Thursday, December 5, 2019

DC, MSHAMA ATAKA WANAFUNZI WASICHANA WANAOPATA MIMBA WACHUKULIWE HATUA.

NA MWAMVUA MWINYI,KIBAHA

MKUU wa wilaya ya Kibaha ,mkoani Pwani ,Assumpter Mshama ameeleza iko haja ya kuwa na usawa wa kijinsia kwa watoto wa kike na wa kiume pindi mwanafunzi wa kike anapopata mimba akiwa shuleni, ili iwe fundisho kwa wanafunzi wengine .


Ameeleza, inapaswa mtoto wa kike nae achukuliwe hatua sawa na mtoto wa kiume kwani ujauzito hautokani na upande mmoja bali ni ushirika wa watu wawili wa jinsia mbili tofauti.


Akizungumza katika  mahafali ya wanafunzi wa chuo cha ufundi stadi VETA Pwani, pamoja na mambo mengine, Mshama alisema ifikie hatua kila mwanafunzi apate adhabu sawa baada ya kupeana mimba ili kukomesha tabia hiyo.


“Kwa wilaya hii wote mtapata adhabu, haiwezekani mtoto wa kike aendelee kutamba wakati muda mwingine unakuta mtoto huyo ndio alikuwa chanzo cha kumtongoza mwalimu au mwanafunzi mwenzie, hamjawahi kuona hilo!,  Alihoji Mkuu huyo wa wilaya.


Aidha Mshama alishauri Vijana hao waliomaliza chuo cha ufundi stadi VETA,   kujiajiri kwa kufungua  viwanda vidogo vidogo na kutengeneza vifaa vyenye ubora ili waweze kupambana na tatizo la ukosefu wa ajira.


Mapema wakisoma risala yao mbele ya mgeni rasmi wanachuo ZAHARA ABDUL na IDD ATHUMANI waliiomba serikali ya mkoa huo, kutoa kipaumbele cha ajira na fursa mbalimbali zilizoko ndani ya mkoa.

Nae kaimu mkuu wa chuo hicho, Karim aliainisha changamoto kubwa inayoikabili chuo ni upungufu wa mabweni.

ZAIDI YA WATOTO 14,000 BAGAMOYO KUPATIWA VYETI VYA KUZALIWA.

Image may contain: 4 people, people smiling, people sitting
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Fatuma O. Latu, amefungua rasmi mafunzo kwa wataalamu watakaoendesha zoezi maalumu la uandikishaji na usajili wa watoto wenye umri chini ya miaka mitano ili wapatiwe vyeti vya kuzaliwa bure.

Mafunzo kwa Wataalamu wasajili hao yamelenga kuwajengea uwezo ili kutekeleza mpango wa usajili wa watoto kwa kasi inayotakiwa na kwa ufanisi mkubwa.

“Ni wajibu wenu kuhakikisha zoezi hili mnalitekeleza kwa weledi mkubwa, ili muisaidie Serikali kupata takwimu sahihi zitakazoisaidia kupanga shughuli za maendeleo katika Halmashauri yetu ya Bagamoyo, hivyo umakini mkubwa unatakiwa wakati wa mafunzo ili kupata uelewa sahihi wa kutekeleza zoezi” Amesema Bi. Fatuma Latu


Anaongeza “Kila mtoto ana haki ya kusajiliwa na kupata cheti cha kuzaliwa kwani cheti hiki kina umuhimu mkubwa, ikiwa ni pamoja na kumtambulisha mtoto wakati wa kupata huduma muhimu za kijamii, mfano; wakati wa kuandikishwa shule, kuingia chuo kikuu, wakati wa kujiandikisha ili kupata kitambulisho cha Taifa, kuomba pasipoti ya kusafiria na matumizi mengine mengi muhimu, hivyo ni wajibu wa kila mzazi kuhakikisha anatumia fursa hii kuhakikisha mtoto wake anasajiliwa na kupatiwa cheti cha kuzaliwa”


Jumla ya watoto 14,565 wanatarajiwa kusajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa kupitia mpango huu maalumu katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, ambapo zoezi la usajili wa watoto ili kupatiwa vyeti vya kuzaliwa linatarajiwa kuanza siku ya tarehe 06/12/2019 na litaendelea hadi tarehe 19/12/2019.


Usajili huu wa watoto utafanyika katika Ofisi za Kata zote 11 za Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, pia katika Vituo vya kutolea huduma za Afya, ambavyo ni Zahanati zote, Vituo vya Afya na katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, ambapo Mzazi anatakiwa kufika katika Vituo hivyo vya usajili akiwa na nakala (copy) ya kadi ya kliniki au tangazo la mtoto kuzaliwa ili kufanya usajili huo.

Mpango wa usajili na utoaji vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano katika Mkoa wa Pwani, unatekelezwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya watu wa Canada, Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia watoto (UNICEF) pamoja na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA).

Tuesday, November 26, 2019

Korea, Tanzania yajadili Geospatial information, Tanzania kunufaika na mpango huo


Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani Wizara ya Ardhi Hamdounny Masour akisoma hotuba katika ufunguzi wa wa mkutano wa siku mbili wa Geospatial Information Road Show uliowakutanisha wataalamu wa masuala ya ardhi kutoka nchini Korea na Tanzania.


Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania Tae Ick Cho akitoa hotuba yake katika ufunguzi wa wa mkutano wa siku mbili wa Geospatial Information Road Show uliowakutanisha wataalamu wa masuala ya ardhi kutoka nchini Korea na Tanzania unaofanyika kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es salaam.







Imeelezwa kuwa matumizi ya teknolojia hasa ICT yana tija sana katika kuyafikia maendeleo.

Hayo yamebainishwa katika mkutano wa siku mbili wa Geospatial Information Road Show uliofanyika jijini Dar es salaam ambao uliwakutanisha wataalamu wa masuala ya ardhi kutoka nchini Korea na Tanzania.

Akizungumza katika kikao hicho, Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania Tae Ick Cho amesema Teknolojia bora katika kukuza uchumi ndiyo  silaha kubwa na pekee ya kimaendeleo na yenye kuleta ushindani katika soko la dunia na hilo litafanikiwa kam ataifa litajikita zaidi katika kuwekeza katika teknolojia.

 Amesema bila hiyo hatutaweza kushindana na mataifa mengine yenye teknolojia ya juu, tukumbuke msemo wa ukiona vyaelea ujue vimeundwa , hivyo hatuwezi kuendelea bila ya kuweka mbele teknolojia, kushirikiana na kuondoa vikwazo



Amesema kwa muda mrefu Tanzania na Korea Kusini zimekuwa na ushirikiano wa hali ya juu hasa katika masuala ya biashara zilizoruhusu kuvuka mipaka na hiyo yote ni kwa malengo ya kukuza uchumi baina ya nchi hizo mbili.

Pia amesema tangu kuanzishwa kwa Geospatial Information Road Show malengo makuu ni pamoja na kuendesha semina za kiteknolojia katika usajili ardhi, mikutano ya biashara baina ya Serikali ya Tanzania Makampuni wakilishi ya Korea yaliyopo nchini pamoja na kupeana taarifa mbalimbali katika masuala ya ardhi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa upimaji na ramani kutoka Wizara ya Ardhi Hamdounny Masour amesema faida ya mkutano huo ni kwamba Taifa litaidika na taarifa mbalimbali ambazo wataalamu hao wanazo.

Amesema kupashana habari na kubadilishana uzoefu baina ya kampuni kutoka Korea na Tanzania ni moja katika ya hatua kubwa ambayo itasaidia nchi hizo mbili kufikia malengo.

Masour amesema kuwa kupitia mkutano huo wataendelea kudumisha ushirikiano huo pamoja na kupeana taarifa za kisekta katika masuala ya upimaji wa ardhi.

“Ushirikiano baina ya nchi hizo mbili umekuwa wa kindugu na kupitia Geospatial Information Road Show na Wizara ya Ardhi tutaendelea kupeana taarifa za kisekta ili kuweza kuyafikia maendeleo” ameeleza.

Mkutano huo uliodumu yangu 2013 umewakutanisha wadau kutoka Wizara ya Ardhi nchini pamoja na Wizara ya Ardhi, miundombinu na usafiri kutoka Korea pamoja na wataalamu mbalimbali yakiwemo makampuni makubwa 12 kutoka nchini Korea.



Thursday, November 21, 2019

Serikali yasisitiza udhibiti magonjwa yasiyoambukiza





Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Juliana Shonza akifungua tamasha la michezo la wiki ya kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ambukiza Novemba 9, 2019 jijini Dodoma ambapo kilele chake ni Novemba 14, 2019.


Na Eleuteri Mangi, WHUSM, Dodoma



Michezo ni nyenzo madhubuti katika kulinda afya za wanadamu kwa kuwajengea uimara na ustahimilivu, kukuza stadi za kijamii kiubunifu na kiuongozi ili kuwawezesha wanamichezo na watu wote kujifunza vitu vipya vinavyoweza kuchangia kutunza afya zao ili waweze kujiletea maendeleo yao wenyewe na taifa kwa ujumla.

Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 inatambua umuhimu wa michezo ikiwemo kuhamasisha Umma wa Watanzania kushiriki katika michezo na mazoezi ya viungo. Kwa kutambua jambo hilo, Serikali imewezesha upatikanaji wa viwanja na vifaa vya michezo vilivyo bora na vya kutosha kwa ajili ya kuimarisha maendeleo ya michezo nchini.  

Kama taifa, kumekuwa na mtazamo chanya kwa viongozi kuthamini michezo kuanzia ngazi ya Serikali Kuu hadi Serikali za Mitaa kupitia mikoa, wilaya, tarafa, kata, vijiji, mitaa na vitongoji.

Kwa kulitambua na kulithamini suala la michezo kwa watu wa rika zote kuwa ni muhimu kwa afya, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan mwaka 2016 alipokuwa akizindua kampeni ya kitaifa ya kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwenye viwanja wa Leaders Club jijini Dar es Salaam aliagiza watu katika maeneo yao nchini kushiriki kufanya mazoezi ambayo ni sehemu ya michezo.

Ili utaratibu wa kufanya mazoezi uwe endelevu, Makamu wa Rais alisisitiza “……….kila Jumamosi ya pili ya mwezi itakuwa siku ya mazoezi kwa afya, kwa sababu mazoezi ni afya na nawaasa wananchi kufanya mazoezi na kuanzisha na kujiunga na vikundi vya mazoezi na Serikali itatimiza wajibu wake wa kuweka mazingira mazuri ya kufanyia mazoezi kote nchini.”

Wananchi wamekuwa na mwitikio mkubwa katika kulifanyia kazi agizo hilo kwa kuweka utaratibu wa kufanya mazoezi ambao umeongeza idadi ya vikundi vya mazoezi ya pamoja katika maeneo mbalimbali ya nchini. 

Hamasa ya kufanya mazoezi sasa imekuwa nzuri ambapo Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto zimeanzisha utaratibu wa kuwa na bonanza, matamasha ya michezo pamoja na vilabu vya kufanya mazoezi. Hatua hii imekuwa ni chachu mpya ya kutekeleza agizo la Makamu wa Rais Mama Samia la kufanya mazoezi kwa manufaa ya afya za Watanzania.

Akiwasilisha Bungeni hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2019/2020 ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Waziri mwenye dhamana ya wizara hiyo Dkt. Harrison Mwakyembe aliliambia bunge na Watanzania wote kuwa, miongoni mwa majukumu ya sekta ya michezo ni kuratibu na kusimamia maendeleo ya michezo nchini ikiwa ni pamoja na kuimarisha ushiriki wa wananchi katika michezo.

Mojawapo ya vitu vinavyoshirikisha watu wengi kujiunga na kufanya mazoezi ni kuwa na matamasha ya michezo mbalimbali ambayo yanalenga kuhamasisha wananchi kushiriki katika michezo ikiwa ni pamoja na kufanya mazoezi ya viungo ili kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ambayo yamekuwa yakiongezeka kwa kasi  hapa nchini.

Magonjwa hayo hutokana na mitindo isiyofaa ya maisha kama matumizi ya tumbaku, lishe duni, matumizi ya pombe kupita kiasi, pamoja na kutoshughulisha mwili au kutofanya mazoezi ya viungo mara kwa mara. Magonjwa kama kisukari, shinikizo la juu la damu, magonjwa ya moyo na mishipa, saratani, pumu na magonjwa ya akilini miongoni mwa magonjwa hayo, ambapo yasipodhibitiwa huwa na sugu na yenye kuhitaji gharama kubwa kuyatibu.

Hapo awali, magonjwa hayo yalikuwa yakiwaathiri watu wenye umri mkubwa zaidi ya miaka 45, lakini kwa sasa yanazidi kuathiri watu watu wengi wakiwemo watoto wenye umri mdogo.

Naibu Wiziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza hivi karibuni akiwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa tamasha la michezo la wiki ya kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza lililofanyika Novemba 09, 2019 katika uwanja wa Jamhuri Dodoma alihimiza watu kuchukua uamuzi wa kufanya mazoezi ili kujenga afya zao.

“Mazoezi ni jambo lolote linalohusisha misuli na kusababisha kuongezeka kwa mapigo ya moyo na kasi ya kupumua. Wataalam wa afya wanasema kuwa kiwango cha mazoezi kinacholeta faida ni mazoezi yasiyopungua dakika 30 kwa siku angalau siku tatu kwa wiki na yanayomfanya mtu kutokwa na jasho” alisisitiza Naibu Waziri Shonza.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri Shonza watumishi wanaofanya kazi ofisini wametakiwa kuongeza bidii ya kufanya mazoezi kulingana na mtindo wa maisha ya mtumishi mmoja mmoja kuendana na hali yake ya maisha.

Kwa watumishi wa umma na sekta binafsi pamoja na watu wengine wanaotumia magari, wanapaswa kupanga shughuli ambazo zitawafanya kila siku watembee kwa miguu, wanaoishi au kufanya kazi ghorofani wajitahidi na wajizoeshe kutumia ngazi kila siku badala ya lifti, mtu anapokwenda mahali popote watumie njia ndefu kutembea badala ya njia ya mkato pamoja na kupunguza muda wa kutazama televisheni, badala yake muda huo utumike kufanya shughuli zinazotumia viungo vya mwili kama kufua, kuosha vyombo, kuosha gari, kusafisha nyumba, kazi za bustani na kufyeka majani ambazo zinasaidia kujenga utimamu wa mwili.

 Naibu Waziri Shonza ametoa rai kwa  waajiri kuboresha mazingira ya kazi kwa kuhakikisha watumishi wao wanashiriki katika michezo na kufanya mazoezi hata maeneo yao ya  kazi na kutoa mfano wa kuanzisha timu mbalimbali za michezo na kutenga siku maalum katika mwezi kwa ajili ya mabonanza ya michezo. Mazingira rafiki ya kufanyia mazoezi kazini ni pamoja kutenga vyumba vya mazoezi na na kununua vifaa vya michezo. Hatua hiyo itaimarisha afya za watumishi na kupunguza gharama za matibabu katika taasisi husika.

Aliongeza kuwa ili kufanya mazoezi kuwa endelevu, maafisa michezo na utamaduni wa mikoa na wilaya wana wajibu wa kuongeza uhamasishaji na uundaji wa vikundi vya mazoezi ya pamoja katika maeneo yao.

Wizara nyingine zenye uhusisano na mchango katika kufananikisha wananchi kufanya mazoezi ni Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Wizara hizo zina mamlaka ya kusimamia na kuweka mazingira bora ya watu kufanya mazoezi kwa kuendelea kutenga viwanja vya michezo na kuzuia uuzaji wa maeneo ya wazi hususani viwanja vya michezo na kuboresha barabara za waenda kwa miguu na baiskeli ili kuhamasisha watu kutembea na kuongeza usalama wa mazoezi.

Aidha, mamlaka  za  usafiri, zinawajibu wa kuboresha usafiri wa jumuiya ili kuongeza idadi ya watu wanaotumia usafiri wa jumuiya kwa sababu tafiti nyingi zinaonesha kuwa utumiaji wa usafiri wa jumuiya unaongeza uwezekano wa kutembea na kufanya mazoezi na hivyo kupunguza magonjwa yasiyoambukiza.

Matamasha ya michezo pamoja na matamasha mengine yakiwemo ya utamaduni yanatakiwa kuwa kichocheo cha kushirikisha vitu vingi ikiwemo michezo ya jadi na mashindano ya baiskeli katika maeneo mbalimbali ambayo yana mchango mkubwa katika kutunza afya za washiriki wa michezo hiyo.

Wakati wa matamasha hayo, ni vema wananchi wahamasishwe kupima afya zao hususani wa magonjwa yasiyoambukiza kwani tiba ya mapema ina manufaa kwa kuwa inapunguza uwezekano wa watu kupatwa na madhara zaidi. Hatua hiyo inaweza kuondoa magonjwa hayo moja kwa moja. Ili kuongeza hamasa ya wananchi na wanamichezo kupima afya zao, upimaji huo unapaswa kuwa ni wa bure ili watu wengi zaidi wapate fursa ya kupimwa.

Hivi karibuni Shirika la Afya Duniani (WHO) limetoa mwongozo wa kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza ambapo mataifa yameazimia kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu, (SDGs) ili kupunguza kwa theluthi moja vifo vya mapema vitokanavyo na magonjwa yasiyo ya kuambukiza ifikapo mwaka 2030.

Akizungumzia mwongozo huo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Tedros Adhanon Ghebreyesus alisema, “Zaidi ya nusu ya watu duniani wanaishi mijini, na idadi yao inaongezeka. Viongozi wa miji wanapaswa kuchukua maamuzi ambayo yataboresha afya za wakazi wao, ili miji iweze kuchipua na kustawi. Kila mtu anapaswa kupata huduma ambazo zitaboresha afya, huduma za usafiri wa umma ziwe salama, makazi ya nje yawe safi na salama, mlo uwezo mzuri na huduma za afya ziwe bora.”

Naye Balozi wa WHO katika kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza (NCDs) na majeraha, Michael Bloomberg alisema kuwa shirika hilo lipo mstari wa mbele katika kusambaza mikakati hiyo duniani kote ili kuokoa maisha ya mamilioni ya watu.

“Tunafanya kazi kuhamasisha uelewa miongoni mwa viongozi wa miji na watunga sera kuhusu manufaa halisi yanayoweza kupatikana pindi programu hii ya kuboresha miji inapofanya kazi.” alisisitiza Balozi Bloomberg.

Ni kweli, wataalamu wa afya wanashauri kuwa ni vema kila mtu awajibike kuitunza afya yake kwa kufuata mtindo bora wa maisha kwani afya njema ni msingi wa maendeleo. Hatua hii inaunga mkono kauli mbiu tamasha la michezo la wiki ya kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ambukiza inayosema “Tutembee pamoja katika kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza.”



CHUO CHA KFDC KIBAHA CHAJIVUNIA MAFANIKIO



Mkuu wa chuo cha maendeleo ya wananchi Kibaha (KFDC) Joseph Nchimbi akizungumza na wazazi, wanafunzi na viongozi mbali mbali wa serikali ambao walihudhulia katika mahafali ya kuwaga wanafunzi wa chuo hicho yaliyofanyika mjini Kibaha.(PICHA NA VICTOR MASANGU)

NA SCOLASTICA MSEWA, KIBAHA


CHUO CHA Maendeleo ya Maendeleo ya wananchi Kibaha chajivunia mafanikio  kwa kupanua wigo wa udahili wa wana chuo kutoka Mikoa yote Tanzania.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Kibaha Joseph Nchimbi wakati wa mahafali  ya chuo hicho ambapo jumla ya wanachuo 142 wamehitimu kati yake wanawake 42 na wanaume 100.

" Chuo chetu cha KFDC kimepiga hatua kubwa katika kutoa mafunzo bora na kufanya vijana wengi kuomba nafasi katika chuo hiki ,kwa kipindi cha miaka mitatu kimeweza kudahili wanafunzi wengi na kufanya vizuri"  alisema Joseph 

Joseph alisema mafanikio mengine ambayo wanajivunia wanachuo wote ambao wametoka katika chuo hicho wamepata ajira serikalini ,sekta binafsi na wengine wamejiari wenyewe sekta binafsi kutokana na ujuzi waliosomea chuoni ikiwemo ufundi umeme ,ufundi magari ufundi uchomeleaji na uundaji vyuma.

Aidha alisema idadi ya wakufunzi kila siku wanaongezeka waliohamia katika chuo hicho hivyo kupunguza uhaba wa wakufunzi waliokuwepo hapo awali wanaendelea kupata huduma bora kutoka kwa Wakufunzi wa Shirika la Elimu Kibaha.

Joseph alisema Chuo cha Maendeleo Kibaha (Kibaha Folk  Development College )kilianzishwa mwaka 1964  kikijulikana kama Farmers Training Centre  chini ya mradi wa pamoja wa serikali ya Tanganyika na nchi ya za Nordic uitwao  Tanganyika Nordic Project.

Alisema katika chuo  hicho kuna fani mbalimbali kwa ajili ya kujifunza  ikiwemo ufundi selemala,ufundi ushonaji,ufundi uashi,ufundi bomba,kilimo,mifugo na hotelia.

Joseph alisema chuo   hicho kinachangia nguvu  kazi muhimu inayohitajika katika uchumi wa viwanda uwezo wa chuo kuchukua wanachuo 500 lakini kwa sasa chuo kina wanafunzi 295 .

Kwa upande wake Mwanafunzi wa Chuo hicho cha Maendeleo ya Wananchi, Emanueli Leonard alisoma risala ya wanachuo wanaohitimu mwaka wa pili alielezea changamoto za chuo hicho ikiwemo uchakavu wa majengo,upungufu wa kompyuta,ukosefu wa jengo la kompyuta,uchakavu wa karakana za kujifunzia na ukosefu wa jengo la kujifunzia

Naye mgeni rasmi  Mjumbe wa Bodi wa shule hiyo   Elisante Ngure alipongeza Serikali kwa kuvitunza vyuo vya ufundi vilivyopo hapa nchini .

Ngure aliwataka wana chuo waliohitimu chuoni hapo watumie elimu waliopata kwa kujiongezea ajira na kuzingatia nidhamu kwani nidham ndio siri ya mafanikio  pia wajenge   umoja na  mshikamano .

Aliwataka vijana kuchangamkia fursa katika kukopa mikopo ya Serikali ambayo inatolewa ngazi ya halmashauri ya Wanawake Vijana na Watu Wenye ulemavu.