Monday, March 4, 2019

UMEME UTUMIKE KUONGEZA UFAULU SHULENI- MGALU.

Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Bi. Subira Mgalu, Akizungumza wanafunzi wa Shule ya Msingi Chalinze Mzee iliyopo Chalinze Mkoani Pwani kabla ya kuzindua na kuwasha Umeme rasmi katika kijiji cha Chalinze Mzee Mkoani Pwani.
..................

Na Yasini Silayo, Pwani

Naibu Waziri wa Wizara ya Nishati Mhe. Bi. Subira Mgalu akizindua na kuwasha rasmi miradi ya Umeme Vijijini katika Vijiji vya Chalinze Mzee A-C na Nero Vilivyoko Chalinze, Mkoani Pwani Leo ametoa Rai kwa vijiji vyote ambavyo tayari vimefikiwa ama kuunganishwa na huduma ya Nishati ya Umeme kuitumia fursa hiyo kuboresha ufaulu pamoja na kuinua kiwango cha elimu kwa ujumla.


“Ni mategemeo yetu kuwa ujio na matumizi ya Nishati ya umeme utaboresha na kuongeza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa shule mbalimbali kutokana mazingira wezeshi ya kujisomea na kujifunza muda wote kwa kutumia mwanga wa umeme lakini pia kuendana na mahitaji ya elimu ya kisasa inayojikita zaidi katika sayansi na teknolojia hususan matumizi ya kompyupa na maabara za kisasa za mafunzo kwa vitendo” Alisema Mhe. Subira, Akiwa katika shule ya Msingi Chalinze Mzee kijiji Cha Chalinze mzee A, Mkoani Pwani.


Naibu Waziri Mgalu, Aliongeza kuwa, Ndoto ya Serikali ya Awamu ya Tano ni, kusambaza Nishati ya umeme Nchi Nzima na kwa wananchi wote, umeme utakaokuwa chachu ya maendeleo katika nyanja mbalimbali ikiwemo za Maendeleo ya Huduma za kijamii sambamba na zile za Kiuchumi, sekta ya elimu kwa vijana na watanzania kwa ujumla ikiwemo kama miongoni mwa sekta za vipaumbele.


Naye mwalimu mkuu wa shule hyo aliyejitambulisha kwa jina la Marianus Nyalale, mbali na kuelezea shukurani zake kwa kufikishiwa umeme mpaka shuleni hapo, alisema kuwa Shule ina matarajio makubwa ya kufanya mabadiliko makubwa ya kiufundishaji na ufaulu mara baada ya kuunganishwa na huduma ya umeme wa TANESCO.


“Tunategemea kuanza mpango wa kutafuta fedha kwaajili ya kununua compyuta na vifaa mbali mbali vya kufundishia vinavyotumia umeme lakini pia hivi sasa wanafunzi wataweza kujisomea madarasani hata vipindi vya jioni” alisema Mwl. Nyalale


Aidha, Mhe. Mgali akizindua na kuwasha rasmi umeme katika kijiji cha Nero, alisisitiza na wananchi pia kuchangamkia fursa ya umeme kwa kufanya shughuli mbalimbali za kimaemdeleo na kiuchumi. 


Shughuli zitakazopelekea wao kujiongezea kipato lakini pia kukuza uchumi wa Nchi kwa ujumla.

Sunday, March 3, 2019

Watanzania acheni matumizi ya "headphones" kupita kiasi...Waziri asema ni chanzo cha usikivu hafifu

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (kulia) akifanyiwa uchunguzi wa sikio na Daktari bingwa wa masikio Dkt. Godlove Mfuko katika Hospitali ya Taifa Muhimbili - Mloganzila

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Bw. Makwaiya Makani akizungumza jambo katika siku ya Usikivu Duniani ambayo kitaifa imefanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili - Mloganzila

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (aliyeketi) akiwekewa vifaa vya uchunguzi wa usikivu na mtaalam wa usikivu Bi. Tedi Uiso kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili - Mloganzila.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu(kulia) akisalimiana na watoto waliofika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya usikivu. 




Dar Es Salaam
Spika za masikioni maarufu kwa jina la “Headphones” zimetajwa kuwa chanzo kinachopeleka tatizo la usikivu hafifu kwa watu.
Hayo yamesemwa leo na Waziri mwenye dhamana ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu alipokuwa akizungumza na wananchi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila Jijini Dar Es Salaam katika kuadhimisha siku ya usikivu duniani.

Waziri Ummy amesema kuwa matumizi ya simu za kisasa yameongeza kasi ya watu kutumia spika za masikioni jambo ambalo linahatarisha kuwa na watu wengi wenye matatizo ya usikivu. 

“Unakuta kijana kuanzia asubuhi mpaka jioni ameweka spika za masikioni anasikiliza muziki hawajui wanajiweka katika hatari ya kupata tatizo la usikivu” amesema Waziri Ummy na kuendelea kusema kuwa kundi la vijana liko hatariki kupata matatizo ya usikivu.
Waziri Ummy ametumia nafasi hiyo kutoa rai kwa wananchi kupunguza matumizi ya spika za masikioni ili kuweza kujikinga na matatizo ya usikivu.
“Nitoe rai kwa vijana wapunguze matumizi ya spika za masikioni kwa muda mrefu, tusipo kuwa makini tunaweza kujikuta tuna taifa lenye watu wengi wenye matatizo ya kutosikia vizuri” amesema Waziri Ummy. 
Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa tatizo la usikivu hutokea pia kwa njia mbalimbali ikiwemo kwa kuzaliwa na tatizo hilo au kulipata ukubwani kutokana na sababu nyinginezo ambazo zinaambata kwa kukaa kwa muda mrefu kwenye sehemu zenye kelele nyingi pamoja matatizo yanayoambata na afya ya sikio.
Waziri Ummy amesema kuwa ni jambo jema kuona sasa matibabu ya matatizo ya usikivu hafifu yanapatikana hapa hapa nchini huku akiwataka wananchi kukata bima za afya ili kuweza kupata matibabu kwa uhakika.
“Serikali imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha tatizo hili linazuiliwa kabla ya kutokea lakini pia kuhakikisha matibabu yanapatikana yakiwemo kutumia mashine ya mawimbi ya sauti, upasuaji wa kuziba tundu la ngoma ya sikio pamoja na kupandikizwa vifaa vya kusaidia kusikia” amesema Waziri Ummy.

Hata hivyo alisema takwimu zinaonyesha kuwa mwaka 2018 Hospitali ya Muhimbili imefanikwa kuwapatia wagonjwa 116 vifaa vya mawimbi ya sauti, wagonwja 43 walifanyiwa upasuaji wa kuziba tundu la ngoma ya sikio.
Waziri Ummy amesema kuwa Serikali itaendelea kuboresha huduma za matibabu ya kibingwa na kuhakikisha matibabu yanapatikana hapa hapa nchini.
Awali akitoa taarifa yake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Bw. Makwaiya Makani amesema kuwa wamekuwa wakifanya jitihada mbalimbali katika eneo la usikivu ikiwemo kutoa huduma ya upandikizaji vifaa vya usikivu kwa Watoto wenye matatizo ya hayo.

“Tangu mwezi Juni mwaka 2017 tayari watoto 21 wamepandikizwa vifaa vya usikivu kitaalam kwa jina la 'cochlear implants” amesema Bw. Makani 
Bw. Makani amesema kuwa wameendesha kliniki ya siku mbili katika Hospitali ya Mloganzila kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya matatizo ya usikuvu ambapo watu 264 wamejitokeza kati yao watu 172 walihitaji uchunguzi zaidi wa usikivu, watu 64 wamekutwa na matatizo ya usikivu na tayari wamepatiwa rufaa kwa ajili ya matibabu zaidi na watu 31 wamekutwa na nta za masikioni,pia watu 26 wamekutwa na maambukizi kwenye masikio ambao wamepatiwa rufaa ya matibabu zaidi.
Tatizo la usikivu linazidi kuongezeka siku hadi siku. Inakadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 5 ya watu duniani wana tatizo la usikivu. Tatizo hili litaongezeka maradufu kila mwaka. Inatakiwa kila mmoja achukue hatua kujikinga na tatizo hili ikiwemo kuepuka sehemu zenye kelele na pia kusikiliza mziki kwa sauti kubwa na kwa muda mrefu na kwa kutumia spika za masikioni.

Friday, March 1, 2019

HALMASHAURI YALAZIMISHWA KUHAMISHA DAMPO

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima (wa pili kutoka kushoto) akimsikiliza Mratibu wa Kanda kutoka Baraza la Taifa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Bw. Godlove Mwamsojo mara baada ya kutembelea dampo lililopo katika Kata ya Saja, Kijiji cha Itengelo Wilaya ya Wanging’ombe. Naibu Waziri Sima ameagiza kufungwa kwa dampo hilo na kuteketeza taka zote zilizopo.
…………………..
Na Lulu Mussa,Njombe
Halmashauri ya Mji wa Makambako Wilayani Njombe imeagizwa kusitisha mara moja utupaji wa taka ngumu katika dampo lililopo katika Kata ya Saja, Kijiji cha Itengelo Wilaya ya Wanging’ombe kutokana na kutokidhi matakwa ya Sheria ya Mazingira na malalamiko yaliyotolewa na wananchi katika vijiji vya jirani.
Agizo hilo limetolewa hii leo Mkoani Njombe na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima mara baada ya kufanya ziara ya kikazi na kumuagiza Kaimu Mkurugenzi wa Mji wa Makambako Bw. Rashid Hozi kutafuta eneo maalumu litakalokidhi mahitaji husika ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya athari kwa mazingira
Akiwa katika eneo hilo la dampo la Makambako ambalo kwa hivi sasa liko katika Wilaya ya Wanging’ombe, Mhe Sima ameshuhudia wananchi wakiingia kiholela katika dampo hilo kwa ajili ya kuokota bidhaa mfano chupa za plastiki kwa ajili ya kuziuza.
“Serikali inatumia pesa nyingi katika huduma za afya ni wakati sasa tupunguze mzigo huu kwa magonjwa yanayoweza kuepukika kwa kuwa na mazingira safi na salama. Kuanzia sasa ni marufuku wananchi kuingia dampo kuokota chupa za plastiki, hii inahatarisha afya zao wenyewe, hivyo utaratibu wa kutenganisha taka uanzie katika vyanzo vya uzalishaji” Sima alisisitiza.
Awali Mratibu wa Kanda wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira  (NEMC) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Bw. Godlove Mwamsojo amesema kuwa Baraza limetoa notisi ya siku sitini (60) kuanzia tarehe 01/02/2019 kwa Halmashauri hiyo ya kusitisha utupaji wa taka katika eneo hilo na kuwaagiza kuteketeza taka zote zilizopo katika kipindi kilichotajwa.
Bw. Mwamsojo amesema kuwa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004, kifungu cha 119 kinazitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kutafuta namna bora ya kuteketeza taka ngumu katika maeneo yao na kuainisha kuwa dampo hilo kwa sasa liko katika eneo la mwinuko hivyo kipindi cha mvua hutiririsha maji ambayo si salama kwa wakazi wa maeneo ya chini.
Wakati huo huo, Naibu Waziri Sima pia amemuagiza Mratibu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuhakikisha anafuatilia utekelezaji wa agizo hilo na endapo Halmashauri haitatekeleza agizo hilo hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yao .
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Mji wa Makambako Bw. Rashid Hozi amekiri kupokea barua ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira na kuahidi kutekeleza maagizo yaliyotolewa kwa muda muafaka.
Naibu Waziri Mussa Sima, yuko katika ziara ya kikazi katika mikoa ya Nyanda za juu Kusini kuainisha changamoto za kimazingira katika sekta ya afya ikiwa ni pamoja na  kukagua mitambo ya kuteketeza taka hatarishi katika Hospitali, kujionea hali ya madampo katika mikoa husika endapo utaratibu wa kutenganisha taka unazingatiwa ili kuzuia wananchi kuzifuata baadhi ya bidhaa zinazo rejerezeka katika maeneo ya dampo kwa lengo la kudhibiti milipuko ya magonjwa.
Katika Mikoa ya Njombe, Mbeya na Iringa Mheshimiwa Sima pia atapata fursa ya kuembelea kwenye ikolojia ya vyanzo vya maji vinavyo changia maji katika bonde la Rufiji.

Prof. Mohamed Janabi atoa tathimi ya undendaji kazi wa Taasisi ya moyo Nchini, Bodi yasifu


Kuongezeka wa idadi ya wagonjwa wanaofanyiwa vipimo na uzibuaji wa mishipa ya damu ya moyo ambayo imeziba kupitia  mtambo wa Cathlab ni ishara kuwa watu wengi wanahitaji kupata huduma hiyo.
Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi wakati akisoma ripoti ya utendaji kazi wa Taasisi hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu ya Oktoba hadi Desemba kwa bodi ya Wadhamini.
Prof. Janabi alisema tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo mwaka 2016 hadi 2018 katika mtambo wa Cathlab wameona zaidi  ya wagonjwa 2389 ambao waliwafanyiwa vipimo na kuwazibua  mishipa ya damu ya moyo iliyokuwa  imeziba.
“Kupitia mtambo huu tunafanya upasuaji wa moyo wa  bila kufungua kifua kupitia tundu dogo linalotobolewa kwenye paja.  Kwa mwaka jana pekee tulifanya upasuaji kwa wagonjwa 1056 na kuvunja rekodi katika nchi za Afrika Mashariki na Kati”, alisema Prof. Janabi.
Alisema hivi sasa madaktari wa magonjwa ya moyo kwa watoto kupitia mtambo huo wa Cathlab  wameanza  kuziba matundu na kuzibua mishipa ya damu iliyoziba.
“Kipindi cha nyuma watoto walikuwa wanafanyiwa upasuaji huu na madaktari wageni hii ilitokana na kutokuwa na daktari wa kutoa huduma hiyo katika Taasisi yetu. Mwaka jana daktari wetu mmoja aliyekuwa anasoma Afrika ya Kusini amerudi baada ya kumaliza masomo yake na anafanya upasuaji siku ya Jumatano”,.
“Tumetenga siku moja kwa wiki ambayo ni jumatano watoto wanafanyiwa upasuaji wa kuziba matundu na kuzibua mishipa ya damu iliyoziba, uhitaji ni mkubwa na mtambo uliopo ni mmoja. Kuna haja ya kuwa na mtambo mwingine wa Cathlab ili wagonjwa wengi wenye uhitaji wa huduma hii waweze kuipata”, alisema Prof. Janabi.
Katika hatua nyingine Prof. Janabi alisema mwezi wa sita mwaka huu Madaktari Afrika kutoka nchini Marekani watakuja nchini kupanda  mlima Kilimanjaro kwa ajili ya kuchangia fedha za matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini Prof. William Mahalu aliipongeza menejimenti na wafanyakazi wote wa Taasisi hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutoa huduma ya matibabu ya magonjwa ya moyo.
Prof. Mahalu ambaye pia ni daktari bingwa wa upasuaji wa  moyo na mishipa ya damu alisema kufanya vizuri kwa mtambo wa Cathlab kunaonesha kuwa watu wengi  wanahitaji huduma hiyo na wao  kama bodi wameona  kunahaja ya kuongeza mtambo wa pili wa Cathlab ili wagonjwa wengi wapate huduma hiyo.
“Mmetuambia hivi karibuni mmesaini mkataba wa makubaliano ya  kuletwa kwa wagonjwa kutoka nchi ya Malawi na Visiwa vya Zanzibar kwa ajili ya matibabu, hongereni sana. Endeleeni kufanya kazi kwa bidii na kujituma ili watu wengi zaidi wafaidike na huduma mnayoitoa”, alisema Prof. Mahalu.
Alisema miaka minne au mitano ijayo wataalamu kutoka nje ya nchi  wanaokuja  kufanya kambi maalum za matibabu ya moyo watakuja nchini kujifunza  kutoka kwa watanzania  baada ya wao kuja kutoa msaada.
Prof. Mahalu alimalizia kwa kuwataka wataalamu wa magonjwa ya moyo kufuatilia maendeleo ya  wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi hiyo pindi wanaporuhusiwa kurudi nyumbani.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu akizungumza jambo na wafanyakazi wa maabara alipotembelea maabara hiyo kwa ajili ya kuangalia mashine mpya za uchunguzi wa vipimo vya magonjwa ya moyo zilizofungwa. Watatu kulia kutoka kwa Prof. Mahalu ni mjumbe wa bodi Dkt. Donan Mbando.
Watoto wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa wanacheza gemu kama walivyokutwa  na mpiga picha wetu. Watoto wawili kati yao wamefanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua  na wawili wanasubiri kufanyiwa upasuaji wa moyo.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu na mjumbe wa bodi hiyo Dkt. Donan Mbando wakitoka kuangalia wodi mpya ya watoto wenye magonjwa ya moyo ambayo imejengwa na kufanyiwa ukarabati.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu na mjumbe wa bodi hiyo Dkt. Donan Mbando wakiangalia chumba cha wagonjwa walioko katika uangalizi maalum (ICU) kilichopo katika wodi  mpya ya watoto wenye magonjwa ya moyo ambayo imejengwa na kufanyiwa ukarabati. Chumba hicho kikianza kufanya kazi kitakuwa na vitanda nane na kuweza kurahisisha kutoa huduma kwa watoto wanaohitaji matibabu  ya dharula.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu akiangalia (medical gas bed head panel) mahali pa kuchomeka mashine ya kutolewa hewa ya matibabu  kwenda kwa mgonjwa  katika wodi mpya ya kulipia ya watoto wenye magonjwa ya moyo ambayo imejengwa na kufanyiwa ukarabati. 
Picha na JKCI

Ratiba rasmi ya kuaga mwili wa Ruge, Dar es salaam Kesho Jumamosi March 2

Mwili wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba umewasili nchini leo mchana, 1, Machi, 2019.

Mwili wake unatarajia kuagwa Jumamosi, 2 Machi, 2019 katika ukumbi wa Karimjee, Jijini Dar es salaam kabla ya kusafirishwa mkoani Kagera kwaajili ya mazishi yatakayofanyika Jumatatu, 3 Machi, kijijini kwao Kiziru wilayani Bukoba.

Hii hapa ni ratiba rasmi ya kuuaga mwili wake.


Advertisemen