Friday, September 20, 2019

RC NDIKILO AMUAGIZA RMO KUOMBA KIBALI KUCHUNGUZA MTOTO ALIYECHOMWA SINDANO NA KUMSABABISHIA KUPOOZA

NA MWAMVUA MWINYI, KIBAHA.

MKUU wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo amemuagiza Mganga Mkuu wa mkoa (RMO) kuandika barua kuomba kibali Wizara ya afya ili kutuma tume kuchunguza mtoto aliyechomwa sindano na kupooza mguu. 

Ndikilo aliyasema hayo mjini Kibaha wakati alipofanya mkutano wa wazi wa kusikiliza matatizo na kero mbalimbali za wananchi ambapo mama wa mtoto huyo Asha Juma alitoa kilio cha mwanae mbele ya mkuu huyo wa mkoa. 


Akielezea juu ya tukio la mwanae aitwaye Abbas Msosa (14) ambaye anasoma kidato cha kwanza shule ya sekondari Bundikani Wilayani Kibaha, Asha Juma, alisema kuwa mwanaye alikuwa akiumwa na alimpeleka kituo cha afya mkoani kwa ajili ya matibabu. 


Asha alisema kuwa alipokuwa anapatiwa matibabu alichomwa sindano ambayo ilimsababishia maumivu na kusababisha mguu wake kupooza kutokana na kuchomwa sindano ya Quinine alipokuwa akiumwa Malaria miaka tisa iliyopita.


“Naomba suala langu lishughulikiwe kwani hata majibu ninayopewa na waliohusika na suala la mtoto wangu wananipa majibu ambayo hayaridhishi ninachokitaka ni kupata haki ya mtoto wangu ambaye amepata matatizo kutokana na matibabu aliyopewa,” alisema Asha Juma.


“Nimezunguka sana kwenda kwenye kituo hicho cha afya cha Mkoani lakini sipati majibu yanayoeleweka nakuomba unisaidie nateseka sana kwani nahangaika na mwanangu na sina msaada wowote nakuomba unisaidie nipate haki ya mwanangu,” alisisitiza kwa masikitiko Bi Asha Juma.


Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa suala hilo analifahamu kuwa mtoto wake alipatiwa matibabu kwenye kituo hicho cha afya na baada ya mwanae kuchomwa sindano alipatwa na tatizo hilo.


“Lifanyiwe kazi na kama kuna mtu ambaye alizembea na kusababisha tatizo hili ili hatua za kinidhamu zichukuliwe kwani kwa sasa hatuwezi kutoa majibu kujua kama ni uzembe au la hili likitolewa ufafanuzi na wataalamu itakuwa ni vizuri ili liweze kwisha kwani lazima kuwe na majibu ambayo yatakuwa ni ya kitaalamu,”alisema Ndikilo.


Alisema kuwa suala hilo limekuwa la muda mrefu sana na mama huyo amekuwa akihangaika sana na ameshafika ofisini kwake mara kwa mara na ameshamsaidia hivyo kuna haja ya kuhakikisha linafikia mwisho ili naye aweze kuridhika kwani anaona kama hajapata haki yake.

MAGAZETI YA LEO SEPTEMBA 20, 2019.

Thursday, September 19, 2019

DC, ZAINABU AITAKA HALMASHAURI YA BAGAMOYO KUONGEZA KASI YA KUKUSANYA MAPATO.

Mkuu wa Wialay ya Bagamoyo, Bi Zainabu Kawawa ameitaka Halmashauri ya Bagamoyo kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi na ushuru wa Serikali ili kuongeza mapato ndani ya Halmashauri hiyo.


Mkuu huyo wa wilaya ameyasema hayo katika kikao cha Baraza la madiwani cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2018/19 kilichofanyika ukumbi wa Halmashauri hiyo.


Alisema katika Halmashauri mbili zilizopo wilayani humo, Halmashauri ya Chalinze inaendelea kufanya vizuri katika kukusanya mapato huku akiinyooshea kidole Halmashauri ya Bagamoyo kwa kuzorota katika ukusanyaji wa mapato.


Alisema Taasisi zote za serikali wilayani humo kwa sasa makusanyo yao ni mazuri ikilinganishwa na awali lakini Halmashauri ya Bagamoyo imerudi nyuma katika ukusanyaji wa mapato.


Aidha, aliwataka madiwani ambao katika maeneo yao ndio kuna vyanzo vya mapato kutoa ushirikiano na watendaji kata na wenyeviti wa vitongoji ili kurahisisha ukusanyaji wa mapato.


Alisema Halmashauri ya Bagamoyo bado ina vyanzo vingi vya mapato ambavyo vikitumika vizuri vitaweza kuiingizia mapato Halmashauri hiyo.


Alitoa onyo kwa watumishi wa serikali ambao hawawajibiki katika nafasi zao na kwamba atakaebainika kuwa yeye ni sababu ya kushuka kwa mapato ya Halmashauri hiyo, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ikiwa ni pamoja na kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi ili atoe maelezo ya kutosha.


Aliongeza kwa kusema kuwa, uendeshaji wa serikali unategemea mapato hivyo kuzembea katika ukusanyaji wa mapato ni kurudisha nyumba maendeleo.

Sehemu ya madiwani wa Halmashauri ya bagamoyo wakifuatilia hutuba ya Mkuu wa wilaya
katika kikao cha Baraza la madiwani cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2018/19 kilichofanyika ukumbi wa Halmashauri hiyo.
Wakuu wa idara wa Halmashauri ya bagamoyo wakifuatilia hutuba ya Mkuu wa wilaya
katika kikao cha Baraza la madiwani cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2018/19 kilichofanyika ukumbi wa Halmashauri hiyo.
Watendaji kata wa Halmashauri ya bagamoyo wakifuatilia hutuba ya Mkuu wa wilaya
katika kikao cha Baraza la madiwani cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2018/19 kilichofanyika ukumbi wa Halmashauri hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, Ally Ally Issa (kulia) na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Bi Fatuma omari Latu, wakijadili jambo kwenye kikao hicho chacha Baraza la madiwani cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2018/19 kilichofanyika ukumbi wa Halmashauri hiyo.