Mkuu wa Wilaya ya Oloililai, Rift Valley nchini Kenya Mhe. Andrew Mwiti Mathew amesema serikali ya Kenya haiungi Mkono wachochezi wa vurugu, ghasia na maandamano nchini Tanzania, akiahidi kuzuia Wakenya kuchochea na kushiriki kwenye vurugu na maandamano haramu.
Mhe. Mwiti amebainisha hayo leo Disemba 08, 2025 mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, wakati wa Kikao cha ujirani mwema kilichofanyika Wilayani Longido, ikihusisha Kamati za Ulinzi za Mkoa wa Rift Valley na Mkoa wa Arusha, kama sehemu ya kuimarisha usalama na biashara kwenye eneo la mpaka wa Namanga.
"Sisi tuwahakikishie kuwa tumejipanga vizuri kuzuia wachochezi na mtu yeyote ambaye anaweza kuwa na nia ya kuja kujiunga na wale watakaokuwa wanapanga kufanya maandamano ambayo tayari tumehakikishiwa kuwa ni haramu kwani hayajaruhusiwa kisheria." Amesisitiza Mhe. Mwiti.
Awali katika maelezo yake, Mhe. Makalla ameihakikishia Kenya kuwa serikali ya Tanzania imejipanga kikamilifu kuhakikisha hakuna vurugu wala matukio ya uvunjifu wa amani yatakayojitokeza kesho Jumanne Disemba 09, 2025, akiwataka wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii bila ya kuwa na wasiwasi wowote.
Mhe. Makalla kadhalika katika kikao hicho ameahidi kuwa serikali ya Tanzania itaendelea kuhakikisha mpaka wa Namanga unaendelea kuwa salama pamoja na kuheshimu mipaka iliyopo na kuimarisha ufanyaji wa biashara kupitia mpaka huo ili kuleta tija kwa wananchi wa nchi hizo mbili.





No comments:
Post a Comment