Monday, August 14, 2023
MAKAMU WA RAIS DKT. MPANGO AWAHIMIZA WATANZANIA KUFANYA KAZI KWA BIDII.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amewahimiza waumini na Watanzania kwa ujumla kuendelea kufanya kazi kwa bidii katika kilimo, ufugaji, biashara na kutumikia umma kwa uadilifu ili kuchangia katika ujenzi wa Taifa.
Makamu wa Rais ametoa wito huo mara baada ya kushiriki Misa Takatifu katika Kanisa Katoliki la Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Parokia ya Kiwanja cha Ndege mkoani Dodoma, Misa iliyoenda sambamba na Maadhimisho ya miaka 47 ya Parokia hiyo. Amewasihi viongozi wa dini kutokatishwa tamaa na makwazo mbalimbali wanayokutana nayo katika utume wao na kuendelea kuombea jamii na Taifa zima ili Mwenyezi Mungu aendelee kujalia amani na ustawi.
Makamu wa Rais amesema hali ya maadili katika Taifa kwa ujumla hairidhishi ikishuhudiwa kuporomoka kwa maadili na kuongezeka kwa vitendo visivyompendeza Mungu. Ametoa wito kwa wazazi, walezi na walimu kusimamia kiadilifu malezi na makuzi ya watoto na vijana kwa manufaa ya Taifa zima.
Halikadhalika Makamu wa Rais amewataka vijana na watoto kuwa na heshima na adabu ili kuweza kukua vizuri na kufanikiwa maishani. Amesema heshima hiyo inapaswa kuwa kwa wazazi, nyumba za ibada, serikali pamoja na mamlaka zingine ambazo zimewekwa na Mungu hapa Duniani.
Katika ibada hiyo pia kumezinduliwa kanisani hapo sanamu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu pamoja na kufanyika kwa sherehe ya kumbukumbu ya Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Msimamizi na Mwombezi wa Parokia hiyo.
Ibada hiyo imeongezwa na Padre Africanus Kimario akisaidiwa na Paroko wa Parokia hiyo Padre Emmanuel Mutambo na Mapadre wengine na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini na serikali.
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
13 Agosti 2023
Dodoma.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akishiriki Misa Takatifu katika Kanisa Katoliki la Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Parokia ya Kiwanja cha Ndege mkoani Dodoma, Misa iliyoenda sambamba na Maadhimisho ya miaka 47 ya Parokia hiyo leo tarehe 13 Agosti 2023.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akizungumza na waumini pamoja na viongozi mbalimbali wa dini na serikali mara baada ya kushiriki Misa Takatifu katika Kanisa Katoliki la Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Parokia ya Kiwanja cha Ndege mkoani Dodoma, Misa iliyoenda sambamba na Maadhimisho ya miaka 47 ya Parokia hiyo leo tarehe 13 Agosti 2023.
RAIS DKT. SAMIA AWAKARIBISHA MADAKTARI BINGWA KUTOKA MAREKANI.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Agosti 13, 2023 amewakaribisha Madaktari Bingwa wa Mifupa kutoka nchini Marekani katika hafla ya chakula cha mchana Ikulu Chamwino Dodoma.
Rais Samia amewashukuru madaktari hao kwa moyo wao wa kujitolea kuwasaidia Watanzania kupata huduma za matibabu ya kibingwa.
Madaktari hao bingwa wameweka kambi katika Hospitali ya Serian Lutherani Jijini Arusha ambapo wanatoa matibabu ya kubadilisha nyonga na goti bure kuanzia Agosti 11 mpaka 17, 2023.
Hafla hiyo imehudhuriwa pia Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu, Viongozi waandamizi wa Wizara Taasisi za Afya, Madaktari pamoja na wadau wengine wa Sekta ya Afya nchini.
Saturday, August 12, 2023
Friday, August 11, 2023
SAFARI YA WACHIMBAJI NCHINI CHINA KULETA TIJA – DKT. KIRUSWA
Naibu Katibu Mkuu Ataka watumie ziara kujifunza
Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa ameutaka ujumbe wa wadau wa Sekta ya Madini wapatao 100 wakiwemo wachimbaji wadogo, wachimbaji wa Kati, Wafanyabiashara wa madini na watoa huduma migodini wanaotarajia kwenda nchini China kuhakikisha safari hiyo inaleta matunda kwa kuleta wawekezaji wengi na kupata vifaa vya kisasa ili kuongeza uzalishaji wa madini nchini.
Wadau wengine, wanaoshiriki katika ziara hiyo ni wataalam wa madini kutoka taasisi za Wizara ya Madini, taasisi za Fedha ikiwemo Benki ya CRDB na wadau wengine muhimu.
Dkt. Kiruswa ameyasema hayo katika hafla fupi ya kuiaga timu hiyo Agosti 11, 2023 jijini Dar es Salaam, ambapo amesema kuwa, ubalozi wa China kwa kushirikiana na Kampuni ya Touchbroad ya nchi hiyo imeandaa ziara ya wachimbaji kutoka Tanzania ili kuwawezesha kukutana na wawekezaji wa Sekta ya Madini nchini China, kutembelea viwanda vya kutengeneza mitambo na vifaa vya uchimbaji na uchenjuaji wa madini na kuwawezesha kupata uzoefu na wafanyabishara wa madini waliopo China na kupata teknolojia za uchimbaji na uchenjuaji.
"Niwaombe kila mmoja wenu akiwa China ahakikishe anatimiza malengo yake kadri anavyoweza ili ujuzi mtakaoupata uje kuwasaidia kuboresha biashara zenu na kuongeza tija,” amesema Dkt. Kiruswa.
Vile vile, amezipongeza taasisi za fedha kwa kuendelea kuwasaidia wachimbaji na wafanyabiashara katika kuhakikisha wanapata mikopo ya fedha kwa kuwa karibu na wafanyabiashara wa madini na amewataka kuangalia uwezekano wa kupunguza riba ili kupata wateja wengi na kuruhusu wachimbaji wadogo kupata mikopo yenye riba ndogo.
Kwa upande mwingine, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amewataka wachimbaji hao kutumia ziara hiyo kujifunza na kupata uzoefu watakapotembelea viwanda vya kutengeneza mitambo na vifaa vya uchimbaji.
Naye, Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji wa Madini nchini (FEMATA), John Bina amesema kuwa, ziara hiyo nchini China inakwenda kufungua milango ya nchi kuvutia wawekezaji wengi kuendelea kuja kwa kuwa nchi ina sera nzuri katika uwekezaji.
Viongozi wengine walioshiriki ni pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Madini Kheri Mahimbali, Mbunge wa Viti Maalum Iringa Dkt. Rita Kabadi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dkt. Venence Mwasse, Mjumbe wa Bodi ya STAMICO Lucas Seleli, mwakilishi wa benki ya CRDB pamoja na wataalam kutoka Wizara na taasisi zake katika safari inayolenga kukutana na wawekezaji wa Sekta ya Madini nchini China.

























































