Monday, June 3, 2019

MKUTANO WA NISHATI KWA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI WAANZA ARUSHA

Image may contain: 3 people, people sitting and indoor
 Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Fedha na Utawala, Christopher Bazivamo, akifungua Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, ngazi ya wataalamu, Juni 3, 2019 jijini Arusha.
.............................................


Na Veronica Simba – Arusha

Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, umeanza leo Juni 3, 2019 jijini Arusha.


Akifungua Mkutano huo katika siku ya kwanza katika mkutano huo ambao unahusisha ngazi ya wataalamu wa sekta husika, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Fedha na Utawala, Christopher Bazivamo, amewataka kujadili kwa uwazi changamoto zinazokabili nchi wanachama hususan upatikanaji wa umeme wa uhakika ili kuainisha mikakati ya kuzitatua.


“Jamii zetu bado hazijawa na umeme wa uhakika ukilinganisha na sehemu nyingine za Dunia, hii ni changamoto ambayo tunahitaji kuitafutia ufumbuzi, tujadili kwa uwazi ili tuone wapi tunakwama na namna gani tutatue,” alisisitiza.


Akifafanua zaidi, Bazivamo alisema changamoto za nishati kwa nchi za Afrika Mashariki zinahusisha mambo mbalimbali ikiwemo nishati ya kupikia ambayo alieleza kuwa asilimia kubwa ya wanajamii wa ukanda husika bado wanatumia kuni na mkaa; hali inayochangia uharibifu wa mazingira.


Alisema haitoshi kuwaonesha wananchi kuwa nishati ipo isipokuwa kuchukua hatua za kuifanya ipatikane kwao na kwa bei wanayoweza kuimudu.


Aidha, Bazivamo amewashauri wataalamu husika, kuhakikisha wakati wanahamasisha uwekezaji katika uzalishaji wa umeme, wahamasishe pia uwekezaji katika usambazaji wa nishati hiyo ili kuwezesha hali ya upatikanaji wake kwa jamii.


Pamoja na mambo mengine, Mkutano huo wa 14 unatarajiwa kupokea na kujadili taarifa za utekelezaji wa miradi na program katika sekta ya nishati pamoja na maagizo yaliyotolewa katika Mkutano wa 13 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati.


Aidha, Mkutano huo utapokea Rasimu ya Makubaliano ya Awali (MoU) iliyoandaliwa na Sekritarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu Mradi wa Umeme wa Nsongezi katika Mto Kagera unaotarajiwa kutekelezwa kwa ushirika wa nchi za Tanzania, Uganda na Rwanda ili ipitiwe na nchi husika.


Mkutano ngazi ya Mawaziri utafanyika Juni 7 mwaka huu, ambayo ndiyo siku ya mwisho ya mkutano husika.
Tanzania inawakilishwa na wataalamu mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati, Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na taasisi mbalimbali zinazohusiana na nishati kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.
Image may contain: 4 people

 Wajumbe wa Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, ngazi ya wataalamu, wakishiriki ufunguzi wa Mkutano huo Juni 3, 2019 jijini Arusha.
Image may contain: 6 people 

Wajumbe wa Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, ngazi ya wataalamu, wakishiriki ufunguzi wa Mkutano huo Juni 3, 2019 jijini Arusha.
Image may contain: 4 people, people sitting    
Wajumbe wa Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, ngazi ya wataalamu, wakishiriki ufunguzi wa Mkutano huo Juni 3, 2019 jijini Arusha.
Image may contain: 8 people 
Wajumbe wa Mkutano wa 14 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki, ngazi ya wataalamu, wakishiriki ufunguzi wa Mkutano huo Juni 3, 2019 jijini Arusha.

SERIKALI HAINA MPANGO WA KUVIBADILI VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI KUWA VETA- OLE NASHA.

Image may contain: 1 person, smiling
Serikali imesema haina mpango wa kuvibadili Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kuwa VETA na badala yake imejikita katika kuviboresha Vyuo hivyo kwa kuvikarabati na kuviongezea vifaa vya kujifunzia na kufundishia ili viweze kutoa mafunzo bora zaidi.


Kauli hiyo imetolewa Bungeni leo Juni 03, 2019 na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha, wakati akijibu swali la Mhe. Mohamed Omary Mchengerwa (Rufiji), aliyetaka kujua kama serikali haioni umuhimu wa kukibadili chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ikwiriri FDC kuwa VETA ili kubadili fikra za wananchi wa Rufiji, Kibiti na Ikwiriri na hatimaye kuleta mwamko wa elimu.


Ole Nasha amesema serikali inaendelea kuvikarabati vyuo hivyo ambapo awamu ya kwanza ya ukarabati unaohusisha vyuo 20 upo katika hatua za mwisho za ukamilishaji na kwamba awamu ya pili inatarajiwa kuanza mapema mwezi Juni, 2019.


Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ikwiriri kilikuwa katika Awamu ya kwanza na ukarabati umekamilika.


Aidha katika mwaka wa fedha 2019/20 Rufiji ni miongoni mwa wilaya zilizotengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) cha Wilaya.


"Kwa sasa, Serikali haina mpango wa kuvibadili Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kuwa VETA na badala yake, imejikita katika kuviboresha Vyuo hivyo kwa kuvikarabati na kuviongezea vifaa vya kujifunzia na kufundishia viweze kutoa mafunzo bora" alisema Ole Nasha


Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vilianzishwa kwa lengo la kumsaidia mwananchi kukabiliana na changamoto za kimaendeleo katika mazingira yake kwa kumpatia Maarifa na Stadi anuwai ambapo vyuo hivi hutoa Elimu ya Ufundi Stadi katika hatua ya Kwanza hadi ya Tatu.


Mafunzo yanayotolewa katika vyuo hivyo ni pamoja Ujasiriamali, Kilimo, Uvuvi, ufugaji na mengine kulingana na mahitaji ya eneo husika na kwamba hivi sasa nchini kuna vyuo vya maendeleo ya wananchi 55.

BODI YA NISHATI VIJIJINI YATAKA MKANDARASI KUONGEZA KASI YA KUSAMBAZA UMEME.

NA HADIJA HASSAN, LINDI


Bodi ya Wataalamu wa Nishati Vijijini (REA) imemtaka mkandarasi wa State Grid anaetekeleza Mradi wa Kusambaza umeme Vijijini kupitia Mpango wa Rea Mkoani Lindi kuongeza Magenge ya vijana ili kuharakisha Ukamilishaji wa Usambazaji wa Umeme Katika Mkoa huo.


Wito huo umetolewa na kaimu mwenyekiti wa Bodi hiyo Dk, Andrew Komba walipokuwa katika zihara ya siku mbili Mkoani humo kwa lengo la kukagua utekelezaji wa mpango wa usambazaji wa umeme vijijini.


Komba alisema pamoja na Bodi kuonyesha kuridhishwa na kazi zilizofanywa na mkandarasi huyo Mzawa lakini bado inamshauri kuongeza magenge ya vijana ili kazi iliyosalia iweze kumalizika kwa wakati.


Hata hivyo bodi ilimtaka mkandarasi huyo kuwa pamoja na kupeleka miundombinu hiyo ya umeme pia ahakikishe anaendelea kuunganisha huduma hiyo kwa wananchi.


Alisema ili azima ya Serikali ya kusambaza umeme vijijini iweze kukamilika inaenda sambamba na wananchi kuunganishiwa pamoja na kutumia huduma hiyo.


"hili lisiishie hapa tuu katika kupeleka miundombinu lengo kuu la Serikali kuleta huduma ya umeme Vijijini ilikuwa ni pamoja na kuhakikisha Wananchi wanaunganishiwa ili waweze kupata huduma hivyo malengo yenu mnayopanga kutekeleza yaendane na kusambaza umeme kwa wananchi" Alisema Dk, Komba.


Nae Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Rea mhandisi Amosi Maganga alitumia nafasi hiyo kuwaasa wananchi wa Mkoa huo ambao wamepitiwa na mradi wa umeme vijijini kuchangamkia fursa ya umeme waliyoipata kuunganisha umeme katika maeneo yao pamoja na kuanzisha shuguli ndogo ndogo za kiuchumi ili kuweza kujiongezea kipato.


Alisema Serikali tayari imeshatoa fedha za kutosha ili kutekeleza miradi hiyo ikiwa pamoja na kushusha gharama za uunganishwaji lengo likiwa kuwafikia wananchi wote katika maeneo yao tena kwa bei nafuu.


Nae mkurugenzi wa State Grid Charles Mlawa anaetekeleza Mradi huo wa usambazaji Umeme Vijijini Katika Mkoa wa Lindi aliihaidi Bodi hiyo kukamilisha kazi kabla ya mwezi desemba mwaka huu.


Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa Mradi huo wa Rea Meneja wa Shirika la umeme Tanesco Mkoa wa Lindi Felisian Makota alisema kuwa Mradi huo wa Rea hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi Bilioni 20 za kitanzania sawa na Bilioni 4.7 kwa fedha za kimarekani na unatarajiwa kuunganishwa katika vijiji 133 vya Mkoa huo.


Aidha Makota pia alibainisha Wigo wa mradi huo ni kuunganisha 33kv Msongo wa kati wa umeme kwa km 392.350, 04/023kv Msongo mdogo wa Umeme 380,60km, 50kvA Mashine umba 185 Pamoja na 100KVA Mashine Umba 2, wateja wa laini moja 4708 na Wateja wa laini tatu 524 ambapo alieleza kuwa kazi hizo kwa sasa zimeshakamilia kwa Zaidi ya asilimia 40