Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia Wazee na Watoto, Mhe. Doroth Gwajima, Jumanne ya leo tarehe 26 Oktoba
2021, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Kituo kipya cha Elimu ya
Masafa (CDE), kilichojengwa kwa ufadhili wa Serikali ya Marekani kupitia kituo
cha Kuzuia na kudhibiti maradhi (CDC).
Sherehe za Uzinduzi huo zitafanyika
katika kituo hicho kilichopo mkoani Morogoro, Wilaya ya Morogoro karibu na
Mizani ya Zamani, na zitahudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Mashiriki ya kimataifa,
uongozi wa Mkoa wa Morogoro, Chuo Kikuu Mzumbe na Mwakilishi Mkazi wa
Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Maradhi cha Marekani CDC, Dr. Mahesh
Swaminathan.
Ujenzi wa Kituo cha Elimu ya Masafa
(CDE) Morogoro, ulianza Januari 2016, kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto na Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti
Maradhi (CDC). Lengo la Kituo hicho ni kuendelea kutoa mafunzo yenye ubora kwa
wafanyakazi wa Afya waliopo kazini, kwa njia ya masafa kupitia mtandao na
Mafunzo ya ana kwa ana.
Kituo hicho kitapanua wigo, uratibu,
maendeleo na kutekeleza mpango wa Serikali kupitia Wizara ya Afya wa kutoa
mafunzo ya masafa na kutekeleza mipango ya elimu kwa walengwa kufikia Viwango
vya Kitaifa.
Kupitia msaada uliotolewa na Kituo
cha Kimataifa cha CDC, Kituo hicho kimefungwa vifaa vya kisasa vitakavyowezesha
mafunzo kwa njia ya mtandao kuendeshwa nchi nzima, kutumia teknolojia kuendesha
mikutano kwa njia ya video, pamoja na kujenga mfumo wa utunzaji kumbukumbu kwa
kozi za masomo ya kielektroniki zitakazokuwa zinatolewa.
Wadau wengine walioshiriki kwa karibu
kufanikisha kukamilika kwa utendaji wa kituo hicho ni Shirika la Marekani la
Maendeleo ya Kimataifa (USAID) na Shirika la Sayansi ya Usimamizi wa Afya (MSH)
ambao kwa kiasi kikubwa wameshiriki katika kuandaa mitaala ambayo itasadia
kufikiwa malengo ya Kituo ya utoaji huduma za Afya zenye ubora kwa watoa huduma
na wadau wa afya nchini kote.
Hadi sasa Kituo cha Elimu Masafa
kimenufaisha wataalamu wa Afya takribani 34,357, hivyo kukamilika kwa jengo la
Kituo hicho kutaongeza idadi ya wanufaika.
Mashirika mengine yanayotazamiwa
kushiriki sherehe hizo ni pamoja Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), Shirika la
Idadi ya Watu Ulimwenguni (UNFPA), Shirika la Menejimenti na Maendeleo ya Afya
(MDH), Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na
Utamaduni (UNESCO), Benjamin Mkapa Foundation, I-Tech Tanzania, Shirika
la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto (UNICEF), JHPIEGO, Mfuko wa Kimataifa
(Global Fund), Amref, CRS, CSSC, PATH, Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania na
wadau wengine mbalimbali wanaotoa huduma za Afya nchini.