Thursday, November 21, 2019

Rais Dkt. Magufuli Amestahili PhD ya Heshima








Na Mwandishi Wetu-Dodoma

Utendaji mzuri katika eneo lolote ni tunu na uwezo wa kuleta mageuzi ya kweli kwenye jamii yoyote ile inayolenga kupiga hatua  kufikia maendeleo endelevu yanayotokana na Dira ya Maendeleo iliyowekwa na jamii husika.

Kufikiwa kwa malengo hayo katika nchi yetu kunatokana na uongozi madhubuti  na utendaji  mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwekeza vyema katika Sekta ya Elimu, Nishati, Maji,Uchukuzi, Mawasiliano na Afya.

Msingi wa Mafanikio yaliyofikiwa katika kipindi cha miaka minne yanatokana na aina ya uongozi wa Rais Magufuli wa kuzingatia kuwapo kwa ushahidi wa mahusiano chanya kati ya  “Kiongozi na Matokeo”  sambamba na ukuaji wa uchumi.

Hivyo Basi, uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika sekta ya elimu umeonesha mafanikio makubwa kupitia Mpango wa Elimu Msingi (Basic Education) bila malipo wenye lengo la kuhakikisha kuwa kila mtoto wa Tanzania mwenye sifa ya kwenda shule anapata haki ya kupata elimu bila kikwazo cha ada na michango mingine.

Katika kukuza sekta hii Chuo Kikuu cha Sokoine kilipatiwa matrekta 10 mapya ili kufundishia wataalamu wa kilimo,katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kulifanyika ujenzi wa mabweni,halikadhalika mikopo kwa wanafunzi wa wa Elimu ya Juu imeongezwa hadi shilingi bilioni 450 kwa mwaka 2019/ 2020 ikilinganishwa na shilingi bilioni 427.5 zilizotengwa mwaka 2018/2019.

Hatua nyingine ni pamoja na ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi unaoendelea katika wilaya nyingi hapa nchini, ujenzi wa madarasa, matundu ya vyoo,maabara na miundombinu mingine ya sekta hii imechangia kukuza kiwango cha elimu.

Katika sekta ya nishati Rais Magufuli amewezesha kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa kufua umeme wa  maji katika mto Rufiji unaojulikana kama mradi wa kufua umeme wa  Mwalimu Nyerere utakaozalisha megawati 2115, hapa Mhe. Rais amewahi kunukuliwa akisema “Umeme ni Maendeleo, ni kichochea muhimu cha ukuaji wa uchumi kwa taifa lolote,bila ya kuwepo kwa umeme wa uhakika ndoto yetu ya kujenga uchumi wa viwanda haitatimia.”

Sekta ya uchukuzi nayo haikuachwa nyuma kupitia utekelezaji wa miradi ikiwemo ujenzi wa Reli ya Kisasa kwa kipande cha Dar es Salaam hadi Morogoro umefikia asilimia 70 na kipande cha Morogoro Makutopora unaendelea kwa kasi na umefikia asilimia 20 , mradi huu umetoa ajira kwa watanzania wapatao 6,335 sawa na asilimia 90 ya wafanyakazi wote.

Kukamilika kwa mradi huu kutachangia kasi ya ukuaji wa uchumi wa nchi kuongezeka na hivyo ustawi wa wananchi utaleta tija katika uzalishaji.

Uboreshaji wa miundombinu ya Bandari ya Dar es Salaam mwaka 2018/2019 unaendelea na unalenga kuifanya kuwa ya kisasa na kuwa na gati zenye uwezo wa kuhudumia meli nyingi  na kubwa zaidi ya ilivyokuwa awali, kwa sasa gati namba 1 hadi 7 zimeboreshwa na ujenzi wa gati jipya la kuhudumia meli zilizobeba magari umefikia asilimia 65.

Bandari ya Tanga na Mtwara nazo zimeboreshwa na kuongeza uwezo wa kuhudumia meli kubwa na kwa idadi kubwa zaidi, usafiri katika maziwa yote nchini umeimarishwa kwa kujengwa kwa meli mpya na kukarabatiwa kwa zile zilizopo hivyo wananchi wanaotegemea usafiri huo katika ziwa Tanganyika, Victoria na Nyasa wameongeza kasi ya shughuli za kiuchumi.

Baadhi ya Miradi inayoendelea  katika sekta ya  uchukuzi ni pamoja na ile ya ujenzi wa  barabara za juu kwenye makutano ya Ubungo, upanuzi wa barabara ya Kimara Mwisho hadi Kibaha Km 19.2 kutoka njia mbili hadi njia nane, ujenzi wa daraja jipya  la Salenda na miundombinu ya mradi wa mabasi yaendayo kasi Awamu ya II na III.

Kufikia mwezi Februari 2019, jumla ya miradi 65 ya maji vijijini ilikamilishwa ambapo wananchi milioni 25.36 waishio katika vijiji hivyo wamenufaika kwa kupata maji safi na salama,hali hiyo inaendana na malengo  ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa.

Katika kusimamia rasilimali za nchi Rais Magufuli amewezesha kutungwa kwa sheria kwa ajili ya usimamizi thabiti wa rasilimali ya madini, Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusu Umiliki wa Maliasili Na.5 ya mwaka 2017 na Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi No.6 ya mwaka 2017 pamoja na kufanya marekebisho ya Sheria ya Madini sura ya 123.

Kwa upande wa Sekta ya Kilimo inayoajiri wananchi takribani asilimia 75 hadi 80 ambapo kwa kutambua umuhimu wa sekta hii Rais Magufuli alizindua Programu ya kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II). Programu hii inalenga kuleta mageuzi katika sekta hii kwa maana ya mazao, mifugo na uvuvi ili kuongeza uzalishaji na tija, kufanya  kilimo kiwe cha kibiashara na kuongeza pato la wakulima hususan wakulima wadogo kwa ajili ya kuboresha maisha na usalama wa chakula na lishe.

Kwa kuwa Rais Dkt. Magufuli amewezesha ujenzi wa vituo vya afya 352 na hospitali za wilaya 67 na hospitali za kanda zinaendelea kujenga ni wazi kuwa mchango wake katika kuboresha maisha ya wananchi unamfanya kuwa  na sifa za kutunukiwa shahada hii. Hakika usemi wa wahenga usemao chanda chema huvikwa pete leo umetimia kwa Mhe. Rais Magufuli kutunukiwa Shahada ya Sayansi ya Udaktari wa Falsafa.



Mwisho.












Tuesday, November 19, 2019

Soma tamko la pamoja la kutoka mtandao wa kutokomeza ndoa za utotoni (TECMN), waipongeza mahakama ya rufaa


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


TAMKO LA PAMOJA KUTOKA MTANDAO WAKUTOKOMEZA NDOA ZA UTOTONI TANZANIA KUIPONGEZA MAHAKAMA YA RUFAA YA TANZANIA



Mtandao wa Kutokomeza Ndoa za Utotoni Tanzania (TECMN), unaojumuisha mashirika na Asasi zisizo za kiserikali zaidi ya 50 ukiratibiwa na Shirika la Jukwaa la Utu wa Mtoto kwa Sauti Moja tunapongeza Mahakama ya Rufaa ya Tanzania   kwa uamuzi wake wa kubatilisha kifungu namba 13 na 17 vilivyopo kwenye sheria ya ndoa  No. 5 ya mwaka 1971 (Sura 29).

Mtandao wa Kutokomeza Ndoa za Utotoni kwa muda mrefu tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012 umekuwa ukifanya jitihada na mikakati mbalimbali ya uhamasishaji na uelimishaji juu ya athari ya ndoa za utotoni na kwa vipindi tofauti wanachama wa mtandao wamekuwa wakifanya tafiti mbalimbali kuonesha ukubwa wa tatizo la ndoa za utotoni na visababishi vyake ambavyo ni pamoja na umasikini, mila na desturi pamoja na sheria ya ndoa ya mwaka 1971 kifungu cha 13 and 17 ambayo inaruhusu mtoto wa kike kuolewa kuanzia umri wa miaka 14.

Kwa nyakati tofauti Mtandao umeweza kuhamasisha jamii, wanahabari, viongozi wa dini, viongozi wa kimila na viongozi wa serikali katika ngazi tofauti ili wachukue hatua au washirikiane na Mtandao katika jitihada za kutokomeza ndoa za utotoni pamoja na kuunga mkono jitihada za mtandao za mabadiliko ya sheria ya ndoa ya mwaka 1971.

Katika kuhakikisha tatizo la ndoa za utotoni na mabadiliko ya sheria ya ndoa yanatekelezwa ili kulinda haki na ustawi wa mtoto wa kike; Mtandao uliweza kufanya mazungumzo na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Kamati ya Katiba na Sheria, Kamati ya  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Umoja wa Wabunge Wanawake Bungeni. Vilevile katika vipindi tofauti, Mtandao uliweza kufanya mazungumzo na  Spika wa Bunge, Naibu Spika na Mwanasheria Mkuu wa Serikali zikiwa ni harakati za kutafuta kuungwa mkono jitihada za Mtandao unaolenga kuleta mabadiliko chanya yatakayomnusuru mtoto wa kike dhidi ya ndoa za utotoni.



HALI YA NDOA ZA UTOTONI TANZANIA IKOJE KWA SASA?

1.      Tanzania ni moja ya nchi zenye kiwango cha juu cha ndoa za utotoni duniani. Kwa mujibu wa takwimu za UNICEF za kati ya mwaka 2010 na 2017, Tanzania ni ya tatu kwa kuwa na viwango vya juu vya ndoa za utotoni baada ya Sudan Kusini na Uganda. Sudan Kusini kiwango cha watoto wa chini ya miaka 18 wanaoozwa ni asilimia 52 na nchini Uganda ni asilimia 40. Tanzania ni asilimia 31. Nchini Kenya, ni watoto asilimia 23 wanaoozwa kabla ya kutimiza miaka 18.

2.      Kwa wastani, kati ya watoto watano (5) wakike wawili (2) huolewa kabla ya umri wa miaka 18. Utafiti wa afya na watu (TDHS 2015) unaonesha kuwa asilimia 31% ya wanawake kati ya umri wa miaka 20 – 24 waliolewa wakiwa na umri wa chini ya miaka 18.

3.      Takwimu za ndoa za utotoni kimkoa; Shinyanga (59%), Tabora (58%), Mara (55%), Dodoma (51%), Lindi (48%), Mbeya (45% -), Morogoro (42%), Singida (42%), Rukwa (40%), Ruvuma (39%), Mwanza (37%), Kagera (36%), Mtwara (35%), Manyara (34%), Pwani (33%), Tanga (29%), Arusha (27%), Kilimanjaro (27%), Kigoma (26%), Dar es Salaam (19%) na Iringa (8%).

4.      Ndoa za utotoni kwa hapa Tanzania huathiri zaidi watoto wa kike kwani kwa wastani wanawake wengi huolewa mapema zaidi kwa tofauti ya umri wa miaka 5 wakilinganishwa na wanaume.



UAMUZI WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA KUHUSU MABADILIKO YA SHERIA YA NDOA YA MWAKA 1971 KIFUNGU NAMBA 13 NA 17

Baada ya kusubiri kwa muda mrefu,  hukumu ya mahakama iliyokatwa na serikali Julai 8, 2016 kupinga kesi ya kikatiba iliyofunguliwa  na Rebeca Gyumi (Mwanachama wa Mtandao-Msichana Initiative) ya kupinga sheria ya ndoa ya mwaka 1971 kifungu namba 13 na 17, hatimaye, tarehe 23 ya mwezi Julai mwaka 2019 Mahakama ya Rufaa ya Tanzania ilikubaliana  na maamuzi yaliyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania kubadilisha vifungu hivyo kwa kua ni vya kibaguzi na vinakiuka haki ya kikatiba ya kujieleza kwakua mtoto mwenye  umri wa miaka 14 hawezi kuingia katika mkataba wa ndoa kwa kuwa hana  ufahamu kiasi cha kuweza kujihusisha na mkataba wa ndoa na kuiamuru serikali kuibadilisha sheria hiyo ndani ya mwaka mmoja kumruhusu mtoto wa kike kuolewa akiwa na umri kuanzia miaka 18. .

Hukumu hii ni ushindi kwa watoto wa kike wa Tanzania kwani imewapa ulinzi wa kisheria, pia hii ni hatua muhimu sana kwetu sisi kama mashirika na wadau mbalimbali wa maendeleo ya jamii tunayopigania haki za watoto wa kike kwa kuona hatua ya kwanza inayopelekea watoto wa kike kupata haki zao za msingi kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Watoto wa kike wa Tanzania wapo huru kisheria  kilichobaki ni kuunganisha nguvu zetu kwa pamoja katika kuhakikisha tunatoa elimu kwa wadau, viongozi, Jamii na watoto kwa ujumla kwa lengo la kuwaelimisha wahusika wote juu ya sheria hii na athari zinazotokana na ndoa za utotoni ili kuwasaidia na kuwalinda watoto wa kike wafikie malengo na ndoto zao za kielimu.

Katiba ya Tanzania inasema  binadamu wote huzaliwa huru, na wote ni sawa na kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake (Ibara ya 12 (1)). Inaeleza zaidi kwamba watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya yeyote miongoni mwao kubaguliwa, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria. Sheria zinazoweka umri wa chini tofauti wa kuoa au kuolewa baina ya mvulana na msichana ni za kibaguzi na zinakiuka haki ya usawa mbele ya sheria.



ATHARI ZA NDOA ZA UTOTONI

Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inaruhusu ndoa za utotoni. Inakadiriwa kwamba asilimia 37 ya wasichana Tanzania wanaolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18. Umasikini, mila za kijamii na kiutamaduni, unyanyasaji wa kijinsia,  , vyote hivyo vinachangia ndoa za utotoni.



ATHARI YA NDOA ZA UTOTONI

·         Kupoteza fursa za elimu na ujuzi wa kazi

·         Kupata maambukizo ya virusi vya ukimwi (VVU) au magonjwa ya zinaa (STD)

·         Kunyanyasika kisaikolojia, kimwili, kijinsia

·         Kuyumba kiuchumi na kudumu katika umasikini,

·         Kukosa au kushindwa kujitawala

·         Unyanyasaji wa kimwili  unyanyasaji wa maneno

·         Vifo vya watoto wachanga na watoto wa kike pindi wanapojifungua kwa kuwa viungo vyao vya uzazi bado havijakomaa

·         Vifo vya wajawazito

·         Kuharibika kwa mimba





SHAURI LA REBECA GYUMI

Baada ya kuona changamoto zote wanazokutana nazo watoto wa kikekatika suala zima la kuolewa wakiwa na umri chini ya miaka 18, Rebeca Gyumi alifungua shauri kwa niaba ya watoto wa kike  walio katika hatari ya kuingia kwenye ndoa za utotoni. Shauri la Rebeca Gyumi dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Katika Shauri la Madai Na.5 ya 2016 (Shauri la Rebeca Gyumi) lilipinga uhalali wa kikatiba wa ndoa za utotoni. Matokeo yake ni kwamba mahakama kuu Tanzania ilitamka kwamba vifungu vya 13 na 17 vya sheria ya ndoa ni vya kibaguzi na vinakwenda kinyume na katiba.

KUPINGA SHERIA INAYOHUSIANA NA NDOA ZA UTOTONI

Sheria ya Ndoa imeweka vigezo vinavyohitajika kwa watu wanaoingia katika ndoa. Kwa mujibu wa sheria, umri wa chini kwa wasichana kuolewa ni miaka 15 na kwa wavulana ni miaka 18. Kwa mujibu wa kifungu cha 13 cha sheria, wavulana na wasichana wanaweza kuoa au kuolewa mapema zaidi, yaani wakiwa na umri wa miaka 14, kwa idhini ya mahakama na miaka 15 kwa idhini ya wazazi.

Kifungu cha 17 cha Sheria kinaelezea kwamba kwa ndoa ya msichana mwenye umri wa chini ya miaka 18, baba yake ni lazima atoe idhini kuruhusu ndoa hiyo, kama baba yake amefariki, basi mama yake. Kama wazazi wote wamefariki, walezi wake ni lazima watoe idhini. Kama hakuna mlezi , hakuna idhini inayohitajika.

Kwanini Rebeca Gyumi alipinga vifungu vya 13 na 17 vya Sheria hii kwa misingi kwamba:

1.      Vinakiuka Ibara Ya 12(1) ya katiba ya Tanzania, katiba ambayo inatoa usawa kwa watu wote mbele ya sheria;

2.      Vinakiuka Ibara ya 13(1) (2) ya katiba ya Muungano wa Tanzania ambayo inawalinda watu dhidi ya ubaguzi kwa misingi ya kijinsia;

3.      Watu walio chini ya umri wa miaka 18 ni watoto na hawana uwezo wa kufanya mamuzi sahihi juu ya kuoa au kuolewa;

4.      Vinakiuka Ibara ya 21(2) ya Katiba ya Tanzania kwa kutowapa wasichana fursa ya kushiriki kikamilifu katika uamuzi wa kuamua mustakabali wa maisha yao

5.      Vinamnyima mtoto haki ya kupata elimu na uhuru wa mawazo.

Tarehe 8 julai, 2016, Mheshimiwa Jaji Lila J., Mheshimiwa Jaji Kihio J. na Mheshimiwa Jaji Munisi J. walieleza kwamba vifungu vya 13 na 17 vya sheria ya Ndoa vimepitwa na wakati na vinakwenda kinyume na katiba.



MASUALA MUHIMU KWENYE UAMUZI WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA

1.      Ndoa za Utotoni  Zinakwenda Kinyume na Maslahi Muhimu ya Mtoto.

Kwa sababu hiyo, mahakama ilieleza kwamba vifungu vya 13 na 17 vya sheria ya Ndoa vinaruhusu watoto kuingia katika ndoa. Mahakama Kuu ya Tanzania ilieleza kwamba haifai kuwaingiza watoto katika majukumu makubwa ya ndoa. Pia ilidokeza kuhusu hatari kubwa ya kiafya inayowakabili wasichana pale wanapoolewa wakiwa na umri mdogo.

2.      Haki ya Usawa Mbele ya Sheria na Kutobaguliwa kwa Namna Yoyote.

Mahakama ilisema kwamba vifungu hivyo  havitoi usawa kwa wasichana na wavulana katika njia mbili. Kwanza umri wa ndoa ni tofauti kati ya mvulana na msichana. Pili, wasichana chini ya miaka 18 wanahitaji ridhaa ya wazazi kuolewa wakati wavulana hawahitaji. Tofauti hii inaleta maana kwamba, wasichana na wavulana hawatendewi sawa chini ya vifungu vya 13 na 17 vya sheria ya Ndoa. Kwa hiyo, iliamuliwa kwamba vifungu hivyo vinawabagua wasichana na vinakiuka Ibara za 12 na 13 za katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

3.      Sheria ya Kimila na Kiislamu Hazitumiki Kwenye Masuala Yaliyoainishwa Kwenye Sheria Ndoa.

4.      Serikali ilijaribu kutetea sheria zinazoruhusu ndoa za utotoni kwa msingi kwamba ilifanikiwa ili kuziweka kwa pamoja Sheria tofauti za Kimila, Kiutamaduni na Kidini katika ndoa. Mahakama ilikataa hilo kwa maelezo kwamba kifungu cha 11(4) cha Sheria ya Usimamiaji Haki na Matumizi ya Sheria Kinasema. “Kanuni za  sheria za kimila na kanuni za Sheria za Kiislamu hazitatumika katika suala lolote lililoanishwa katika Sheria ya Ndoa”.



5.      Haki ya Kushiriki Katika Maamuzi Yanayogusa Maisha Yako

Mahakama kuu ilibainisha kwamba itifaki ya Maputo inazihamasisha nchi wanachama kutunga sheria ambazo zitahakikisha kwamba hakuna ndoa inayofungwa bila kuwapo uamuzi wa uhuru na ridhaa kamili ya pande zote na kwamba umri wa chini wa mwanamke kuolewa lazima uwe miaka 18.

Kwakua Tanzania imeridhia chombo hicho cha kikanda, umefika wakati sasa wa kuchukua hatua stahiki za kisheria kuhakikisha kwamba haki iliyotolewa chini ya ibara 21(2) ya kikatiba inapatikana kwa wote

6.      Vifungu vya Sheria Havistahili Kutumika Tena

Katika uamuzi wake, Mahakama kuu ilitamka kwamba, vifungu katika Sheria ya Ndoa ambavyo vinaruhusu ndoa za utotoni havistahili kutumika.

Mahakama ilibaini kwamba kumekuwa na maendeleo kadhaa ya kisheria katika sheria ya Ndoa. Maendeleo haya yamefanywa ili pengine kuhakikisha kwamba, “Ustawi na ulinzi wa mtoto wa kike unaimarishwa, na utu na heshima ya mwanamke kwa ujumla vinalindwa”

Kwa mfano, Sheria Maalumu ya Makosa ya Kujamiiana (SOSPA) ya mwaka 1998 imebainishwa adhabu kwa watu wanaojihusisha kimapenzi na watoto. kwa hiyo, kuruhusu ndoa za utotoni ni kama kutoa kibali cha kufanyika kwa uhalifu.

Mahakama iliona kwamba katika sheria kama za SOSPA na Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, Serikali kupitia sheria kama hizo ni kama imekiri kimyakimya kwamba haki ya watoto kulindwa inazidiwa nguvu na haja ya kuendeleza ndoa za utotoni.

Mahakama katika shauri la Rebeca Gyumi iliamuru Serikali kufanya marekebisho ya sheria ndani ya mwaka mmoja na kusahihisha vifungu vya kibaguzi vya 13 na 17 na kuweka miaka 18 kama umri wa chini unaostahili kwa ndoa kwa wavulana na wasichana. Shauri la Rebeca Gyumi ni ushindi wa kipekee kwa mtoto wa kike wa Tanzania. Linaonesha kwamba wanawake wanapaswa kuwa na haki ya kuridhia kuolewa na kwamba, umri wa chini wa kuoa/kuolewa lazima uwe miaka 18 kwa mwanamme na mwanamke. Pia linasisitiza kwamba mila na desturi hazipaswi kutumika kuwabagua wanawake au kuwanyima haki zao.

Tunaipongeza serikali ya Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania kwa kuendeleza jitihada za kuwalinda watoto kwa sheria na sera zinazowalinda watoto wa kike ikiwa ni pamoja na marekebisho yaliyofanywa kwenye sheria ya Elimu ya mwaka 1978 ambayo imeweka vifungu vinavyo zuia watoto wa kike kupewa ujauzito wakiwa shuleni na kutoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 kwa yoyote atakeyepatikana na hatia.  .

Mwisho tunaiomba serikali kutekeleza maamuzi ya hukumu na kubadili vipengele husika.

Ni jukumu letu sote kuchukua hatua kuwalinda watoto na kukemea vikali vitendo vya ndoa za utotoni.



                     KWA SAUTI MOJA TUNASEMA   NDOA ZA UTOTONI SASA BASI !



Tamko hili limetolewa leo tarehe 19/11/2019 na Mtandao wa Kutokomeza Ndoa za Utotoni na kusomwa na Mratibu wa Mtandao.





Kwa Mawasiliano Zaidi:

Michael J. Sungusia

Mratibu wa Mtandao TECMN

Simu +255222775 010 au +255743 902858

Barua Pepe, michael@cdf.or.tz


Rais Magufuli ateua Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa TMA


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

Description: Description: Description: Description: Description: Coat of ArmsKURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

Simu: 255-22-2114512, 2116898
Baruapepe: press@ikulu.go.tz
Tovuti : www.ikulu.go.tz              

Nukushi: 255-22-2113425


OFISI YA RAIS,
      IKULU,
 1 BARABARA YA BARACK OBAMA,  
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ikulu, Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amemteua Dkt. Buruhani Salum Nyenzi kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA).

Dkt. Nyenzi (Tanzania Bara) anashika wadhifa huo kwa kipindi cha pili.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amemteua Dkt. Makame Omar Makame kuwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TMA.

Dkt. Makame (Zanzibar) ni Mhadhiri Mwandamizi wa Jiografia katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi John Kijazi imeeleza kuwa uteuzi wa viongozi hao umeanza tarehe 18 Novemba, 2019.





Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Mfumo wa TANePS Kuleta Tija na Ufanisi Katika Sekta ya Ununuzi ya Umma





Na Jovina Bujulu, MAELEZO, Dar es Salaam

Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli imeendelea kujidhihirisha jinsi inavyofanya kazi kwa ufanisi na weledi kwa kuhakikisha inatekeleza mipango yake kwa kasi inavyotakiwa. 

Hatua hiyo inapelekea utendaji wa kazi za Serikali kuwa bora na zenye tija kwa wananchi siku hadi siku na zenye nia ya kuleta mabadiliko katika utekelezwaji wa miradi mbalimbali ambayo hutumia pesa nyingi za umma inayoendana na thamani ya pesa.

Kwa kuzingatia kuwa fedha zitumikazo katika utekelezaji wa miradi ya Serikali kwa kiasi kikubwa hutumika kupitia mfumo wa ununuzi wa umma. Ili kuleta tija kwa taifa, Serikali imeamua kuimarisha eneo hilo kwa kuanzisha Mfumo wa Ununuzi kwa njia ya Kielektroniki (TANePS) ambao unasimamiwa na Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) chini ya Wizara ya Fedha na Mipango.

Ili uwe endelevu, mfumo umetayarishwa kwa mujibu wa Sheria ya Ununuziwa Umma ya Mwaka 2011na Kanuni za Ununuzi wa Umma chini ya Tangazo la Serikali Na. 446 la Mwaka 2013. Sehemu ya XI ya Kanuni hizo inabainisha utaratibu wa mfumo wa manunuzi kwa njia ya mtandao kwa mujibu wa Kanuni ya 343,mambo yatakayotekelezwa kwa mfumo ni pamoja na usajili wa watumiaji, mchakato wa zabuni, ununuzi wa bidhaa, mnada wa mtandaoni, malipo ya ada mbalimbali pamoja na usimamizi wa mikataba mbalimbali.

Akizungumza mfumo huo hivi karibuni Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Doto James alisema kuwa mfumo umeanzishwa ili kuiwezesha Serikali kupata thamani halisi ya fedha zinazotumika kupitia ununuzi wa bidhaa, huduma na kazi za ujenzi.

Mfumo wa ununuzi umeanza kutumika tayari kuanzia mwezi Machi 2018 kwa mujibu wa Kanuni ya 342(1) ambapo baadhi ya taasisi za umma zimeunganishwa baada ya kukamilisha taratibu muhimu ikiwemo mafunzo kwa watumiaji wa mfumo huo na mfumo huo upo wazi kwa wafanyabiashara kujisajili.

Akielezea baadhi ya faida za mfumo huo, Katibu Mkuu James alisema kuwa ni pamoja na kurahisisha ushiriki wa wazabuni kwenye michakato ya ununuzi na hivyo kuongeza ushindani na ufanisi na kupunguza muda unaotumika katika mchakato wa zabuni.

“Mfumo huu utaongeza uwazi na kupunguza vitendo vya rushwa ikiwa ni pamoja na kuongeza kiwango cha uwajibikaji kutokana na urahisi wa uhakiki wa michakato ya zabuni inayoendeshwa, kupunguza gharama za ununuzi kutokana na uokoaji wa muda,  pamoja  na kupunguza  muda wa kuandaa vikao na tathmini yake pamoja na kuimarika kwa utunzaji wa kumbukumbu za ununuzi.” alisisitiza Katibu Mkuu James.

Inakadiriwa kwamba kuanzishwa kwa mfumo huu kutaokoa wastani wa shilingi bilioni 34 katika miaka mitano ya kwanza, hali ambayo itaipunguzia Serikali mzigo mkubwa uliokuwa unatokana na matumizi yasiyo na tija ambayo yalikuwa kwenye mfumo wa kawaida.

Kwa kuzingatia manufaa ya mfumo huo, Serikali imeagiza PPRA kuhakikisha kuwa ifikapo tarehe 31, Desemba, mwaka huu ihakikishe kwamba taasisi zote za nunuzi nchini ziwe zimeungwa katika mfumo huo.

“ Natoa wito kwa wazabuni, taasisi binafsi na za umma  na wananchi kwa ujumla kuungana na Serikali kwa kutoa ushirikiano wa kutosha ili kufanikisha azma ya Serikali  ya kuwa na mfumo wenye tija kwa taifa” alisema James.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA), Mhandisi Leonard Kapongo alisema baada ya kupatiwa maelekezo hayo Mamlaka ilianza kutoa  mafunzo kuhusiana na matumizi ya mfumo wa TANePS kwa maafisa wa ununuzi na TEHAMA wa taasisi za Umma.

“Mpaka sasa Mamlaka imefanikiwa kuunganisha taasisi 418, huku  wataalamu waliopatiwa mafunzo kutoka taasisi nunuzi ikifikia 1,600 ambapo mara baada ya kupatiwa mafunzo taasisi zao huunganishwa kwenye mfumo na kuendelea kutekeleza michakato yote ya ununuzi inayofuata” alisema Mhandisi Kapongo.

Mhandisi Kapongo alitoa rai kwa wakuu wa taasisi kuhakikisha kwamba wanatumia mfumo huo kwani ni takwa la Sheria ya Ununuzi na Kanuni zake, na kwamba PPRA watafuatilia kwa karibu kuhakikisha matumizi sahihi ya mfumo huo.

Watoa huduma mbalimbali, wazabuni na makandarasi wameshauriwa kuchangamkia fursa ya kushiriki kwenye michakato ya zabuni kwa kujisajili TANePS kupitia tovuti ya mfumo ambayo ni, www.taneps.go.tz ambapo watapata maelekezo mbalimbali ya namna ya kujisajili.

Akizungumzia faida ya mfumo huo kwa wazabuni, Mhandisi Kapongo alisema kuwa ni mfumo uliorahisishwa sana kwa vile hawatahitaji tena kutumia makabrasha au kusafiri kwa ajili ya kuwasilisha zabuni zao.

“Mambo yote hayo yatafanyika kwa njia ya mtandao, yakihusisha kutangazwa kwa mipango ya ununuzi ya mwaka, matangazo mahsusi ya zabuni na Wazabuni waliosajiliwa kuweza kupakua nyaraka za zabuni na kuziwasilisha kwa taasisi nunuzi kwa njia ya mtandao na majibu ya washindi wa zabuni yatatangazwa kwenye mtandao wa mfumo” alisema Mhandisi Kapongo.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya PPRA, Balozi Dkt, Marten Lumbanga ameunga mkono mfumo huo na kuongeza kuwa utarahisisha kazi na kuweka uwazi kwa mapato ya Serikali yanayoingia kupitia ununuzi kwa taasisi za umma.


Uchaguzi Mkuu CHADEMA Kufanyika Desemba 18, 2019

 

Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema kimetangaza ratiba ya uchaguzi wa viongozi wake ngazi ya Taifa.

Mchakato huo unaanza na uchukuaji na urejeshaji fomu kuanzia  Novemba 18 hadi Novemba 30, 2019 huku mkutano mkuu ukifanyika Desemba 18, 2019.

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vicent Mashinji akizungumza na wanahabari makao makuu ya chama hicho, Kinondoni jijini Dar es Salaam alisema uchaguzi huo utaanza kwa kuchagua viongozi ngazi ya mabaraza na kufuatiwa na viongozi wakuu wa chama ngazi ya Taifa.

"Tutakuwa na Mkutano Mkuu wa Taifa itakuwa December 18, 2019, tushapeleka mialiko kwa watu mbalimbali, miongoni mwa mambo tutakayoyafanya siku hiyo ni kuchagua Viongozi Wakuu wa Chama

"Mchakato tunaoanza nao ni kuchukua na kurudisha fomu za Wagombea, huu mchakato unaanza November 18, 2019, wote ambao wangependa kugombea nafasi mbalimbali wanakaribishwa kuja kuchukua fomu, kujaza kwa ufasaha na kwenda kugombea" Amesema 
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vicent Mashinji

Amesema baada ya kupitia majina ya wote walioomba, Desemba 8, 2019 kamati tendaji ya baraza la vijana na wazee watakutana na kufuatiwa na mkutano mkuu wa uchaguzi wa viongozi wa mabaraza hayo Desemba 9, 2019.

Dk Mashinji amesema Desemba 10, 2019 kamati tendaji ya baraza la wazee na vijana itakutana ambapo ni vikao vinavyofanyika kufuatiwa na mkutano mkuu.

Serikali yalifunga Kanisa la Mfalme Zumaridi Jijini Mwanza

Uongozi wa Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza umepiga marufuku ibada zinazoendeshwa na kiongozi wa kanisa la Mfalme Zumaridi lililoko mtaa wa Iseni kata ya Butimba hadi hapo Serikali itakapojiridhisha kuwa ibada hazikinzani na sheria za nchi.
 
Agizo la kupiga marufuku limetolewa  jana Novemba 18, 2019 na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza Daktari Philis Nyimbi akiwa ameongozana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo katika eneo la kanisa hilo.

Amesema kanisa hilo limekuwa likitumia katiba ya kanisa lingine ambalo ni Pentecoste Christian Church of Tanzania  na pia limekuwa likitembea na Katiba ya Kanisa hilo.

DC Nyimbi amesema kiongozi wa Kanisa hilo la Mfalme Zumarid amekuwa akiendesha kanisa hilo bila kufuata sheria za nchi wala maandiko matakatifu kwa kujiita Mungu wa Dunia, Mfalme wakati yeye ni Mwanamke.

Diamond Platnumz atunukiwa tuzo ya kujali na kuthamini jamii..wasema anastahili kupewa hongera na kutiwa moyo




Taasisis ya The Foundation for Conserving Natural Resources Based for Future Generation (FCRFG) na wadau wengine wametangaza nia yao ya kumtuza msanii maarufu hapa nchini Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz tuzo maalum ikiwa ni sehemu ya kutambua jitihada zake anazozifanya katika jamii.

Diamond ameweza kujitoa na kusaidia jamii kwa njia tofauti, ameweza kuwalipia watoto gharama za upasuaji wa moyo katika hospitali ya Taifa Muhimbili, kufuturisha watu wa makundi maalum, kutoa michango ya madawati, kutoa bodaboda kwa vijana na kusaidia wakina mama wajasiliamali.

Akizungumza na wanahabari mapema hii leo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya TCRFG Bw. Omary Kalekela amesema wameamua kufikia maamuzi hayo baada ya kutafakali kwa kina kazi anazofanya msanii huyo kwa jamii.

“sisi kama wadau wa maendeleo tumeona msanii huyu amefanya mengi mazuri lakini kubwa ambalo limetugusa ni suala la kujitolea kuwalipia watoto wenye matatizo ya moyo pale hospitali ya taifa ya Muhimbili, ni kitendo ambacho kinatia moyo na faraja kwa jamii, kukaa kimya bila kumpa pongezi na kumtia moyo itakuwa si uungwana na ni uchoyo wa fadhila, sisi kama wadau wa maendeleo hatupo tayari kuwa wachoyo wa fadhila” alisema Kalekela.

Alisema tuzo hiyo inatarajiwa kutolewa katika ofisi za wasafi media, Jumamosi hii, pia siku hiyo Diamond Platnumz atavalisha joho maalum na kukabidhiwa Jogooo ikiwa ni ishara ya ujemedari wake wa kufanya kazi bila kuchoka licha ya kwamba hakusoma na kufikia ngazi ya digrii.

Pia Taasisi hiyo ilitumia nafasi hiyo kumpongeza Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kujitoa kwake na kuwathamini wasanii hadi kufikia hatua ya kutoa milioni 100 kwa ajili yao, lakini pia amesema wataendelea kumuombea Rais na wasaidizi wake wawe na afya njema na waendelee kutekeleza majukumu yao wakiwa na afya njema.

Sunday, November 17, 2019

Chuo kikuu cha Dar es salaam chafanya mahafali ya 49 kwa duru ya pili, zaidi ya wanafunzi 8,000 wahitimu









Selemani magali

Chuo Kikuu cha Daresalaam kimefanya mahafali yake ya 49 dulu ya pili na tatu huku ikiwashauri wahitimu kwenda kuyafanyia kazi yote waliyojifunza ikiwemo kuwa wabunifu na kujitengenezea ajira kwa kufanya ujasiliamali.

Mahafili hayo ambayo yalifayonyika katika ukumbi wa mlimani city yalishuhudia wahitimu wa digrii za uzamili, awali, astashahada na vyeti wakitunukiwa tuzo mbalimbali.

Akizungumza kabla ya kuwatunuku wahitimu, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuuu cha Dar es salaam Prof William A.L Anangisye alisema kwa ujumla katika mwaka 2019 wahitimu 8,313( wanawake 3201 au asilimia 38.5) wamefuzu na wamestahili kutunukiwa tuzo mbalimbali za Chuo kikuu cha Dare salaam.

Alisema kwa duru la pili kulikuwa na jumla ya wanafunzi 5, 444 (wanawake 2,194 sawa na asilimia 40.3) kati yao, 95 (wanawaker 33 sawa na asilimia 34.7) wamefuzu na wanastahili kutunukiwa shahada ya uzamivu; 575 (wanawake 223 sawa na 38.9%) wamefuzu na wanastahili kutunukiwa shahada za umahili; 250 (wanawake 102 sawa na 40.8%) wamefuzu masomo ya stashahada za uzamili; na 4,276 (wanawake 1,747 sawa 40.9%) wamefuzu na wanastahili kutunukiwa shahada za awali.

Aidha akitoa nasaha zake kwa wanafunzi, Anangisye aliwataka wanafunzi hao kwenda kuwa chachu ya maendeleo, akisema wameandaliwa vizuri kupambana kuleta maendeleo kwao wenyewe na Taifa kwa ujumla na kwamba Chuo kinawategemea kwenda kuleta mabadiliko na kukiletea heshima katika jamii.

“Mnapoondoka hapa na kujiunga na jamii  kama sehemu ya nguvu kazi ya muhimu, mnafahamu kwamba mnaingia katika ulimwengu unaobadilika haraka mno. Ni muhimu nanyi mkawa wepesi mno wa kujifunza mambo mapya na kubadilika kwa haraka ili msiachwe nyuma na wakati. Ni vyema kuzingatia msingi huu katika kutekeleza kazi zenu za kitaaluma mtakaozokuwa mkizifanyana katika maisha yenu ya kila siku” Alisema Anangisye

Pia amewataka wanafunzi kuwawatu wa kutafuta fursa badala ya kusubili fursa kuwafuata jambo ambalo si rahisi kutokea kwa ulimwengu wa sasa, lakini pia amewashauri kuacha woga na wawe na hulka ya kujaribu mambo ambayo yanaonekana ni magumu n ahata pale watakaposhindwa kufikia mafanikio , wasife moyo, bali waendelee kuwa na ari ya kujaribu tena na tena mpaka mafanikio yapatikane