Monday, May 6, 2019

DKT. NDUGULILE ATOA RAI KWA VIONGOZI WA KISIASA KUTOINGILIA KAZI ZA TAALUMA YA AFYA

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (kulia ) akipokea maelezo kutoka kwa mmoja wa wakunga ya namna wanavyowahudumia wakina mama wajawazito na watoto wakati alipotembelea Banda la Chama cha Wakunga Tanzania(TAMA),  katika Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo yamefanyika Kitaifa katika Uwanja wa Bariadi Mkoani Simiyu.
......................................


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile ametoa rai kwa viongozi wa Kisiasa hapa nchini kuacha kuingilia kazi za Kitaaluma katika sekta ya Afya na kuwaomba wawaache wataalam wafanye kazi zao kwa misingi na miiko ya Kitaaluma inayowaongoza.


Dkt. Ndugulile ameyasema hayo katika Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi, chini ya Kauli Mbiu “Wakunga Watetezi wa Haki za Wanawake”, ambapo alikuwa akimwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.


Amesema hivi karibuni kumekuwa na matamko yanayotolewa na baadhi ya viongozi wa kisiasa yanayowakatisha tamaa watumishi wa sekta ya afya na baadhi ya viongozi wameanza kuingilia masuala ya kitaalum, hivyo akawaomba ikiwa viongozi hao  watakutana na changamoto za watendaji wa afya waishirikishe wizara ya afya ili wachukuliwe  hatua kwa mujibu wa taaluma zao.


“Niwaombe sana viongozi wa Serikali na Viongozi wa vyama, masuala ya kitaaluma yanashughulikiwa kitaaluma kama kuna changamoto na wanataaluma ndiyo maana tuna mabaraza ya taaluma na ndiyo maana sisi wizara tupo mtushirikishe, nimelisema hili kwa sababu nimeona sekta imeanza kuingiliwa” alisema Dkt. Ndugulile.


Aidha, Dkt. Faustine Ndugulile amewataka wakunga hapa nchini kuendelea kuzingatia miiko na misingi ya taaluma yao katika huduma wanazotoa kwa jamii na kuahidi kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote watakaokiuka misingi hiyo kwa kuwa jamii inahitaji heshimu, utu, upendo na kutiwa moyo
Katika hatua nyingine. 


Dkt. Ndugulile ametoa wito kwa  wadau mbalimbali wa maendeleo na jamii kwa ujumla kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ili changamoto ya vifo vitokanavyo na uzazi vibaki kuwa historia ambapo amesema kwa sasa wanawake 11,000 wanakufa kila mwaka kutokana na uzazi.


Rais wa Chama cha Wakunga Tanzania, Bibi. Feddy Mwanga ameiomba Serikali kuongeza idadi ya wakunga ili mkunga aweze kutoa huduma kwa kiwango kinachokubalika Kitaifa na kimataifa huku akisisitiza Serikali kuona haja ya kujenga nyumba za wakunga katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya vinavyoboreshwa na vinavyojengwa.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthoy Mtaka amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa shilingi bilioni saba  fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na shilingi bilioni 4.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali tatu za Wilaya Bariadi, Busega na Itilima ambazo ujenzi wake unaendelea vizuri.


Aidha, Kiswaga ameshukuru Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia idadi ya watu Duniani(UNPFA) kwa namna linavyoshirikiana na Serikali mkoani Smiyu kwa kukarabati baadhi ya vituo, kununuaa vifaa mbalimmbali, kutoa mafunzo kwa wakunga jitihada ambazo zimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.


Akitoa taarifa ya Mkoa, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini amesema
Idadi ya wakunga katika vituo vya kutolea huduma za afya Simiyu imeongezeka hali iliyofanya wajawazito wengi kujifungulia katika vituo vya afya kutoka asilimia 62 mpaka asilimia 68, hivyo vifo vya mama wajawazito vimepungua kutoka vifo 48 mwaka 2017 mpaka vifo 40 mwaka 2018.


Naye Makamu Mwakilishi Mkaazi wa UNFPA hapa nchini, Dkt.Hashina Begum amesema kwa kushirikiana na Chama cha Wakunga nchini (TAMA) limetoa mafunzo kwa wakunga 90 kutoka katika vituo vilivyoboreshwa ili kuwasaidia wakina mama wajawazito na watoto kupata huduma za dharura na kupunguza vifo kwa mama na mtoto vitokanavyo na uzazi.

  
Grace Magengeni Mkunga kutoka Jijini Dodoma amesema” siku yetu imefana tunashukuru hotuba ya Naibu Waziri imetutia moyo katika kuwahudumia wanawake na watoto, nawashauri wenzangu tusimamie taaluma zetu tufanye kazi kwa bidii naamini hao wanaotuingilia majukumu yetu wataachaa maana ni kweli,  tunashukuru Naibu Waziri kulisemea hili suala”

WAGANGA WAKUU WA MIKOA WAPEWA MWEZI MMOJA KUTATHMINI UTENDAJI WA KAMATI ZA AFYA ZA MIKOA NA WILAYA ZAO.

 Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia afya Dkt Dorothy Gwajima akizungumza na Kamati ya uendeshaji ya huduma za afya ya mkoa wa Ruvuma mjini Songea.
..........................................


Waganga wakuu wa Mikoa Tanzania Bara wamepewa mwezi mmoja kuhakikisha kuwa wanazifanyia tathmini ya kina Kamati za Uendeshaji Huduma za Afya za Mikoa na Wilaya zao kuona kama zinaendana na kasi ya mabadiliko yanayokusudiwa na Serikali ya Awamu ya Tano.


Agizo hilo limetolewa jana Mei 05, 2019  mjini Songea na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dkt. Dorothy Gwajima wakati akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Uendeshaji Huduma za Afya ya Mkoa wa Ruvuma pamoja na Wajumbe wa Kamati za Uendeshaji Huduma za Afya kutoka Halmashauri ya Namtumbo, Halmashauri ya Wilaya ya Songea pamoja na Manispaa ya Songea.


Alisema anawapa siku 30 Waganga Wakuu wa Mikoa yote kuhakikisha kuwa wanafanya tathmini ya Wajumbe waliopo katika ofisi zao kama wanatosha kuendelea na nyadhifa zao za kusimamia jukumu la uendeshaji huduma za afya katika mikoa na halmashauri zao.


Dkt Gwajima ameongeza kuwa endapo itabainika kuwa baadhi ya Wajumbe wa Kamati hizo hawana sifa na kupelekea kushindwa kutekeleza majukumu yao ya usimamizi na uendeshaji huduma za afya katika maeneo yao, Waganga Wakuu wa Mikoa watalazimika kuwaweka pembeni Wajumbe hao na kuunda upya Kamati ambazo zitaweza kuiendeleza agenda ya mabadiliko katika sekta ya afya.


“Kinyume na hapo katika ziara hizi ninazoendelea kuzifanya mikoani nikikuta yupo Mganga Mkuu wa Mkoa ambaye ametulia tu, mapungufu katika vituo bado yapo na amewezeshwa na Serikali, ajue wazi kuwa yeye atakuwa kuwa hatoshi” alisema Dkt Gwajima na kuongeza:


“Haiwezekani tukute mapungufu madogo kabisa katika vituo, ambayo yangeweza kuonwa na wao walioko huko eti hayaonekani hadi tuje sisi kutoka Tamisemi ndiyo mapungufu hao yafanyiwe kazi,”amesisitiza Dkt Gwajima.


Naibu Katibu Mkuu huyo ameonya tabia iliyojengeka miongoni mwa Wajumbe wa Kamati za Uendeshaji Huduma ya Afya kukimbilia kuomba msamaha pindi zinaposhindwa kutekeleza majukumu yake kwa makusudi.


Alisema huu ni wakati wa kuboresha sekta ya afya katika vituo vya afya na zahanati kwa kuhakikisha kuwa mazingira ya utoaji huduma yanaboreshwa ili yaweze kuwavutia wananchi wengi kukimbilia kupata huduma katika zahanati na vituo vya afya vinavyomilikiwa na serikali ikiwemo hospitali za halmashauri.


Dkt Gwajima amesema kuwa kamwe hatawapa nafasi Wajumbe wa Kamati za Uendeshaji Huduma za Afya wa Mikoa na Wilaya ambao siku zote wamekuwa ni watu wa visingizio vya kuomba kusamehewa ama kupewa muda kuwa wamefahamu mapungufu yao wakati mapungufu husika ni yale yale ambayo kila siku Serikali inatoa maelekezo kuwa yafanyiwe kazi.


Alisema angependa kuona Kamati za Uendeshaji Huduma za Afya katika Mikoa na Halmashauri zikijikita katika kuongelea mambo ya ubora wa huduma kwa mteja “’quality care” na kuwa, mteja ni mfalme na si vinginevyo. 

Serikali imeshirikisha Wananchi na kutuwezesha miundombinu safi na dawa za kutosha, bajeti ya kufuatilia huduma inatolewa, semina za uongozi zinafanyika, maelekezo yanatolewa je, tatizo huwa linatokea wapi?


“Hivi vitu vidogo vidogo vya kitaalamu tubebe sisi wenyewe, Wananchi wametuunga mkono, tumeweza kushirikiana nao kujenga zahanati na vituo vya afya katika mikoa na halmashauri zetu hivyo ni jukumu letu sasa kuhakikisha kuwa tunatoa huduma bora za afya kwa Wananchi na kuondoa hii tabia ya kuwepo kwa malalamiko yanayosababishwa na uzembe katika kufuatilia na kusimamia,” alisema.


Kwa mujibu wa Dkt. Gwajima, katika ziara zake alizokwisha zifanya katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Njombe na Songea amejionea mapungufu mbalimbali ya utoaji wa huduma bora za afya katika vituo vya afya na zahanati ambayo yapo ndani ya uwezo wa Kamati za Usimamizi na Uendeshaji Huduma za Afya katika mikoa na halmashauri husika.


Ameongeza kuwa mapungufu hayo ambayo ameyashuhudia kwenye vituo vya afya na zahanati zinazomilikiwa na umma yametokana na watoa huduma waliopo katika vituo hivyo kutopata usimamizi unaostahili kutoka kwa Kamati za Usimamizi na Uendeshaji wa Huduma za Afya za Mikoa na Halmashauri husika.


Dkt Gwajima anaamini kuwa, kushindwa kwa Kamati za Uendeshaji na Usimamizi wa utoaji huduma za afya katika ngazi za mikoa na halmashauri kutekeleza majukumu yao, ndiko kulikopelekea kukithiri kwa uchafu katika majengo ya vituo vya afya na zahanati, kushindwa kufanyiwa matengenezo muhimu ya kuboresha mazingira ya zahanati na vituo hivyo licha ya vituo hivyo kuwa na fedha za uendeshaji wake.


 “Unakuta kituo kina fedha za kutosha kwenye akaunti lakini mapungufu madogo madogo ya kukera yamejaa,” ameeleza Naibu Katibu Mkuu.


Amesema hali hiyo imesababishwa na kushindwa kwa Kamati za Uendeshaji Huduma za Afya za Mkoa (RHMT) na zile za Halmashauri (CHMT) kwa kutofanya kazi ya ufuatiliaji wa utoaji huduma bora na utaalam kwenye vituo vya afya nchini licha ya kuwezeshwa na Serikali.


Sambamba na kuwataka Waganga Wakuu wa Mikoa kuzitathmini Kamati hizo, Dkt Gwajima pia amewataka wajumbe wa Kamati hizo kutambua kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli ipo na agenda moja tu ya kuleta mabadiliko katika sekta ya afya na kuwagusa watumiaji wa huduma hizo kwa huduma zenye ubora unaostahili.


“Hatutapimwa kwa idadi ya semina au uwepo wa kituo cha afya tu karibu na Wananchi bali kwa ubora huduma zinazotoleewa katika vituo hivi, vinginevyo Wananchi watakuwa karibu na vituo husika lakini hawavitumii,” amesema.


Dkt Gwajima amebainisha mapungufu kadhaa aliyoyaona kwenye ziara yake kuwa ni pamoja na Kamati za Uendeshaji Huduma ya Afya kushindwa kuzifanyia kazi changamoto mbalimbali zinazojitokeza kwenye vituo vyao vya afya na zahanati, kuwepo kwa malalamiko toka kwa wagonjwa, kukosekana kwa takwimu sahihi za utendaji kazi na Wajumbe wa Kamati za uendeshaji huduma za Afya kushindwa kuandika vizuri kumbukumbu za taarifa za kazi za ikiwemo mihutasari ya vikao na wengine kutokaa kabisa vikao muhimu.


Akiwa katika kituo cha afya Mjimwema Manispaa ya Songea Naibu Katibu Mkuu Dkt.Gwajima alipokea kero za wagonjwa kuhusu uwepo wa kauli mbaya toka kwa baadhi ya watumishi wakiwemo wauguzi na matabibu, tatizo la ukosefu dawa na vifaa tiba muhimu hususan vya akina mama wajawazito.


“Hapa Mjimwema nimebaini kasoro nyingi mojawapo kauli mbaya za watumishi na tatizo la dawa na vifaa tiba kwa wagonjwa ” ameonya Dkt .Gwajima.


Aidha, alimpongeza tabibu msaidizi mmoja aliyeibuliwa na mteja kwamba, anatamani watoa huduma wote wangekuwa kama tabibu huyo anayeitwa Lidya Mwakyusa Hii ni mara ya pili kwa wateja kuwataja hadharani watumishi watoa huduma wenye huduma inayojali mteja akiwemo Edward Mapunda wa Kituo cha Afya cha Halmashauri ya Njombe.


Dkt. Gwajima amewapongeza watoa huduma wanaotambua wajibu wao kuwa, mteja ni mfalme na amewataka kutovunjwa moyo na baadhi ya watumishi wasiozingatia maadili ya kazi na kuleta kero kwa wateja.


Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Dkt. Jairy Khanga ameahidi kuchukua hatua za mapema kufanya mabadiliko ya utendaji kazi wa Kamati za Usimamizi wa Huduma za Afya katika Mkoa wa Ruvuma

 

Sunday, May 5, 2019

MLANDIZI QUEENS KUPATIWA GARI

Na Omary Mngindo, Mlandizi.


MKURUGENZI wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani Butamo Ndalahwa, amewaahidi gari viongozi na wachezaji wa timu ya soka ya Mlandizi Queens, inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania Bara. 


Ndalahwa ametoa ahadi hiyo mwishoni mwa wiki, alipotembelea kambi ya timu hiyo iliyopo Mlandizi Kibaha Vijijini mkoani hapa, ambapo alisema ameguswa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya ukosefu wa gari inayoikabili timu hiyo. 


Alisema kuwa mara kadhaa viongozi na wachezaji wa timu hiyo wamefika ofisi kwake, wakihitaji mchango kwa ajili ya kukodi basi litakalowapeleka mikoani kwa ajili ya ushiriki wa michuano ya Ligi wanayoshiriki inayoendelea ukingoni. 


"Muda mfupi nilikuwa na wachezaji wenzenu na kiongozi katika upandaji wa miti kwenye hospitali yetu inayojengwa Disunyara, tukiwa pale nilizungumza na Mbunge Humoud Jumaa kuhusiana na changamoto ya usafiri inayowakabili," alisema Butamo. 


Aliongeza kwamba binafsi amepokea changamoto ya usafiri inayowakabili, huku akiahidi kulifikisha suala hilo ngazi ya Mkoa, ambapo alisema anaimani watashirikishwa wabunge kuhakikisha timu hiyo inakuwa na usafuri wake. 


"Historia yangu ni mwanamichezo, kwakuwa mpo katika halmashauri yetu nitahakikisha nafanya juhudi za kupatikana kwa gari la timu yatu, Rais wetu John Magufuli ameonesha njia katika michezo hivyo nasi hatuna budi kuunga mkono juhudi hizo," alisema Ndalahwa. 


Kwa upande wake nahodha wa timu hiyo Wema Richard alimshukuru Mkurugenzi huyo, huku akisema kwamba wanakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwemo ya kutoungwa mkono na mashabiki hali inayosababisha kujiona kama wakiwa. 


Kiongozi wa timu hiyo Miraji Miraji alifurahia ahadi hiyo, huku akisema kwamba kwa sasa wachezaji wanadai posho kiasi cha shilingi milioni moja, ambapo Butamo ameahidi kuwapatia, huku akianza na shilingi laki tano atayoikabidhi Jumatatu.