Friday, October 11, 2019

MSIPENDE KUPELEKANA MAHAKAMANI: WAKILI.

Wakili wa kujitegemea Jovin Rutainulwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake.
...............................


Na Alodia Dominick , Bukoba

Wananchi mkoani Kagera wameaswa kujiepusha na masuala ya kukimbilia mahakamani kushitakiana badala yake wamalize migogoro yao kwa kutumia wana familia, na viongozi wa dini katika kukwepa kupoteza muda wa kufanya shughuli za kimaendeleo katika jamii.

Ushauri huo umetolewa jana na Wakili wa kujitegemea Jovin Rutainulwa wakati akiongea na vyombo vya habari ofisini kwake katika manispaa ya Bukoba mkoani humo ambapo ilikuwa siku ya kupinga adhabu ya hukumu ya kunyongwa duniani.


Wakili Rutainulwa amesema wananchi wanapaswa kuepukana na masuala ya kukimbizana mahakamani kwa migogoro midogo midogo ambayo inaweza kumalizwa na viongozi wa dini pamoja na wanafamilia badala yake watumie muda wa kwenda mahakamani kwa kufanya shughuli za kujiingizia kipato.


‘’Mahakama huzaja kesi ambazo nyingine hupaswa kuishia katika ngazi ya jamii na kesi nyingi hazina msingi ni za kupoteza gharama, muda na kujenga chuki zisizokwisha wananchi acheni kukimbilia mahakamani tafuteni njia mbadala za kutatua migogoro yenu labda Pale inaposhindikana ndo mahakama ihusike’’. Alisema wakili Jovin Rutainulwa.



Ametoa wito kwa mahakama kuendelea na mfumo walio nao wa kupunguza mashauri mahakamani kwa njia ya usuluhishi na kusikiliza kesi kwa haraka huku akitoa pongezi  kwa Wanasheria wa serikali na wa kujitegemea kwa kazi wanazofanya katika kuhakikisha wateja wao wanapata haki zao kwa muda na kwa mujibu wa sheria.

Cletus France mkazi wa Bukoba vijijini amesema, jamii ya mkoa wa Kagera inapaswa kubadilika kwa kubadili tabia ya kupenda kushitakiana mahakamani kwani jambo hilo licha ya kupoteza muda pia hupoteza rasilimali fedha na kurudisha maendeleo nyuma.
 

WATUMISHI WA UMMA WAASWA KUJIANDIKISHA.


Na Mwandishi Wetu, MOHA

NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Ramadhan Kailima, ametoa wito kwa watumishi wa umma na Watanzania kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura ili kutumia fursa hiyo kuchague viongozi wenye sifa karika  Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Kailima aliyasema hayo Mjini Dodoma jana asubuhi baada ya  kujiandikisha katika daftari hilo kwenye kituo kilichopo Mtaa wa Chimuli, Kata ya Makole.
Alisema uzoefu unaonyesha kuwa, kuna mwamko mdogo kwa kundi la watumishi wa umma kujiandikisha, kushiriki uchaguzi huo ili waweze kuchagua viongozi wenye sifa.
“Uchaguzi wa Serikali za Mitaa una umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya nchi na wananchi kwa ujumla, uandikishaji huu umeanza Oktoba 8-14, mwaka huu.
“Kampeni zitafanyika kwa wiki moja kuanzia Novemba 17-23, mwaka huu, uchaguzi utafanyika Novemba 24, mwaka huu…ni muhimu jamii kutambua kuwa, mshindi katika uchaguzi huu atapatikana kwa idadi ya wapiga kura sio asilimia,” alisema.
Kailima alisema ni muhimu Watanzania wakashiriki uchaguzi huo uli watumie fursa hiyo kuchagua kiongozi anayestahili, wasiposhiriki atachaguliwa Mwenyekiti wa Serikali ama mjumbe ambaye jamii kubwa haitapenda achaguliwe.
“Nawaomba wananchi wahudhurie kampeni, waulize maswali kwa wagombea, watumie fursa hiyo kuchagua viongozi ambao ni waadilifu na waaminifu.
“Rushwa ni adui wa maendeleo, wananchi mjiepushe kupokea rushwa, Wizara yangu kupitia taasisi zake za ulinzi na usalama ziko imara, tutaimarisha ulinzi wakati wa kampeni, upigaji kura na utangazaji matokeo,” alifafanua.
Aliwapongeza waandikishaji, wasimamizi wa zoezi hilo kwa kufika mapema kwenye vituo vya uandikishaji wapiga kura.
Alisema vituo hivyo viko sehemu barabarani, mitaani ambapo uandikishaji huo hauna vikwazo kwani hauhitaji kitambulisho cha uraia, cheti cha kuzaliwa.
“Ukifika kituoni utaulizwa majina yako kamili, umri wako, eneo unaloishi…kama eneo lako la kujiandikisha sio hilo utaelekezwa eneo la kwenda kujiandikisha,” aliongeza.
Kwa upande wao, mwandikishaji wapiga kura katika kituo hicho, Peter Ititi na mjumbe wa Serikali ya Mtaa huo, John Fundi walimshukuru Kailima kwa wito alioutoa ili jamii ione umuhimu wa kushiriki uchaguzi huo.

WANAHABARI WAKUMBUSHWA UMUHIMU WA KUFIKISHA HABARI ZA HALI MBAYA YA HEWA KWA WAKATI.



WANAHABARI WAKUMBUSHWA UMUHIMU WA KUFIKISHA HABARI ZA HALI MBAYA YA HEWA KWA WAKATI.

Tarehe 09/10/2019: Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekutana na wadau wa sekta mbalimbali na wanahabari ili kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zinazoweza kujitokeza.
Akiongea wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, mgeni rasmi ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi alisisitiza umuhimu wa vyombo vya habari katika kusambaza taarifa za hali ya hewa ukiwemo utabiri wa hali ya hewa na tahadhari ya hali mbaya ya hewa, huku akitolea mfano wa athari zilizoanza kuonekana mwanzoni mwa msimu wa mvua za vuli za mwaka huu.
“Napenda kusisitiza umuhimu wa warsha hizi ni kuhakikisha jamii tunayoenda kuihudumia inapata taarifa sahihi, kwa wakati na kwa lugha inayoeleweka kirahisi, msimu wa vuli umeanza na matukio mengi ya upepo mkali, mawimbi makubwa na mvua kubwa hivyo taarifa hizi zinakuwa na manufaa pale ambapo zinatumika kwa wakati’, alisema Dkt. Kijazi. Aidha, alivishukuru vyombo vya habari nchini kwa kuendelea kusambaza kwa wakati taarifa za hali ya hewa ikiwa pamoja na tahadhari za hali mbaya ya hewa.
Kwa upande mwingine, Dkt.Kijazi alifafanua kwa wadau wa sekta mbalimbali sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Na.2 ya 2019. Alisema lengo la Sheria hiyo ni kuboresha huduma za hali ya hewa hapa nchini na kutoa mwongozo wa ushiriki wa sekta mbalimbalikatika matumizi ya huduma hizo. Dkt. Kijazi alifafanua vipengele vya sheria hiyo vinavyowahusu wadau wa huduma za hali ya hewa alipokuwa anafunga mkutano huo wa wadau.
Aidha, wadau hao walipata fursa ya kutoa ushauri wa athari zinazoweza kujitokeza kulingana na utabiri wa msimu wa mwaka ulioandaliwa kwa mikoa inayopata mvua za msimu mara moja kwa mwaka ambayo ni mikoa ya kanda ya magharibi, kati, nyanda za juu kusini magharibi, kusini mwa nchi, ukanda wa pwani ya kusini pamoja na maeneo yaliyoko kusini mwa mkoa wa Morogoro.
Kwa upande wa wanahabari waliahidi kuendelea kutoa taarifa sahihi za hali ya hewa kama zinavyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania na waliishukuru TMA kwa kuendesha warsha hizo ambazo zimeendelea kuwajengea uwezo wa kuelewa lugha inayotumika katika utabiri wa hali ya hewa.
Warsha hizo zilifanyika tarehe 08/10/2019 kwa kuwakutanisha wadau wa sekta mbalimbali na tarehe 09/10/2019 kwa kuwakutanisha wanahabari. Utabiri wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 unatarajiwa kutolewa rasmi kwa umma kupitia vyombo vya habari siku ya Alhamisi, tarehe 10/10/2019,makao makuu ya ofisi za TMA, saa tano kamili asubuhi.

TMA YAJIPANGA KUTOA MWELEKEO WA MSIMU WA MVUA ZA MWAKA KWA MWEZI NOVEMBA 2019 HADI APRILI 2020 KWA KUWANOA WANAHABARI



Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi akifafanua jambo kwa wanahabari (hawapo pichani) katika warsha ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 katika ofisi za TMA, Makao Makuu, Ubungo Plaza Dar es Salaam, Tarehe 09 Oktoba 2019.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi katika picha ya pamoja na wanahabari walioshiriki warsha ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 katika ofisi za TMA, Makao Makuu, Ubungo Plaza Dar es Salaam,Tarehe 09 Oktoba 2019.
Wanahabari mbalimbali wakichangia mjadala katika warsha ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 katika ofisi za TMA, Makao Makuu, Ubungo Plaza Dar es Salaam,Tarehe 09 Oktoba 2019.
Mtaalamu wa hali ya hewa Bw. Abuubakar Lungo akifafanua jambo kwa kina kwa mwanahabari kutoka gazeti la habari leo Bi. Theopista Nsanzugwako katika warsha ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 katika ofisi za TMA, Makao Makuu, Ubungo Plaza Dar es Salaam,Tarehe 09 Oktoba 2019.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi akifunga rasmi warsha ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 katika ofisi za TMA, Makao Makuu, Ubungo Plaza Dar es Salaam,Tarehe 09 Oktoba 2019.
Utabiri wa msimu wa mvua za mwaka kwa mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zake utatolewa rasmi siku ya Alhamis,Tarehe 09 Oktoba 2019, Ofisi za TMA, Ubungo Plaza, Dar es Salaam

MKONGEA ATAKA UJENZI WA WODI YA WAZAZI NACHINGWEA UKAMILIKE HARAKA.

 
Kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru Kitaifa, Mzee Ally Mkongea, akifungua kitambaa katika uwekaji wa jiwe la msingi jengo la wodi ya wazazi Hospitali ya Nachingwea.
............................................


Na Hadija Hassan, Lindi.


Wataalamu wanaotekeleza mradi wa Wodi ya kisasa ya Wazazi katika Hospital ya Wilaya ya Nachingwea Mkoani Lindi wametakiwa kuhakikisha ujenzi wa mradi huo unakamilika kwa haraka ili wananchi waweze kutumia jengo hilo.


Wito huo umetolewa na kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru Kitaifa, Mzee Ally Mkongea jana Oktoba 10 2019, alipokuwa anazungumza na wananchi pamoja na watumishi mbali mbali wa Halmashauri hiyo baada ya mbio za mwenge wa Uhuru kuweka jiwe la msingi katika mradi huo.


Mkongea alisema Serikali inapoamua kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa kama hiyo ina lengo la kuondoa kero kwa wananchi wake kwa kusogeza huduma Karibu na wananchi hivyo ni wajibu kwa wataalamu kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati.


Alisema ili kuharakisha ukamilishaji wa jengo hilo ni vyema kuweka oda ya Vifaa mapema wakati ujenzi huo unaendelea ili pia kuepuka kununua vifaa ambavyo sio imara kutokana na uharaka mtakaokuwa nao wa kutoa huduma mara baada ya jengo hilo kukamilika.


Pamoja na mambo mengine Mkongea aliwataka watumishi wa Hospital hiyo ya Wilaya kufanya kazi kwa bidii na kutoa huduma inayostahiki kwa kufuata Sheria na maadili ya kazi yao pamoja na kuwaasa wananchi kuacha kutumia tiba za kienyeji ambazo hazijathibitishwa na wataalamu.


Awali akisoma taarifa ya mradi huo Mganga Mfawidhi wa Hospital ya Wilaya ya Nachingwea Dkt, Elias Zephania alisema mradi huo unaotekelezwa kwa kutumia 'force Acount' kwa wakandarasi wa ndani ulianza 16/04/2019 na ulitakiwa kukamilika 16/08/2019.


Aidha kwa mujibu wa Taarifa ya Zephania inaeleza kuwa mradi huo hadi kukamilika kwake utaghalimu kiasi cha shilingi milioni 431,919,430.88/= ambapo shilingi milioni 400,000,000/= zimetoka Serikali kuu na shilingi milioni 31,919,430.88/= kutoka Halmashauri ya Wilaya.


Alisema jengo hilo la Wodi ya wazazi litahusisha maeneo sita ambayo ni sehemu ya mama kusubiri kabla ya kujifungua, Sehemu ya kujifungulia , chumba cha upasuaji , sehemu ya waliojifungua bila upasuaji, sehemu ya waliojifungua kwa upasuaji pamoja na sehemu ya watoto waliozaliwa kabla ya muda (njiti).


Zephania pia alieleza sababu za Mradi huo kuchelewa kukamilika kwa tarehe iliyopangwa kutokana na changamoto mbali mbali zikiwemo ugumu wa upatikanaji wa mafundi wenye uwezo kwa ajili ya kutekeleza mradi huo pamoja na kuchelewa kusoma kwa bakaa katika mfumo wa malipo wa FFARS baada ya mwaka mpya wa fedha kuanza.


Hata hivyo Zephania alibainisha kuwa ujenzi huo wa wodi utaongeza idadi ya wodi kwenye hospitali hiyo ambapo wodi ya wazazi iliyopo sasa itabadilishwa matumizi kuwa wodi ya watoto, huku wodi ya watoto ya sasa ikiwa wodi ya wanaume upasuaji ambayo awali haikuwapo kabisa.


Nae Mbunge wa jimbo hilo la Nachingwea Hasan Masala kwa niaba ya wananchi wa Wilaya hiyo aliishukuru Serikali ya awamu ya tano kwa kuweka kipaumbele katika sekta ya Afya ambayo ndio msingi wa kaleta maendeleo kwa wananchi.


Masala alisema kuwa uwepo wa jengo hilo utaboresha huduma za mama na mtoto katika Hospital hiyo kwa kuwa na mazingira rafiki kwa mama kujifungu kwa njia ya kawaida na upasuaji.

Facebook yapanua mpango wa kutathmini usahihi wa taarifa zinazochapishwa hadi nchi 10 Kusini mwa Jangwa la Sahara



Nchi za Kenya, Nigeria, Afrika Kusini, Cameroon, na Senegal ni miongoni mwa nchi ambazo zimejumuishwa katika mpango wa kuthibitisha taarifa zinazochapishwa kwenye mtandao wa Facebook uliotangazwa leo hadi kufikia nchi 10 barani Afrika. Mpango huu unatekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la Agence France-Presse (AFP), France 24 Observers, Pesa Check na Dubawa, aidha mpango huu ni mkakati endelevu wa kupanua wigo wa kuthibitisha usahihi na ubora wa taarifa zinazochapishwa kwenye mtandao wa Facebook sambamba na kupunguza usambazaji wa taarifa za uongo kwenye mtandao huu.

Mpango huu unatekelezwa kwa ushirikiano na mtandao wa mashirika ya habari yanayothibitisha usahihi wa taarifa
yaliyoidhinishwa na Mtandao wa Kimataifa wa Kuthibitisha Taarifa usioegemea mrengo wowote, mpango huu wa uthibitisha taarifa zinazochapishwa utatekelezwa nchini Cote d’Ivoire, Ethiopia, Zambia, Somalia na Burkina Faso kupitia shirika la AFP,  nchini Uganda na Tanzania shirika la Pesa Check na AFP ndio watakaosimamia utekelezaji wa mpango huu, taarifa zinazochapishwa kwenye mtandao wa Facebook katika Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo zitathibitishwa na shirika la habari la France 24 na AFP huku nchini Guinea Conakry ikisimamiwa na shirika la habari la France 24, nchini Ghana taarifa zitathibitishwa na shirika la Dubawa.

Facebook inatumia kielelezo cha
maoni yanayotumwa na watumiaji wa Facebook kuainisha habari za uongo, taarifa hii hutumwa kwa mashirika mengine kuthibitisha usahihi wake. Taarifa, picha na video zote zinazochapishwa kwenye mtandao wa Facebook ndani ya nchi zitathibitishwa kuhakikisha kwamba ni za kweli. Mashirika tunayoshirikiana nayo kwenye mpango huu yakijiridhisha kwamba kuna habari ya uongo, Facebook itaweka habari hiyo sehemu ya chini ya Taarifa za Habari, kufanya hivi kutapunguza usambazaji wa taarifa husika.

Kojo Boakye, ni afisa Mkuu wa Sera ya Umma katika kampuni ya Facebook barani Afrika, anasema: “Kupanuliwa kwa wigo wa kuthibitisha habari na mashirika mengine hadi nchi 15 ndani ya kipindi cha mwaka mmoja ni ushahidi tosha kwamba Facebook imejitolea na kuweka kipau mbele barani Afrika, sambamba na kuongeza idadi ya lugha zinazotumika barani Afrika kama sehemu ya mpango huu. Tunafanya kila juhudi kutekeleza wajibu wetu wa kuchukua hatua madhubuti kupambana na habari za uongo zinazosambazwa kwenye mtandao wa Facebook, tunafahamu kwamba tatizo la habari za uongo limekuwa tatizo sugu, na mpango huu ni mkakati muhimu katika kutafutia tatizo hili ufumbuzi wa kudumu. Tunafahamu kwamba kutumia Mashirika Mengine Kuthibitisha Taarifa hakutatua changamoto hii kabisa, lakini juhudi hii ni mojawapo ya mikakati na mipango tunayoendeleza ili kuimarisha ubora wa taarifa zinazopatikana kwenye mtandao wa Facebook. Ingawa tumepiga hatua kubwa, tutaendelea kuwekeza katika mipango ambayo itatuletea ufanisi utakaohakikisha kwamba Facebook inakuwa sehemu ambayo watumiaji wanapata habari zote, lakini sio kueneza habari za uongo.”

Mashirika ya Kuthitibisha Taarifa wanaposoma taarifa kuthibitisha ukweli wa habari husika, Facebook itaionyesha habari hiyo kwenye
Makala Yanayohusiana chini ya sehemu ya Taarifa za Habari. Wasimamizi wa Kurasa na watumiaji wa Facebook watapata arifa watakapojaribu kutuma habari au ikiwa tayari wametuma habari ambayo imethibitika kwamba ni uongo, kufanya hivyo kunawapa watu uwezo wa kujiamulia taarifa ambazo wangependa kusoma, kuziamini, na kutuma.

Kuhusu mpango wa kuthibitisha taarifa zinazochapishwa kwa lugha ya Kiingereza na Ufaransa  katika nchi nane barani Afrika Phil Chetwynd, Mkurugenzi wa Habari za Ulimwengu wa Shirika la AFP amesema:, “Usimamizi wa AFP una furaha kubwa kupanua wigo wa mpango wa kuthibitisha taarifa zinazochapishwa kwenye mitandao kwa ushirikiano na Facebook. AFP ina uzoefu wa muda murefu na sifa za ubora wa hali juu katika taaluma ya uanahabari barani Afrika na tutatumia mtandao wa mashirika na wanahabari wetu wabobezi katika bara hili kupambana na usambazaji wa habari za uongo.”

Eric Mugendi, Mhariri wa shirika la Pesa Check ambalo jukumu lake ni kuthibitisha taarifa zinazochapishwa kwa lugha ya Kiswahili ameongeza kwamba: “Mitandao ya jamii kama Facebook imebadilisha, sio tu vyanzo vya habari miongoni mwa Waafrika bali mitandao ya jamii imekuwa chanzo muhimu cha maudhui ya kidijitali au “intaneti” kwa Waafrika wengi. Kwa kiasi kikubwa mitandao ya jamii inaathiri mtazamo wetu wa ulimwengu, mijadala yetu ya umma na mahusiano yetu na watu maarufu katika jamii. Mradi huu ni mkakati utakaoleta ufanisi mkubwa katika kupanua mpango wa kuthibitisha taarifa ili kusahihisha taarifa ambazo zinaweza kuleta madhara hasi katika ulimwengu wa uhalisia. Muradi huu utatusaidia kukabiliana na habari za uongo moja kwa moja na kwa uharaka unaotakiwa. Kupitia muradi huu, tumeona matokeo chanya katika ushirikiano wetu na wachapishaji na umma kwa ujumla. Kadhalika muradi huu unawasaidia wataalam wetu wanaotathmini usahihi wa habari kufikia hadhira kubwa jambo ambalo halingewezekana bila muradi huu. Kwa kweli muradi huu umetusaidia sana kuelewa pengo lililopo na mambo mengine ambayo ndiyo mihimili inayosaidia kusambaza habari za uongo katika bara la Afrika. Mchango wetu unazidi kukua hatua kwa hatua ikiwa ni juhudi endelevu za kujenga jamii ya Afrika iliyohabarishwa sawa sawa.”

Akiunga mkono kujumuishwa kwa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Guinea Conakry, na Cote d’Ivoire
Derek Thomson, Mhariri mkuu wa shirika la France 24 Observers, amesema: “Taarifa za uongo zimekuwa tatizo kubwa barani Afrika. Kila siku watumiaji wetu kutoka bara la Afrika wanatutumia picha na habari ambazo wanazipata kwenye mitandao ya jamii wakiuliza kama maudhui ya picha na taarifa hizo ni sahihi. Unaweza kuthibitisha? Ni wajibu wetu kama wanahabari kuhakikisha kwamba tunathibitisha taarifa zinazosambaa ili tutoe taarifa sahihi. Kushiriki kwetu katika mradi huu wa Facebook kunatusaidia kuhakikisha kwamba wale wanaotuma taarifa za uongo wanajua kwamba tuna ukweli na hawawezi kutupotosha”
Caroline Anipah, Afisa Mipango katika shirika la Dubawa (Ghana) ameongeza kusema: “Katika shirika la Dubawa tuna furaha kubwa kuona Ghana, nchi ambayo imekuwa mhanga na kushuhudia taarifa za uongo na uzushi zikienezwa kutokana na ufanisi wa teknolojia na kusambaa kwa intaneti, ikijumuishwa kwenye mpango huu. Dubawa imedhamiria kuimarisha ubora na usahihi wa habari zinazosomwa na umma kwa madhumuni ya kuzuia usambazaji wa habari za uongo na uzushi sambamba na kuendeleza utawala mzuri na kuhimiza uwajibikaji.”