Wednesday, October 17, 2018

DC BAGAMOYO ATAKA WANAFUNZI KIDATO CHA NNE KUJIANDAA NA MTIHANI.

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo, Zaynabu Kawawa. 
...........................

Na Omary Mngindo, Lugoba

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani Zaynabu Kawawa, amewataka wanafunzi wa sekondari ya Lugoba kujiandaa vyema na mithihani yao ya kidato cha nne, inayotaraji kufanyika mwanzoni mwa mwezi ujao.

Kawawa ameyasema hayo katika mahafari ya 27 shuleni hapo ambapo alisema maandalizi mazuri kwa ajili ya mitihani ndiyo itayowawezesha kufanya vyema, hatimae kufikia malengo waliyojiwekea, huku akiwataka wazazi kuchangia sekta hiyo ili kukabili changamoto zilizopo. 

Mkuu huyo aliongeza kwamba serikali inaendelea na uboreshaji wa sekta ya elimu sanjali na kuongeza walimu, kukarabati miundombinu hiyo ikiwemo utoaji wa fedha kila mwezi kutoka serikalini.

"Serikali inataka kuboresha zaidi elimu kuanzia ya msingi na sekondari, ili iwe sawa na ya wanafunzi wasio na ulemavu, hatua inayolenga kuwepo elimu jumuishi kwa wanafunzi wote pasipokubagua," alisema Kawawa.

Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuboresha sekta hiyo ikiwemo wanafunzi wenye ulemavu, huku akipongeza wadau waliojenga darasa la wanafunzi wa elimu maalumu hali inayopaswa kuungwa mkono.

Awali akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Abdalah Sakasa alimwambia Mkuu hiyo kuwa changamoto inayowakabili ni pamoja na gharama ya kununulia kemikali na vifaa vya maabara kipindi cha mitihani ya kitaifa.

Alisema kuwa shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1989 ikiwa ni shule za mwanzoni kwa sasa ina idadi ya wanafunzi wapatao 1,388, ambapi kati ya hao wanafunzi waliohitimu wakiwa 73 ambao ndio walioagwa kwenye mahafali hayo.

"Kwanza tunaishukuru serikali iliyoko madarakani chini ya rais Dkt. John Magufuli kwa kuendelea na utoaji wa fedha kwa ajili hiyo, lakini hazikidhi kutokana na gharama kuwa kubwa, tunaiomba kuangalia uwezekano wa kutuongezea ili kuongeza ufanisi wa masomo ya Sayasi", alisema Sakasa.

Aliongeza kwa kusema kwamva changamoto hiyo imekuwa kubwa, hasa ikizingatiwa kwamba shule hiyo ina wanafunzi wengi wanaosoma masomo ya Sayansi.

"Mbali ya changamoto hiyo, pia tunakabiliwa na uchakavu wa sakafu katika baadhi ya madarasa, utatuzi wake ni kuweka marumaru, kuuna madarasa 17 kila darasa moja linagharimu shilingi milioni mbili,"alimalizia Sakasa.
 
Hawa ni baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne Shule ya Sekondari Lugoba

SERIKALI IMEZITAKA HALMASHAURI KUANZISHA ONE STOP CENTRES KUPAMBANA NA VITENDO VYA UKATILI NCHINI

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Engineer Evalist Ndikilo  kuhusu masuala Afya pamoja na Maendeleo ya Jamii mapema leo ofisini kwake Kibaha Mkoani Pwani.
.........................................
Serikali imezitaka Halmashauri  zote Nchini kuhakikisha zinakuwa na vituo vya huduma za  mkono kwa mkono (Ones Stop Centre) ili kuunga mkono serikali katika juhudi zake za kupambana na vitendo vya ukatili hapa Nchini.


Hayo yamesema leo wilayani kibaha mkoani Pwani na Naibu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile alipotembelea kituo cha huduma za mkono kwa mkono kilichopo katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani.

Dkt. Ndugulile amesema kuwa lengo la vituo hivyo linalenga kupunguza mlolongo wa huduma kwa muhanga wa ukatili kwani vituo hivyo vinatoa huduma za matibabu, huduma za polisi na ushahuri wa kisaikolojia kutoka kwa Afisa Ustawi wa Jamii kwa wahanga wa ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.

Aidha Dkt. Ndugulile amesema nchi kwa sasa ina vituo kumi tu hivyo kutaka maeneo Mikoa mingine kuiga Mkoa wa Pwani kuunga mkono juhudi hizi kwa kuwa takwimu zilizopo zinaonesha Tanzania ina matukio ya ukatili 41,000 na kati ya matukio hayo 13,000 ni ukatili dhidi ya watoto akitaja hali hiyo kuwa ni ujambazi mpya dhidi ya binadamu.

Amezitaja juhudi nyingine za kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto kuwa ni kuwepo kwa madawati ya Jinsia katika vituo vya polisi akitaja idadi ya vituo hivyo kote Nchini kuwa ni jumla ya madawati 500.

Ameongeza kuwa Serikali inawajengea uwezomwalimu wa Shule za Msingi na Sekondari ili kuwa na madawati ya ukatili wa kijinsia kwani vitendo vingi vya ukatili kwa watoto vinatokea katika eneo la shule.

Dkt. Ndugulile pia ameitaka jamii kutofumbia macho vitendo vya ukatili vinavyotokea katika maeneo yao hasa nyumbana katika familia na amesema Serikali itawachukulia hatua watoa huduma za fya watakaojihushisha na uitoaji wa taarifa za uongo kuhusu mashauri ya vitendo vya ukatili.

‘’Baadhi ya wanajamii hapa nchini wanafurahia vitendo vya ukatili kwani wamekuwa wakimalizana kifamilia na kusababisha vitendo hivi kuendelea” alisisitiza Dkt. Ndugulile.

Naibu Waziri Ndugulile ameuagiza Mkoa wa Pwani pamoja na mikoa mingine Nchini kuanzisha dawati la ulinzi wa wanawake na watoto akiongeza kuwa ili ni agizo la serikali hivyo ni lazima mikoa yote Nchini inakuwa na madawati haya ili kutekeleza agizo la serikali.

Akiongea na watumishi wa hospitali ya Tumbi Dkt. Ndugulile amesema kumekuwepo  na kasumba ya adaktari ya kuficha ushahidi kwa watu waliofanyiwa vitendo vya ukatili na kuongeza kuwa hilo ni kosa kisheria na atakayebainika kuficha ushaidi adhabu yake ni kufutiwa usajili.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile yupo katika ziara yake ya siku mbili katika mikoa ya Pwani anmbapo anatembelea na kukagua huduma za afya na maendeleo ya jamii.
 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile pamoja na Mkurugezi Mkuu wa hospitali ya Tumbi Dkt. Edward Wayi akitoa maelezo ya Kituo cha Mkono kwa Mkono (one stop centre) kwa waandishi wa habali kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia mapema leo Tumbi Kibaha Mkoani Pwani.