Wednesday, January 9, 2019

SERIKALI KUSAINI MIKATABA YA UBANGUAJI WA KOROSHO JANUARI 10

Waziri wa Kilimo, Mhe Japhet Hasunga (Mb) akisisitiza mpango wa serikali kusaini mikataba ya ubanguaji wa korosho wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Bodi ya Korosho (CBT) Mkoani Mtwara,  leo tarehe 8 Januari 2019. (Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)
............................

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Mtwara

Serikali imesema kuwa tarehe 10 Januari 2019 itasaini mikataba na wamiliki wa viwanda vya ubanguaji wa korosho waliojitokeza kwa ajili ya kubangua korosho za serikali za msimu wa mwaka 2018/2019 zilizonunuliwa na serikali kwa bei ya Shilingi 3300 kwa kilo.

Waziri wa Kilimo, Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo leo tarehe 8 Januari 2019 wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Bodi ya Korosho (CBT) Mkoani Mtwara.

Alisema kuwa hivi karibuni serikali ilitangaza kuwa korosho ghafi zote zitabanguliwa nchini hivyo utekelezaji wa jambo hilo umeanza, ambapo Bodi ya Nafaka na Mazao mchanganyiko itaingia mikataba ya ubanguaji.

Pamoja na wamiliki wa viwanda kupewa kazi ya kubangua korosho lakini pia serikali imewakaribisha wananchi kujitokeza kubangua korosho za serikali kupitia vikundi au mtu mmoja mmoja. “Wananchi wenye uwezo wa kubangua tunawaomba waende Shirika la kuhudumia viwanda vidogo vidogo-SIDO) kwa ajili ya kujiandikisha ambapo mpaka sasa watu 126 kwa ajili ya ubanguaji na Tani 29 zimechukuliwa kwa ajili


ya kuanza kubanguliwa” Alisisitiza Mhe Hasunga

Katika mkutano huo Waziri huyo wa kilimo Mhe Japhet Hasunga amempongeza Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli kwa kushuhudia utiaji wa saini mkataba wa mauziano ya mahindi kati ya Wakala wa Taifa wa hifadhi ya Chakula (NFRA) na Shirika la Chakula Duniani (WFP) wa Bilioni 21 zitakazoiwezesha NFRA kunua mahindi kwa wakulima hivyo kuimarisha soko la nafaka nchini.

Mhe. Hasunga alisema kuwa pamoja na kuanza ubanguaji kupitia SIDO lakini serikaliimeanza mchakato wa kukufua viwanda vya ubanguaji vya serikali na watu binafsi nchini ili kuongeza ajira kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kuanzisha vituo vya wabanguaji wadogo wadogo.

Akizungumzia kuhusu swala la malipo ya korosho na uhakiki wa wakulima alisema kuwa tayari kiasi cha korosho ambayo imekusanywa kwenye maghala makuu ni Tani 203,938.3 wakati korosho iliyopo kwenye Vyama vikuu vya ushirika ni Tani 29,803.53 inayofanya jumla ya korosho yote iliyopokelewa kwenye vyama vya ushirika na maghala makuu kuwa Tani 233,741.83 sawa na asilimia 84.7 ya lengo lililowekwa la ukusanyaji katika Mikoa ya Mtwara, Lindi, Ruvuma na Pwani.

Kuhusu malipo ya wakulima alisema kuwa miamala ya malipo ambayo imefanyika ni 261,458 yenye jumla ya watu 203,569.

Aidha, vyama 490 vilimelipwa kati ya vyama 617, Alisema


Mkoa wa Mtwara jumla ya vyama 39 bado havijalipwa, Mkoa wa Lindi vyama vitano na Ruvuma viwili hivyo serikali imejipanga ndani ya wiki mbili vyama hivyo kuwa vimelipwa.

Waziri Hasunga amesema kuwa mpaka kufikia jana tarehe 7 Januari 2019 fedha ambazo zimeingizwa kwenye Account za wakulima ni zaidi ya Bilioni 257 huku ambazo tayari zimeingia kwenye Account za wakulima ni Bilioni 226.2 ambapo Zaidi ya Bilioni 30.7 zilizohakikiwa bado hazijaingizwa kwenye Account za wakulima kutokana na taarifa za baadhi ya wakulima hao kutofautiana majina ama vinginevyo. “Tunawaomba sana wananchi kwenda Benki kujiridhisha kama Account zao zinafanya kazi kwani


serikali ina fedha za kuwalipa wakulima wote wa korosho” Alisema

“Tena nisisitize kwa wale wanaofanya biashara ya korosho kinyume na utaratibu maarufu kama (Kangomba) wajisalimishe na kuomba radhi wenyewe kuliko kusubiri serikali iwabaini” Alisema

Vilevile, Mhe Hasunga alisema kuwa wizara yake imeweka mikakati mbalimbali ambapo hadi kufikia Januari 31 mwaka huu zoezi la uhakiki wa wakulima wanaostahili kulipwa liwe limekamilika ambapo zaidi ya asilimia 80 ya wakulima wawe wamelipwa.

Pia amewataka wananchi kupuuza taarifa mbalimbali zizotolewa na baadhi ya wananchi wasiolitakia mema Taifa kupitia mitandao ya kijamii kuwa serikali hailipi wakulima badala yake amesisitiza kuwa serikali ina fedha za kutosha kulipa wakulima wa korosho isipokuwa kangomba wao hawatalipwa.
 Waziri wa Kilimo, Mhe Japhet Hasunga (Mb) akisisitiza jambo wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Bodi ya Korosho (CBT) Mkoani Mtwara,  leo tarehe 8 Januari 2019.
 Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Prof Siza Tumbo akifatilia mkutano wa Waziri wa Kilimo, Mhe Japhet Hasunga (Mb) wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Bodi ya Korosho (CBT) Mkoani Mtwara,  leo tarehe 8 Januari 2019.

MFUMUKO WA BEI KWA MWAKA 2018 WASHUKA, WAVUNJA REKODI MIAKA YA 40.

Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Bw. Ephraim Kwesigabo akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hali ya Mfumuko wa Bei kwa mwezi Desemba 2018 leo jijini Dodoma.
..........................................

Na: Beatrice Lyimo-MAELEZO, Dodoma

Wastani wa Mfumuko wa Bei wa Taifa kutoka Januari hadi Desemba Mwaka 2018 umepungua hadi asilimia 3.5 kutoka wastani wa asilimia 5.3 kama ilivyokuwa mwaka 2017.

Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Bw. Ephraim Kwesigabo wakati akitoa taarifa kuhusu mfumuko wa bei wa mwezi Desemba 2018 pamoja na wastani wa mfumuko huo kwa mwaka mzima.


“Wastani huu wa mfumuko wa bei wa mwaka wa asilimia 3.5 ndiyo wastani mdogo kabisa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 40 iliyopita ambapo tangu mwaka 1970 mfumuko huo ulikuwa 3.6,” ameongeza Kwesigabo.


Aidha, akizungumzia kuhusu mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwezi Desemba ,2018, Kwesigabo amesema kuwa mfumuko huo umeongezeka hadi kufikia asilimia 3.3 kutoka asilimia 3.0 kwa mwezi Novemba 2018.


“Kuongezeka kwa Mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwaka ulioishia mwezi Desemba, 2018 kumechangiwa hasa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula kwa kipindi kilichoishia mwezi Desemba, 2018 zikilinganishwa na bei za mwezi Desemba, 2017, mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwezi Desemba, 2018 umeongezeka hadi asilimia 1.0 kutoka asilimia 0.4 ilivyokuwa mwezi Novemba, 2018,” amefafanua Kwesigabo.


Aidha amesema kuwa, baadhi ya bidhaa ya chakula zilizochangia kuongezeka kwa mfumuko wa bei ni pamoja na nyama kwa asilimia 4.6, samaki wabichi asilimia 8.2, dagaa asilimia 26.2, matunda kwa asilimia 4.3 na mbogamboga asilimia 8.5 baadhi ya bidhaa zisizo za chakula zilizochangia mfumuko wa bei ni pamoja na vitambaa vya kushonea nguo kwa asilimia 2.1, nguo za kiume na za kike kwa asilimia 6.1, nguo za watoto kwa asilimia 3.0, sare za shule kwa asilimia 3.1, dizeli kwa asilimia 27.6, petroli asilimia 10.8 na huduma za malazi kwa asilimia 6.8.


Kwa upande wa nchi za Afrika Mashariki, mfumuko wa bei kwa mwaka unaoishia mwezi Desemba, 2018 nchini Kenya umeongezeka hadi kufika asilimia 5.71 kutoka asilimia 5.58 kwa mwaka ulioishia mwezi Novemba, 2018 na mfumuko wa bei kwa mwaka unaoishia mwezi Desemba, 2018 nchini Uganda umepungua hadi kufika asilimia 2.2 kutoka asilimia 3.0 kwa mwaka ulioishia mwezi Novemba, 2018.

RC NDIKILO AAGIZA WANANCHI WALIOVAMIA ENEO KATA YA PANGANI KUONDOKA MARA MOJA

NA MWAMVUA MWINYI, PWANI 

WAKALA wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoani Pwani ,unatarajia kutumia kiasi cha sh.bilioni 25.4 kwa ajili ya kufanya matengenezo mbalimbali ya barabara kwa bajeti ya mwaka 2018-2019.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na meneja wa TANROADS mkoani hapo, mhandisi Yudas Msangi,  wakati wa kikao cha bodi ya barabara cha mkoa huo .

Alieleza, hadi kufikia septemba 2018 zimepokelewa kiasi cha sh. milioni 958.7  kwa ajili ya matengenezo mbalimbali.

“Katika kipindi hicho kiasi cha shilingi bilioni 2 zimetumika kufanya matengenezo mbalimbali kwenye barabara kuu”, 

“Kazi za matengenezo zilichelewa kuanza kutokana na taratibu za manunuzi na uhakiki wa mikataba ambavyo huchukua muda mrefu kukamilika hasa mikataba inayohakikiwa kwa mwanasheria mkuu wa serikali”alisema Msangi. 

Aidha Msangi alibainisha, mkoa umepanga kufanya miradi ya maendeleo ya barabara zenye urefu wa kilometa 32.5 zenye thamani ya sh.bilioni 2.3.
Alisema,meneja huyo alisema kwenye miradi hiyo ya maendeleo sh. bilioni 1.3 ni bajeti ambapo sh.milioni 969 ni kutoka mfuko wa barabara vilevile bilioni 7.5 ni kutoka serikali zitafanya ukarabati kwa kiwango cha changarawe/udongo.

Nae mkuu wa  mkoa wa Pwani ,mhandisi Evarist Ndikilo alieleza, ili kuboresha barabara za mkoa huo watendaji wanapaswa kuwa waadilifu.

“Kutokana na mkoa kuwa na viwanda vingi uboreshaji wa miundombinu ya barabara utasaidia kuinua uchumi wa wananchi na Taifa”:” Pia Muwe makini na baadhi ya watu wanaoharibu miundombinu ya barabara ,” alisema Ndikilo.
 

WAGONJWA 45 KUFANYIWA UPASUAJI WA MOYO WA KUFUNGUA NA BILA KUFUNGUA KIFUA KATIKA KAMBI MAALUM YA MATIBABU YA MOYO INAYOFANYIKA KATIKA TAASISI YA MOYO JAKAYA KIKWETE KUANZIA TAREHE 7/01/2019 HADI 18/01/2019

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kupitia madaktari wake bingwa wa magonjwa ya moyo kwa kushirikiana na Madaktari Afrika na Shirika la Cardio Start wote kutoka nchini Marekani  wameanza  kambi maalum ya matibabu ya moyo  ya siku 12 kuanzia tarehe 07/01/2019 hadi 18/01/2019 kwa watu wazima .

Matibabu yanayofanyika  katika kambi hiyo ni upasuaji wa kufungua kifua na bila kufungua kifua. 

Upasuaji wa bila kufungua kifua unafanyika kupitia tundu dogo linalotobolewa kwenye paja kwa wagonjwa kuzibuliwa mishipa ya moyo iliyoziba (Percutaneous Coronary Intervention – PCI) na kuwekewa vifaa  vinavyosaidia kurekebisha mapigo ya moyo ambavyo ni (Permanent Pacemaker na High powered devices CRT-P, CRT –D) .

Wagonjwa watakaofanyiwa upasuaji ni wale wenye matatizo ya moyo ambayo ni  valve, mishipa ya moyo iliyoziba, moyo kushindwa kufanya kazi vizuri, matibabu kwa watu wazima waliozaliwa na matatizo ya moyo na wale wenye matatizo ya moyo yaliyotokana  na ugonjwa wa Kisukari.

Kambi hii inaenda  sambamba na utoaji wa elimu kwa madaktari na wauguzi pamoja na kubadilishana ujuzi wa kazi kwa wageni na wataalamu wetu. Katika kambi hii tunatarajia kufanya upasuaji wa kufungua kifua kwa wagonjwa  20 na bila kufungua kifua kwa wagonjwa 25. 

Hadi jana tarehe 8/1/2019 jumla ya wagonjwa nane wamefanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua na wagonjwa wanne wamefanyiwa upasuaji wa kufungua kifua.

Hii ni kambi ya kwanza ya matibabu ya moyo tangu kuanza kwa mwaka huu wa 2019 na ni mara ya kwanza kwa shirika Cardio Start  kuja  hapa nchini kufanya kazi na sisi.