Sunday, October 16, 2016

MBUNGE, RIDHIWANI KIKWETE ACHANGIA DAMU JIMBONI KWAKE.

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akiwa katika zoezi la kuchangia damu kwa ajili ya Mama na mtoto,jimboni humo.
 

Mbunge Ridhiwani akipata maelekezo kutoka kwa wahudumu wa afya katika zoezi hilo la kuchangia damu.
 

Mbunge Ridhiwani Kikwete wa katikati akiwa na Mwenyekiti wa CCM kata ya Chalinze wa kushoto Bwana Nassar Tamim na Mratibu wa zoezi hilo la uchangiaji damu Bwana Lazaro.
 

Mbunge wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akiwa na Diwani wa kata ya Pera wa kulia,na Mwenyekiti wa wakinamama Kata ya Pera Bi.Esther Laban  wakitembea kuangalia lambo la maji lililojaa matope.
 

Mbunge wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akisikiliza mmoja wa kina mama aliyesimama kuzungumza kuhusu kero wanazopata katika shughuli zao za ufugaji.
..................................


Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete,ameshiriki katika zoezi la kuchangia damu linalotambulika ‘’Changia Damu Salama kwa Mama na Mtoto’’lilifanyika jimboni humo ili kusaidia upatikanaji wa damu salama.

Akizungumza katika zoezi hilo Ridhiwani amesema kuwa amevutiwa na zoezi hilo na kuamua kujitolea kuchangia damu ili kumkomboa mama na mtoto.

Katika tukio lingine Ridhiwani amekutana na kufanya  mazungumzo na wakinamama wa jamii ya wafugaji wa kabila la wa Maasai ili kuangalia ni namna gani atasaidia kutatua changamoto zinazowakabili wafugaji katika jimbo hilo.

Aidha amepata nafasi ya kutembelea Lambo la maji lililojaa matope katika eneo la Pera ili kujionea hali halisi ya eneo hilo ili kusaidia kurudisha lambo hilo katika hali yake ya kawaida.


DIWANI VIGWAZA ATOA MSAADA WA DAWA ZA MILIONI 4.5 KWA ZAHANATI 2.

diwa2
Diwani wa kata ya Vigwaza Muhsin Baruan akimkabidhi dawa alizotoa msaada kuungana mkono juhudi za serikali kutatua changamoto za uhaba wa dawa  ,mganga mfawidhi wa zahanati ya Ruvu darajani ,Dkt. Gilbert Mkotigwa.
diwa3
Diwani wa kata ya Vigwaza Muhsin Baruan akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada wa dawa  mbalimbali katika zahanati ya Ruvu darajani na Vigwaza yenye thamani ya mil.4.5
...........................



DIWANI wa kata ya Vigwaza ,Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani, Muhsin Baruan ametoa msaada wa dawa za magonjwa mbalimbali katika zahanati mbili ya Vigwaza na Ruvu Darajani, zenye thamani ya mil.4.5.

Diwani huyo ametoa dawa hizo ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa dawa inazozikabili zahanati hizo ambapolengo ni kutatua changamoto hizo.

Aidha pamoja na  msaada huo, Baruan ametoa matofali 1,000 pamoja na mifuko ya saruji 30 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa nyumba ya mganga mfawidhi wa zahanati ya Ruvu Darajani.

Akikabidhi misaada hiyo ,katika zahanati hizo,alisema ataendelea kutatua matatizo yanayowakabili wakazi wa kata ya Vigwaza katika hudumambalimbali za kijamii, zikiwemo afya, maji, elimu pamoja na kusaidia makundi maalum ikiwemo vijana, walemavu, wanawake na wazee ili aweze kutimiza lengo  la kuchaguliwa  kwake na kutekeleza yale ambayo aliwaahidi wananchi wake.

Alisema fedha zilizotumika kununulia dawa hizo, mifuko ya saruji na matofali ni nguvu yake mwenyewe na ni moja ya ahadi zake alizoahidi kuzitatua ambapo umefika wakati sasa wakutimiza.

Aliongeza kuwa kwasasa watumishi wa afya katika zahanati hiyo wanaishi katika nyumba za kupanga na kupata kero hasa nyakati za usiku akitokea mgonjwa wa dharura.

Kufuatia hali hiyo aliwaomba wadau wa maendeleo, ya afya wajitokeze kushirikiana kujenga nyumba hiyo ili kuondoa kero ya kuishi mbali ya kituo hali inayopelekea madhara kwa wagonjwa na usumbufu kwa mganga.

Baruan aliishukuru serikali kwa kuingiza zahanati ya Ruvu Darajani na kuiomba ipeleke dawa kwenye zahanati kwa wakati ili kuwaondolea usumbufu wananchi.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kumtaka mganga mfawidhi katika zahanati ya Ruvu Darajani, afisa mtabibu zahanati ya Vigwaza, kuzitunza dawa hizo na  kuzitumia pale inapostahiki kwa uadilifu.

Kwa upande wake, mganga mfawidhi wa zahanati ya Ruvu Darajani, Gilbert Mkotigwa, alisema zahanati hiyo ilikuwa haijaingizwa katika mgao wa dawa kutoka bohari ya madawa (MSD) kwa miaka mitatu iliyopita tangu feb 2014 hadi sept 5 mwaka huu.

Alisema  katika kipindi hicho walikuwa wakisaidiwa na zahanati za jirani ikiwemo Visezi, Kidogozero, Milo, Vigwaza pamoja na wilaya ambayo ilikuwa ikitoa mgao kutokana na fedha za OC.

Dk,Mkotigwa alisema kutokana na uhaba huo wa dawa, Diwani aliomba orodha ya dawa zinazohitajika na kufanikiwa kuziwasilisha.

Alisema licha ya kupokea msaada huo lakini bado zahanati inakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo ukosefu wa nyumba ya mganga na watumishi wengine, wodi ya uzazi ambapo kwa sasa kina mama wanajifungulia katika chumba kidogo sana, mashine za kupimia wingi wa damu, sukari na haja kubwa.

Dk.Mkotigwa alisema kukosekana kwa mashine ya kupimia wingi wa damu kunasababisha wajawazito kwenda kupima wingi wa damu kituo cha afya Mlandizi ambayo imekuwa kero kwa wajawazito kufuata huduma hiyo mbali huku ikiwa ni kipimo muhimu kwao tangu kushika mimba hadi kujifungua.

Alimuomba diwani huyo kushirikiana na wahisani wengine kuangalia namna ya kusaidia upatikanaji wa vipimo hivyo na kutafutia ufumbuzi changamoto hizo ili kutoa huduma bora.

Alisema zahanati hiyo inahudumia wagonjwa katiya 400-500 kwa mwezi na wajawazito 10 hadi 15 katika kipindi hicho.

Afisa tabibu wa zahanati ya Vigwaza ,Alexander Ngalawa ,alisema zahanati hiyo ina hudumia vijiji vitano na ipo karibu na barabara kuu ya Morogoro-Dar-es salaam hivyo watu wengi kukimbilia kupata huduma ya afya.

Alisema bado wana upungufu wa madawa ,unaotokana na kupelekewa upungufu wa madawa wanayooda kupitia wilaya kwenda bohari na kusababisha upungufu katika mahitaji yao.

Dk.Ngalawa alieleza kwenye zahanati hiyo wapo watumishi watatu ambao hawatoshi ,mmoja akipata likizo wanabaki wawili ambao wanazidiwa na wagonjwa.