Tuesday, November 15, 2022

DC MALINYI ATOA MAELEKEZO SOMO LA EDK.



Afisa Tarafa ya Malinyi Ms Rehema Rajabu, ambae amemwakilisha Mkuu wa wilaya ya Malinyi, akizungumza na walimu wa somo la dini ya Kiislam (EDK)Wilayani Malinyi. Rehema amewaomba walimu wa kiislam kujitoa kwa dhati kufundisha somo hilo ili kutengeneza maadili ya vijana.








Mwandishi wetu, Malinyi

Mkuu wa wilaya ya Malinyi mkoa wa Morogoro, Mathayo Masele, ametoa rai kwa walimu wa umma wenye uwezo wa kufundisha somo la elimu ya dini ya Kiislam (EDK) kufanya hivyo mara moja huku akisisitiza kuwa hakuna haja ya kuona haya, woga au hofu yeyote.

Akizungumza katika semina ya walimu wa somo hilo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Afisa Tarafa ya Malinyi Ms Rehema Rajabu amesema haoni sababu ya walimu kuwa na hofu ya kufundisha elimu ya dini huku wakijua wazi kuwa kufanya hivyo sio kosa kisheria

 

“Nitashangaa sana kama bado wapo walimu wenye uwezo wa kufundisha somo hili lakini wanajificha kwa kuogopa watu, serikali inapenda kuona jamii inalelewa katika maadili mema na somo hili linajikita kwenye maadili, kwa nini sasa mwalimu uogope kutoa elimu yako,” alihoji Ms Rehema

Aidha, Rehema amewahamasisha wananchi wa Wilaya ya Malinyi kufanyia pupa mambo ya heri ili kukabiliana na tatizo la mmomonyoko wa maadili ambalo linaota mizizi kila kukicha.

“Hapa wilayani bado muamko wa dini uko chini, wengi wamejikita kwenye utamaduni wa asili, nadhani muda umefika wa kubadilika, tuanze kuwapeleka vijana wetu madrasa kujifunza wajibu wao na sababu za kuletwa duniani, naamini nyoyo za watoto wetu zitajengeka kimaadili kwani watakuwa ni watoto wenye hofu na Mungu,” aliongeza.

Vilevile, ameitaka jamii ya Malinyi kuwa na moyo wa kutoa mali zao kwa ajili ya kuendeleza dini, na kwa kuanzia ameshauri kutatua changamoto ya vitabu vya EDK ambayo bado haijapatiwa ufumbuzi

“Walimu wamesema hapa tunalo tatizo la vitabu vya EDK, kwa kuanzia vinatakiwa vitabu vyenye thamani ya Milioni tatu, jambo hili lipo ndani ya uwezo wetu, tutowe mali zetu ili vijana wetu wapate elimu hii muhimu,” alisema.

Ms Rehema amesema katika mambo yanayomuhuzunisha licha ya ukweli kuwa jamii ya Malinyi ni tajiri lakini wamekuwa na moyo mgumu wa kujitoa kwenye mambo ya dini.

Alisema kitendo hicho kimepelekea muamko wa dini kuwa chini na hivyo vijana wengi wa eneo hilo wamejikuta wakiitanguliza Zaidi dunia kuliko akhera yao.

Katika hatua nyingine walimu wa shule za msingi na sekondari wilayani humo wameungana na Kaimu Mkuu wa Wialaya huyo, Ms Rehema kwa kusema kuwa bado kuna changamoto ya somo la dini wilyani humo.

Mmoja wa walimu hao, Bw. Fadhiri Chuma, Mwalimu wa shule ya sekondari Mtimbira alieleza kuwa kunahitajika vitabu vya kutosha ili kufundisha somo hilo, kwani walimu wapo wa kutosha shida ni vitendea kazi.

Alisema licha ya uwepo wa vipindi vya dini, lakini wamejikuta wanashindwa kufanya kazi kwa ufanisi kwa kukosa miongozo ya somo la EDK hali inayopelekea somo hilo kuwa geni kwa watoto wa Malinyi

Pia Mwalimu Shaabani Mandanda kutoka shule ya msingi Nawigo iliyopo Wilaya ya Malinyi amewaomba waislam na jamii kwa ujumla kujitoa kwa hali na mali ili vitabu vya elimu ya dini vipatikane na vijana waanze kupatiwa mafunzo yatakayo wasaidia katika maisha yao.

 

Hali ya somo la EDK Malinyi…

Aidha, akizungumzia hali ya somo la EDK wilayani Malinyi, mmoja wa wazazi wa eneo hilo, Matano Matano alisema ni mbaya sana kwani Wilaya nzima haina watoto wanaosoma somo hilo

“Mtoto akichukua somo hilo kwake inakuwa ni mtihani mkubwa, hakuna Mwalimu wa kufundisha, mwanangu amejitahidi kulichukua kwa sababu msingi wake umejengwa kwenye dini akiwa Zanzibar lakini walimu wa kufundisha somo hilo hapa katika wilaya yetu hakuna.

Nimejaribu kuwafuata walimu kadhaa ambao najua wanafahamu kidogo kuhusu EDK kwa kuahidi kuwalipa kwa mwezi 100,000, ajabu ni kwamba hakuna hata mmoja aliyejitokeza.

Kila mmoja anatoa udhuru, yaani 100,000 kwa mwezi, alafu unafundisha kwa wiki mara moja, watu wanaona shida, vipi mtoto anaweza kupenda somo hilo,” alisema kwa uchungu bwana Matano

Kwa upande wake Amiri wa Islamic Education Panel Kanda ya Mashariki, Abuuswaburi akielezea maendeleo ya somo hilo amesema maendeleo ni ya kuridhisha ukilinganisha na miaka ya nyuma.

 

Amesema kwa mujibu wa Matokeo ya Mtihani wa Taifa wa Elimu ya Dini ya Kiislamu nchini (EDK) kwa mwaka 2022 kiwango cha ufaulu kimepanda kutoka wastani wa asilimia 49.78 kwa mwaka 2021 hadi kufikia wastani wa 66.77.

 

Aidha idadi ya watahiniwa nayo imeongezeka kutoka  watahiniwa 126,088 mwaka 2021 hadi kufikia watahiniwa 142,522 mwaka 2022, ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 16,434 sawa na asilimia 13.3

 

Aidha Wanafunzi 3,567 wamefanya vizuri katika mitihani yao kwa kupata Daraja A huku waliopata Daraja B wakiwa 22,587 na C wakiwa 69,012.

 

Akifafanua ufaulu huo alisema kwa ujumla waliofaulu kwa kupata Daraja A hadi C ni watoto 95,166 sawa na asilimia 66.77, huku watoto 47,356 sawa na asilimia 33.23 wakipata Daraja D na E. Daraja D watoto 45,781 na E watoto 1,575.

 

Naye Mratibu wa Islamic Education Panel Taifa (IEP), Suleiman Daudi, amewakumbusha waislam wa Malinyi na Taifa kwa ujumla kutoa mali zao kwa ajili ya kutengeneza nyoyo za kizazi cha kesho kimaadili.

Friday, November 11, 2022

DKT. MPANGO ATAKA WASANII KUZINGATIA MAADILI YA TAIFA.

 No description available.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango akihutubia viongozi na washiriki mbalimbali wa Tamasha la 41 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni la Bagamoyo wakati wa ufunguzi wa Tamasha hilo linalofanyika katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani leo tarehe 11 Novemba 2022.

..............................................................

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa watanzania wote hususan wasanii wa kizazi kipya, kuepuka kuiga kila tamaduni bila kuchuja wala kuzingatia maadili ya taifa.

 

Makamu wa Rais amesema hayo leo tarehe 11 Novemba 2022 wakati akifungua Tamasha la 41 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni la Bagamoyo linalofanyika katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani.

 

Ametoa rai kwa wasanii wa muziki na filamu kuhakikisha wanazingatia maadili na miongozo ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) pamoja na Bodi ya Filamu Tanzania wakati wa utengenezaji wa maudhui ya kazi zao ili kuepukana na uvunjifu wa maadili unaojitokeza.

 

Makamu wa Rais amesema Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo inapaswa kushirikiana na wadau husika kuendelea kutoa elimu na kutafuta namna bora ya kutatua changamoto zote zinazohusiana na hakimiliki, hakishiriki, mirabaha na mikataba katika sekta ya Utamaduni na Sanaa kwa ujumla.

 

Pia Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii kuhakikisha zinahifadhi, kutunza na kutangaza tamaduni za makabila kupitia utalii wa kiutamaduni (cultural tourism) na kutoa nafasi kwa makabila mbalimbali hapa nchini kuonesha tamaduni zake kwenye chakula, dawa za asili, mavazi, makazi pamoja na aina ya ngoma na burudani zake.

 

Aidha ameagiza kila mkoa kuweka utaratibu wake wa kuendeleza utamaduni wa mkoa huo kama sehemu ya utalii wa kiutamaduni.

 

Halikadhalika Makamu wa Rais ameiagiza Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kutoa kipaumbele katika kuendelea kukitangaza Kiswahili duniani, kuhakikisha inaanzisha Kituo cha Taifa cha Sanaa cha Watoto na Vijana wenye vipaji ambao hawapo kwenye mfumo rasmi wa elimu, kuanza ujenzi wa Jumba Changamani la Uzalishaji wa Filamu pamoja na kuanzisha shule maalum za kukuza vipaji vya wanamichezo (sports academy).

 

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia itaendelea kuunga mkono wasanii hapa nchini na kuzipa kipaumbele sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo ili ziweze kufaidisha vijana wengi zaidi.

 

Kwa Upande wake Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa amesema Wizara hiyo inalenga kuinua kiwango cha Tamasha la Sauti za Busara Zanzibar pamoja na Tamasha la Bagamoyo ili yaweze kufikia viwango vya kimataifa na kufanana na matamasha makubwa duniani.

 

Amesema lengo la Wizara hiyo ni kuhakikisha matamasha hayo yanakuwa na msaada kwa kuongeza kipato kwa wananchi, kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi pamoja na kuitangaza nchi kimataifa.

 

Tamasha la 41 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni la Bagamoyo linafanyika kwa siku tatu tarehe 10-12 Novemba 2022 na kushirikisha wadau mbalimbali wa Sanaa na vikundi vya Sanaa kutoka ndani na nje ya Tanzania.

 No description available.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango akipiga ngoma kuashiria kufunguliwa rasmi kwa Tamasha la 41 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni la Bagamoyo linalofanyika katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) mkoani Pwani leo tarehe 11 Novemba 2022. (Kushoto ni Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa).

 

MKUU WA IDARA YA UJENZI KIBAHA MJINI ACHUKULIWA HATUA ZA KINIDHAMU- NDOMBA

No description available.

No description available.

No description available.

Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha

BARAZA la madiwani Halmashauri ya Mji wa Kibaha ,limemchukulia hatua ya kinidhamu mkuu wa idara ya ujenzi Brighton Kishoa kwa kumkata mshahara wake asilimia 15 ndani ya miaka mitatu , kutokana na uzembe kwenye usimamizi  wa ujenzi wa nyumba ya mkurugenzi na kuisababishia hasara Halmashauri hiyo.

Hatua hiyo ni fundisho kwa wakuu wa idara na watendaji wengine endapo watazembea na kushindwa kufanya kazi kwa mujibu wa sheria.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha,Mussa Ndomba alieleza maazimio hayo katika kikao cha robo mwaka baada agenda iliyojadili makosa ya kinidhamu ya mtumishi huyo ambae amekutwa na makosa ya uzembe na kushindwa kusimamia mradi huo.

Alifafanua, kamati za uchunguzi zimefanya kazi yake na kujiridhisha kuwa mkuu huyo wa idara amefanya uzembe.

“Hakuna anaependa kuchukuliana hatua kama hizi ,Ila inafikia hatua unachoka kutoa maagizo na kuelekeza kila wakati, adhabu hii anastahili  kutokana na makosa aliyopatikana nayo ikiwemo usimamizi mbovu kwenye ununuzi wa vifaa na kusababisha gharama kubwa ya manunuzi wa vifaa kwenye ujenzi huo”aliongezea Ndomba .

Ndomba alitoa wito kwa watumishi wote hadi ngazi ya mtaa kufanya kazi kwa kufuata kanuni na taratibu bila kupingana na miongozo iliyopo.

“Kwa kutofuata miongozo miradi ya Serikali na utoaji huduma haitoonekana wala kuleta tija:” Hivyo asitokee mtumishi yeyote kuturudisha nyuma ,sisi kama Baraza tutakuwa wakali,hatutovumilia,kuona Mtendaji anazorotesha huduma kwa Wananchi,kuanzia sasa tutakuwa wakali, tutachukua hatua kwa wale wote watakaoonyesha utovu wa nidhamu kwenye utendaji kazi wao”alisisitiza Ndomba.

Vilevile, madiwani akiwemo diwani wa Kongowe Hashim Shomari, Diwani wa kata ya Tangini Mfalme Kabuga na diwani wa Visiga Kambi Legeza walieleza, wamechoshwa na changamoto zinazoelekezwa hospital ya Mkoani .

Kufuatia malalamiko hayo ,Baraza hilo limetoa wiki moja kwa idara ya afya kushughulikia baadhi ya changamoto zinazolalamikiwa katika hospital ya Mkoani  .

Walieleza , hospital hiyo imekuwa ikitolewa malalamiko mengi hivyo idara ijitathmini ,na kujitahidi kutatua changamoto zinazoelekezwa katika hospital hiyo na baadhi ya Zahanati .

“Ifikie hatua ya kuona umuhimu wa maagizo na maelekezo mnayopewa na madiwani kila tunapokutana ,nendeni mkajitathmini na kufanya Yale ambayo yatapunguza changamoto zinazotajwa Mara kwa Mara ,”

Tunatoa siku 7 mkatatue mliyoelekezwa”jumatatu kamati ya fedha inakutana iidhinishe hata kama milioni 100 ili utekelezaji uanze”

Nae diwani wa kata ya Pichandege Karim Mtambo ,alihoji sh.milioni 800 zilizoidhinishwa kuendeleza ujenzi wa baadhi ya maeneo katika hospital ya wilaya ya Lulanzi ambayo tayarii imeshaanza kutoa huduma kwa Wananchi.

Mtambo alisema ,imepita muda mrefu ,fedha hizo zipo Lakini hakuna muendelezo wa ujenzi, swali ambalo lilimuibua mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Mshamu Munde na kusema awali zikitoka milioni 500 ambazo zimeshafanyiwa kazi.

Munde alibainisha kwamba ,milioni 800 ni fedha nyingine ambazo zipo kwenye hatua ya Ununuzi na kuanzia wiki ijayo zitafanyiwa kazi kulingana na maelekezo ya fedha hizo kwenye Maeneo ambayo ujenzi unaendelea ili kukamilisha hospital hiyo.

Alisema ,kamati ilihofia kutoa fedha kutokana na tatizo la maji ,Lakini alikaa nao na kuwaambia maji Ni moja ya vifaa vinavyotumika kwenye ujenzi hivyo haiwezekani ujenzi ukasimama kutokana na malipo ya maji.