Wednesday, February 27, 2019

SERIKALI YA AWAMU YA TANO ITAENDELEA KULINDA NA KUKUZA HAKI ZA BINADAMU -PROF KABUDI ALIAMBIA BARAZA LA HAKI ZA BINADAMU LA UMOJA WA MATAIFA

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akihutubia Kikao cha 40 cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kinachofanyika jijini Geneva nchini Uswisi.
 ..................................


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi amesema Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kutekeleza wajibu wake wa kukuza na kulinda haki za binadamu na ustawi wa jamii kama kipaumbele chake na  itaendelea kushirikiana na Baraza hilo kuhakikisha haki za binadamu nchini na duniani kote zinadumishwa.


Prof. Kabudi amesema hayo alipolihutubia Kikao cha 40 cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kinachofanyika jijini Geneva nchini Uswisi.


Prof. Kabudi amesema Serikali ya Tanzania imelenga pamoja na mambo mengine kuimarisha haki za binadamu, utawala bora na utii wa sheria nchini na kuondoa ukatili dhidi ya wanawake, watoto na watu wenye ulemavu.


“Serikali imelenga kuimarisha haki za binadamu, utawala bora, utii wa sheria na kuondoa ukatili dhidi ya wanawake, watoto na watu wenye ulemavu, kwa sasa tunatekeleza mpango mkakati wa kitaifa wa kuondoa ukatili dhidi ya wanawake na watoto wa mwaka 2017/18 – 2021/22, lengo likiwa ni kulinda na kudumisha haki za wanawake, watoto na watu wenye ulemavu,” alisema Prof. Kabudi.


Amesema Serikali pia inazingatia suala la kuwapatia haki kwa haraka wananchi wasio na uwezo kwa kutolea maamuzi kwa haraka mashauri yanayowahusu watu wasio na uwezo na kuwapatia msaada wa kisheria kupitia utekelezaji wa Sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka 2017 ili wananchi hao waweze kupata haki zao kwa wakati.


Aidha, Prof. Kabudi amelihakikishia Baraza hilo kuwa Serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na vyombo vya habari nchini na imeendelea kuhakikisha uhuru wa vyombo hivyo unalindwa huku jumla ya vituo vya redio 152, televisheni 34, magazeti 172  nchini kote yamesajiliwa na kuongeza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira stahiki yatakayowezesha vyombo vya habari kufanya kazi zao kwa uhuru.


Ameongeza kuwa Serikali imedhamiria kuleta ustawi wa jamii kwa kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo ikiongozwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025 na kunadi kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuhakikisha kuwa haki ya kupata elimu, afya na maji zinawafikia wananchi wote.


“Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuhakikisha kuwa haki ya kupata elimu, afya na maji zinawafikia wananchi wote na kuongeza kuwa Serikali inatumia zaidi ya Shilingi Bilioni 23 kwa mwezi kutoa elimu pasipo malipo na hivyo kuongeza udahili wa watoto wanaojiunga darasa la kwanza kwa asilimia 35.2 na asilimia 20.1 kwa wanaojiunga na kidato cha kwanza,” alisema.


Prof. Kabudi pia amesema Serikali imedhamiria kufikisha huduma za afya karibu na watanzania wote ambapo imeongeza bajeti ya afya kutoka Shilingi bilioni 31 mwaka 2015/2016 hadi Shilingi bilioni 269 mwaka 2017/2018 na kuongeza kuwa Serikali inatekeleza mikakati ya kujenga vituo vya afya ambapo hadi sasa imejenga vituo 304, na nyumba za watumishi wa afya 578 zimejengwa nchini kote.


Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa ni chombo cha Umoja wa Mataifa chenye jukumu la kukuza na kulinda haki za binadamu duniani kote na kushughulikia uvunjwaji wa haki za binadamu unaotokea katika nchi wanachama wa umoja huo na kushauri hatua za kuchukuliwa ili kuboresha haki za binadamu duniani.


Baraza hilo pamoja na mambo mengine linatarajia kupokea taarifa mbalimbali kuhusu haki za binadamu duniani na kutoa nafasi kwa viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kutoa maelezo yao kuhusu utekeelezaji wa wajibu wao wa kulinda na kukuza haki za biandamu katika nchi zao.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maofisa wa Tanzania mara baada ya kuhutubia kikao hicho cha Baraza la Haki za Binadamu jijini Geneva Uswissi.

WANANCHI WA MKOA WA TANGA WAAGIZWA KUTUNZA VYANZO VYA MAJI

Tenki hili limekamilika katika Halmashauri ya Kilindi na wananchi walianza kufurahia kupata maji. Matokeo yake Pampu imeungua. Waziri wa Maji Mhe. Profesa Mbarawa amemuagiza Mkandarasi kuhakikisha ananunua pampu mpya na kuifunga haraka iwezekanavyo na siyo kufanya ubabaishaji.

Mhandisi wa Maji wa Wilaya ya Lushoto Bw. Baraka Rajab akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa tenki lenye ujazo wa lita 650,000 linaloendelea kujengwa eneo la Magamba
..............................


Waziri wa Maji, Mhe. Profesa Makame Mbarawa (Mb) amewataka wananchi wa mkoa wa Tanga kwa ujumla kutunza vyanzo vya maji ili viwe endelevu kwa kikazi chetu na kizazi kijacho. Pia amewata watunze miundombinu na kulipa bili za maji kwa wakati.


Waziri Mbarawa aliyasema hayo alipokuwa akizunguka katika Halmashauri za Mkoa huo kukagua miradi ya maji inayotekelezwa katika Mkoa huo.


“Hakikisheni mnatunza vyanzo vya maji na kuvilinda, tusipofanya hivyo itakuwa tunafanya kazi bure hata hiyo miundombinu ambayo tunaijenga kwa gharama kubwa haita saidia maana maji yatakuwa hakuna bila kutunza vyanzo vyetu”, alisema Waziri Profesa Mbarawa.


“Hali ya upatikanaji wa maji katika Halmashauri ya Kilindi, Mkinga, Korongwe, Handeni hairidhishi hivyo basi serikali inafanya jitihada za makusudi ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata majisafi na Salama” alisema.


Akiwa Kilindi waziri alishuhudia kukuta mradi wa ujenzi wa tanki la maji umekamilika lakini pampu imeungua na wananchi hawapati maji. Waziri amemuagiza mkandarasi aliyejenga mradi huo kuhakikisha kuwa ifikapo Ijumaa tarehe 1 Machi, 2019 awe amefunga pampu hiyo na wananchi wapate huduma ya maji safi na salama.


Aidha, Waziri alisema katika maeneo mengi aliyopita ameona kuwa changamotoo kubwa ya miradi ya maji inasababishwa na wataalam wetu kwa sababu ya kuwapa fursa Wakandarasi ya kufanya chochote wanachotaka hivyo amewataka wataalam kuwa waadilifu na kusimamia miradi hiyo kwa ukaribu zaidi.


Ameeleza kuwa Wizara ipo katika mchakato wa kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini mfano wake kama TARURA ambaye anasimamia barabara za vijijini. Tunaamini TARURA anafanya vizuri na sisi tukienda kwenye mfumo huo wa kuwa na Wakala wa Maji Vijijini nasi tutafanya vizuri.


Akiwa katika mji wa Mombo Waziri Mbarawa alikutana na Mbunge wa jimbo hilo Mhe. Mary Chatanda ambaye alimueleza kilio kikubwa cha wananchi wake kuwa ni maji. 


Waziri alisema ameipokea changamoto hiyo na amemuahidi kuwa Wizara itatoa Shilingi Milioni 500 kwa ajili ya kumpatia Mkandarasi Saxon Building ili aendelee na ujenzi wa miradi ya Rwegela na Msambiazi iliyopo Korogwe mjini.


Waziri wa Maji, Mhe. Makame Mbarawa alipata fursa pia ya kuzungumza na wananchi wa Tanga kupita redio ya Tanga Kunani moja kwa moja. 


Wananchi wengi wa Tanga walitoa vilio vyao kuhusu kero ya maji hasa katika Halmashauri za Mkinga na Handeni na sehemu nyingine. 


Waziri ameahidi kuzifanyia kazi changamoto hizo na kusema kuwa hali halisi amejionea mwenyewe na Serikali itajitahidi kuondoa changamoto hizo ili wananchi wapate maji safi na salama.