Sunday, October 29, 2023

TaSUBa KITOVU CHA MAFUNZO TASNIA ZA SANAA NA UTAMADINI NCHINI-DKT. BITEKO

 

Amefunga tamasha la 42 la Kimataifa la Utamaduni Bagamoyo.


Aipongeza Wizara kwa kutangaza utamaduni wa nchi.


Sanaa iwe nyenzo kuunganisha wananchi


Imeelezwa kuwa, Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) ni kitovu cha mafunzo katika tasnia za Sanaa na Utamaduni nchini na Serikali imeendelea kuiboresha taasisi hiyo kwa kutoa fedha za kuboresha miundombinu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia. 


Hayo yameelezwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko alipomwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na TaSUBa mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.


"Niwapongeze Wizara kwa kuitangaza nchi yetu kwa kupitia kazi mbalimbali za utamaduni, sanaa na michezo. Aidha nakupongeza Waziri na wafanyakazi wa Wizara yako kwa kazi kubwa mnayoifanya kila mwaka katika kuliandaa na kuliendesha Tamasha hili kwa kipindi cha miaka 42 sasa," amesema Dkt. Biteko.


Ameongeza kuwa, tamasha hilo lina hadhi kitaifa na kimataifa kwani limehusisha ushiriki wa vikundi vingi vya sanaa vya hapa nchini na vya kutoka nje ya nchi zikiwemo Zambia, Kenya, Burundi, Uganda, Botswana, Afrika Kusini, Canada na nyinginezo.


Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameipongeza taasisi hiyo kwa kukuza utalii wa kiutamaduni (cultural tourism) hapa nchini jambo linalofanya kuendelea kuvutia utalii wa ndani na nje ya nchi.


 "Nawakaribisha na kuwahimiza vijana wote wa kitanzania wenye vipaji vya sanaa kuchangamkia fursa hii kwani sanaa sasa ni ajira hivyo tuitumie vyema kupitia taasisi hii," amesisitiza Dkt. Biteko.


Vile vile, Dkt. Biteko ameitaka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuwa na Mipango mikakati ya kuwasaidia wasanii nchini ili kupitia sanaa hiyo waweze kunufaika kiuchumi na kuitangaza nchi. Amesisitiza wapewe ushirikiano ili Sekta hiyo iwe na mchango mkubwa katika Pato la Taifa.


Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amesema kuwa, tamasha hilo limekua na mafanikio makubwa kwa Bagamoyo na mkoa wa Pwani. Amesema wadau wamejitokeza kwa wingi na kulifanya liwe tamasha bora nchini.


Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa amesema kuwa, tamasha hilo ni fursa ya kutangaza utalii uliopo nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya nchi. Amesisitiza kuwa mwaka 2024 tamasha litakuwa kubwa kwa kuwaleta wadau wengi zaidi nchini.


Wengine walioshiriki kilele cha tamasha hilo ni Mkuu wa Chuo TaSUBa, Dkt.Herbert Makoye, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Halima Okash na Watendaji wa Taasisi za Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wadau wa Sanaa na Utamaduni. Maonyesho hayo ambayo hufanyika kila mwaka yalianza rasmi tarehe 26 mwezi huu na kilele chake ilikuwa Oktoba 28, 2023. 






MAGAZETI YA TANZANIA LEO TAREHE 29 OKTOBA 2023.

 








Saturday, October 28, 2023

ZAIDI YA BILIONI 4 KUTUMIKA UPANUZI WA BARABARA BUKOBA.

 

Na Alodia Babara


Bukoba. 


zaidi ya Shilingi bilioni 4.4 zitatumika katika upanuzi wa barabara ya lami ya njia nne yenye urefu wa kilomita moja katika manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.


Barabara hiyo ambayo tayari imeanza kutengenezwa itasaidia kuondoa kona kali na kupunguza mlima katika eneo la Nyangoye ambalo lilikuwa linasababisha ajali kwa wingi.


Kaimu meneja Wakala wa barabaraTanroads mkoa wa Kagera Mhandisi Ntuli Mwaikokesya akizungumza mbele ya waziri wa ujenzi Innocenti Bashungwa leo Oktoba 28, 2023 amesema, barabara hiyo inajengwa kilomita moja awamu ya kwanza kuanzia mzunguuko wa barabara ya Rwamisenyi hadi mtaa wa Mitagi.


Mhandisi Mwaikokesya amesema kuwa, mradi huo ulishaanza tangu Oktoba mosi, mwaka huu utatekelezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi Oktoba mosi, mwaka 2024 na mkandarasi atakayetekeleza mradi huo ni Abemlo Contractors Ltd.


“Kwa sasa shughuli tunazofanya ni kuhamisha miundombinu ya maji, umeme na simu na wananchi  wameondoa kwa hiyari nyumba zao na mkandarasi anaendelea na shughuli za kusawazisha eneo la mradi” amesema mhandisi Mwaikokesya.


Ameongeza kuwa, barabara hiyo itajengwa awamu nne awamu ya kwanza imeanza, ya pili ni kutoka mtaa wa Mitaga hadi stend kuu ya Bukoba mita 600, ya tatu ni mita 650 ambapo mita 400 kutoka mzunguko wa barabara ya Rwamishenye kwenda Muleba na mita 250 kutoka mzunguko wa barabara ya Rwamishenyi kuelekea barabara iendayo wilaya ya Misenyi na awamu ya nne ni kutoka stend kuu hadi Bandari ya Bukoba.


Aidha Waziri wa ujenzi Innocent Bashungwa amesema kuwa, kipande cha mita 600 kutoka mtaa wa Mitaga hadi stend kuu ya Bukoba ambacho kitatengenezwa awamu wa pili ataenda kumuomba Rais ili serikali iongeze fedha za kipande hicho kitengenezwa kwa awamu moja ambayo tayari imeishaanza.


“Kwa jitihada nzuri za serikali katika ujenzi wa stend kuu ya Bukoba ngoja nikatoe mrejesho kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwamba ule utamu wa barabara ya njia nne wa kilomita moja kuanzia Rwamishenyi usiishie Mitaga basi uje moja kwa moja ili awamu ya kwanza iishie stend kuu” amesema Bashungwa.


Jawil Mahamud ni mkazi wa manispaa ya Bukoba ambaye amesema kuwa, hata kama waliumia nyumba zao kubomolewa, lakini anapongeza kutengenezwa kwa barabara hiyo na kusema kuwa wanahitaji maendeleo na barabara hiyo ilishachukua maisha ya watoto na ndugu zao wengi, wanafurahi kupanuliwa kwake kwani itaepusha ajali zilizokuwa zinatokea eneo hilo.


Aresius Ntwara mkazi wa Hamugembe manispaa ya Bukoba alisema, barabara hiyo ilikuwa finyo hivyo serikali kuipanua kutoka njia mbili kwenda njia nne pamoja na kuondoa changamoto ya ajali pia itasaidia hata mji wa Bukoba kukua kimaendeleo





MAGAZETI YA LEO TAREHE 28 OKTOBA 2023.

 KURASA ZA MBELE











KURASA ZA NYUMA.










Friday, October 27, 2023

DKT. TULIA ACKSON ACHAGULIWA KUWA RAIS WA MABUNGE DUNIANI.

 

Spika wa Bunge la Jamahuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Tulia Ackson amechaguliwa kuwa Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) katika uchaguzi uliofanyika leo Oktoba 27, jijini Luanda nchini Angola.


Dkt. Ackson amechaguliwa kwa kupata kura 172 kati ya kura 303 zilizopigwa na anarithi mikoba ya rais aliyemaliza muda wake, Duarte Pacheco kutoka Ureno aliyekuwa rais wa IPU kwa mihula mitatu.


Tulia alipata ubunge nchini Tanzania mwaka 2015, na baadae kuchaguliwa kuwa Naibu Spika na hatimae Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Akizungumza mara baada ya uchaguzi huo, Dk Tulia Ackson amesema, “Asanteni kwa kuniamini kwa kunichagua, naipokea nafasi hii kwa unyenyekevu huku nikitambua majukumu yote yanayoambatana na nafasi hii, napenda kuwathibitishi tena kuwa,  jitihada zangu za kufanya kazi mkono kwa mkono na wote ili kuifanya IPU iwe na ufanisi zaidi, yenye kuwajibika na uwazi.”

Wabunge wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) walipiga kura ya siri, huku kukiwa na wagombea wanne, ambapo rais mpya Dkt. Tulia Ackson, alipata kura 172 sawa na asilimia 57 ya kura zote zilizopigwa, huku wagombea wengine ni Catherine Gotani Hara kutoka Malawi, aliyepata kura 61, Adji Diarra Mergane Kanouté, kutoka Senegal, aliyepata kura 59, na Marwa Abdibashir Hagi kutoka Somalia aliyeambulia  kura 11. Wote wakiweka historia ya kuwa wabunge wanawake kutoka Afrika, waliogombea nafasi hiyo.

Dkt. Tulia Ackson anakuwa Rais wa 31 wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) na anakuwa mwanamke wa tatu kushika nafasi hiyo baada ya Najma Heptulla kutoka India (1999–2002) na Gabriela Cuevas kutoka Mexico (2017–2020), pia Dkt. Dulia Ackson anakuwa mwanamke wa kwanza kutoka Afrika kushika nafasi hiyo.



Umoja wa Mabunge Duniani IPU inachagua Rais baada ya kila miaka mitatu na lazima anaechaguliwa awe mbunge katika kipindi atakachokuwa Rais.
Rais mpya wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) Dkt. Tulia Ackson akihutubua mara baada ya kuchaguliwa kuwa Rais wa IPU.
Dkt. Tulia Ackson akipongezwa mara baada ya kutangazwa mshindi.
Baadhi ya wabunge wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) wakimpongeza Dkt. Tulia Ackson kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Umoja huo.







MSIGWA AZINDUA RASMI TAMASHA LA SANAA BAGAMOYO.

 



KATIBU Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa amefungua rasmi Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililohudhuriwa na wananchi na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi ambapo alisema kuwa Utamaduni na Sanaa ni Sekta zenye umuhimu mkubwa katika kuleta maendeleo na kukuza ajira hapa nchini.

Katibu Mkuu Bw. Msigwa amesema hayo usiku wa Oktoba 26, 2023 wakati akifungua rasmi tamasha hilo linaloendelea katika viwanja vya Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa).

"Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua kwamba eneo la Sanaa katika nchi yetu ni la kimkakati, ni lazima tulitumie kimkakati, naomba sana vijana wenye vipaji wasizuiliwe kufanya Sanaa, huku nako kuna ajira" amesisitiza Katibu Mkuu Bw. Msigwa.

Hafla ya ufunguzi wa Tamasha hilo ambalo linafanyika kwa siku tatu kuanzia Oktoba 26 - 28, 2023 katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBA) limehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Bodi ya taasisi hiyo Bw. George Yambesi, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa Dkt. Emmanuel Ishengoma, viongozi na wakazi wa Wilaya ya Bagamoyo.

Baadhi ya Wasanii na vikundi vilivyofungua tamasha hilo ni pamoja na:
Wamwiduka Band, Worrious from the East, msanii Vitalis Maembe, na wengine wengi.


Wednesday, October 25, 2023

WAJASIRIAMALI WAHIMIZWA KURASIMISHA BIASHARA BRELA

 


Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.

MKUU wa Wilaya ya Ubungo, Mhe. Hashim Komba amewataka wajasiriamali wanaoshiriki katika maonesho ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni, (BRELA) na wadau wake kutumia fursa hiyo kurasimisha biashara zao ili biashara zao ziweze kukua.

Mhe. Komba ametoa rai hiyo  Oktoba 24, 2023 wakati akifungua Maonesho ya kwanza ya BRELA na wadau wake, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, kwenye viwanja vya Mlimani City jijini Dar es Salaam. 

“Wito wangu kwenu BRELA na wadau wengine wa maonesho haya ni kwamba tuhakikishe hawa wajasiriamali mbalimbali wanakua, hivyo wasaidiwe kwa kupatiwa elimu ili waweze kurasimisha biashara zao,” amesema Mhe. Komba.

Amesema ili kuboresha zaidi maonesho haya BRELA iendelee kuandaa maonesho kama haya katika maeneo mengine yatakayowezesha wadau wengi zaidi kufikiwa. Ameyataja maeneo ambayo yana idadi kubwa ya wajasiriamali katika Wilaya ya Ubungo kuwa ni Mbezi na Manzese, hivyo BRELA itoe kipaumbele kwa kuwapatia elimu kupitia maonesho kama haya. 

Pia ameitaka BRELA kuimarisha mahusiano na mazuri na taasisi zingine za Serikali hususan Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na Serikali za Mitaa ambazo ndizo zinazowakutanisha wafanyabiashara wadogo, wa kati na wakubwa. 

Mhe. Komba amesema Maonesho haya pia yatumike kufanya tathmini ya huduma zinazotolewa sambamba na kuwa na madawati yanayowakutanisha wadau ili kupunguza watu wa kati (Vishoka) ambao wamekuwa kikwazo kikubwa kwa wafanyabiashara. 

“BRELA, Tume ya Ushindani (FCC), Shirika la Viwango Tanzania(TBS) pamoja na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) shirikianeni katika utoaji wa elimu ili kudhibiti na kupambana na Bidhaa bandia, kuthibitisha ubora wa bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali na kuhakikisha wanafanya sajili mbalimbali na kupata leseni," amesema Mhe. Komba.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA Bw. Godfrey Nyaisa amesema BRELA itaendelea kuwahamasisha wadau wake kurasimisha biashara zao kupitia majukwaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kushiriki katika maonesho. 

Maonesho ya BRELA na wadau wake ambayo yatahitimishwa na mkutano wa Wadau tarehe 27 Oktoba, 2023 katika ukumbi wa Mlimani City jijini Da es Salaam, kauli mbiu yake ni "Urasimishaji Bashara katika Mapinduzi ya Nne ya Viwanda." 

Tuesday, October 24, 2023

BODI MPYA YA USHAURI YA WIZARA YA AFYA (MAB) KWA TMDA YAZINDULIWA

 

Na. WAF - Dodoma 


Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu Oktoba 23, 2023 amezindua rasmi bodi mpya ya ushauri ya Wizara ya Afya (MAB) kwa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ambayo inawajumbe Saba. 


Waziri Ummy wakati akizindua bodi hiyo mpya amewataka wajumbe hao kuimarisha usimamizi wa TMDA katika upande wa dawa, vifaa na vifaa tiba ili kusiwepo na upotevu wa aina yoyote wa vifaa tiba hivyo. 


“Kazi kubwa mnayotakiwa kufanya ni ufuatiliaji wa mara kwa mara wa bidhaa duni na bandia zinazoingia kwenye soko ili zisiwafikie wananchi wakazitumia”. Amesema Waziri Ummy 


Lakini pia wakati akifungua bodi hiyo Waziri Ummy amewataka wajumbe hao kuharakisha utoaji wa vibali na leseni mbalimbali ili kutokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara wa dawa, Vifaa na Vifaa Tiba. 


“Kwakweli niwapongeze kwa hili bodi iliyomaliza muda wake, sikusikia malalamiko ya mtu kucheleweshewa leseni au kibali cha kufanya biashara hivyo bodi hii mpya mkaliendeleze hili”. Amesema Waziri Ummy 


Aidha, Waziri Ummy amepongeza bodi iliyopita kwa kufanya kazi zake kwa weledi ambalo TMDA imepiga hatua kubwa kwenye masuala mbalimbali ndani na nje ya chi na mafanikio ambayo Wizara pia inajivunia kuyafikia na kuitaka bodi mpya kuendeleza mazuri hayo. 


“Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana kwa bodi iliyopita ni pamoja na kuboresha mifumo ya utoaji huduma kwa wananchi ikiwemo mifumo ya TEHAMA kwenye kutoa vibali vya uingizaji bidhaa nchini ambapo sasa vibali vinatolewa ndani ya masaa 24”. Amesema Waziri Ummy


Bodi hiyo iliyoundwa na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu ina wajumbe Saba ambayo inaongozwa na Mwenyekiti aliyeongezewa muda kwa kipindi kingine Bw. Erick Shitindi, Prof. Appolinary Kamuhabwa (Mjumbe) ambae ni Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS).


Pia, Bi. Mariam Mwanilwa (Mkurugenzi wa Mishahara na Maslahi ya Watumishi wa Umma-Ofisi ya Rais Utumishi), CPA Chiku Thabit Yusuf (Mkuu wa Kitengo cha Uhasibu Shirika la Hifadhi ya Jami (NSSF), Wakili Patricia Maganga (Mwanasheria Mbobezi).


Vile vile yupo Bw. Daudi Msasi (Mfamasia Mkuu wa Serikali) na Bw. Adam M. Fimbo ambae ni Katibu lakini pia ni Mkurugenzi Mkuu wa TMDA. 





MAGAZETI YA LEO TAREHE 24 OKTOBA 2023

 KURASA ZA MBELE















KURASA ZA NYUMA