kuonesha kwa vitendo namna Ushirika unavyoungana na Serikàli ya Awamu ya Sita katika kutekeleza masuala ya kusaidia jamii inayotuzunguka.

No comments:

Post a Comment