Tuesday, September 17, 2019

RIDHIWANI KIKWETE AKABIDHI VITAMBULISHO VYA MATIBABU BURE KWA WAZEE.

Na Shushu Joel, Chalinze.

MBUNGE wa jimbo la Chalinze, wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete amewakabidhi wazee zaidi ya 500 vitambulisho vya matibabu bure katika jimbo lake.

Akizungumza na wazee wa kata ya Lugoba mara baada ya kuwakabidhi vitambulisho hivyo Kikwete alisema kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha wazee wote nchi nzima wanapatiwa vitambulisho hivyo ili kuondokana na suala la kulipia huduma za Afya.

Alisema kuwa Vitambulisho hivi vitawafanya wazee wa Chalinze kutibiwa bure na bila bugudha ya aina yeyote ile.

Aliongeza kuwa Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli, imejidhatiti kuhakikisha kila jambo lililoahidiwa kwa wananchi linatekelezeka kwa wakati kwa kusudi la kuwaondolea wananchi wanyonge changamoto zao kwa vitendo.

"Naipongeza Serikali yangu kwa jinsi inavyopambana na maendeleo pia utoaji wa huduma kwa wananchi wake kwani wazee wetu ni haki zao kupata Vitambulisho na wamevipata ili kupata huduma hiyo bure" Alisema Ridhiwani Kikwete.


Aidha aliongeza kuwa Wazee kupatiwa vitambulisho ni haki yao kutokana na kuwa Wazee hao walijitoa kwa hali na Mali enzi za ujana wao katika kulipambania taifa hili hivyo Serikali kuwapatia vitambulisho kwa ajili ya matibabu bure ni haki yao.

Kikwete aliwataka Wazee hao kuhakikisha wanavitunza vitambulisho hivyo ili visichakae wala wasivipoteze kwani itakuwa ni changamoto kupatikana kwa wakati.

Aidha Mbunge huyo ametoa wito kwa wauguzi wote wa halmashauri ya Chalinze kuhakikisha wanawapa kipaumbele kwa kuwapatia matibabu ya haraka ili waondoke mapema  wapate muda wa kupumzika.

Kata ambazo wazee wamepatiwa vitambulisho ni Lugoba, Msoga, Pera, Talawanda, Ubena, Miono, Vigwaza na Msata.

Kwa upande wake Muhammed Mzimba amempongeza mbunge wa jimbo hilo Ridhiwani Kikwete Kwa kuwapa kipaumbele wazee wa jimbo zima ili kuhakikisha wanapata huduma za matibabu bure katika vituo vya afya na sehemu zote zinazotoa huduma za kiafya Kwa wazee.

Aliongeza kuwa Kwa sasa wazee hao watatembea kifua mbele kutokana na jinsi serikali ya awamu ya Tano inavyowajali wazee Kwa kupatiwa huduma za afya bure.

Aidha Mzee huyo alisema kuwa mara baada ya kupokea vitambulisho hivyo vitawasaidia sana na kuhakikisha watavilinda na watavitunza ili viendelee kutumika kwenye upande huo wa Afya.

Naye Bi Fatma Musa mkazi wa Msata (62) amewaomba wauguzi kutoa matibabu bila ubaguzi ili nao wajisikie kama wanavyopatiwa huduma watu wengine wenye umri wa chini yao.

Aidha amempongeza Mbunge Ridhiwani Kikwete kwa juhudi zake za kuwapambania wazee wa jimbo lake katika kuhakikisha wanapatiwa huduma ya matibabu bure.

RC. PWANI AMFAGILIA MKURUGENZI WA AZANIA BANK KWA KUUNGA MKONO SERA YA VIWANDA.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo kulia akisalimiana na kumpongeza Mkurugenzi wa Benki ya Azania, Charles Itembe kwa kusapoti masuala ya uwekezaji  mara baada ya kumalizika kwa halfa ya uwekaji wa jiwe la msingi katika kiwanda cha kutengeneza vifungashio kilichopo katika kata ya Pangani Wilayani Kibaha.
.......................................
NA MWANDISHI WETU, PWANI.

WAWEKEZAJI wa  sekta ya viwanda wametakiwa kuhakikisha wanazingatia sheria na taratibu zote za kazi na kuachana na vitendo vya kuvunja sheria za nchi kwa kuamua kuwanyanyasa wafanyakazi wao kwa kuwanyima haki zao za msingi ikiwemo kuwapatia huduma ya matibabu, pamoja na kuwapatia maslahi yao kama inavyotakiwa bila ya  kuwa na vitisho vyovyote ili kutimiza azma ya serikali ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu  wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja  kwa ajili ya uwekeji wa  jiwe la msingi katika kiwanda cha kutengenezea vifungashio (WANDE PRINTING)  vitumikavyo katika sekta ya chakula, kilimo, viwanda, afya,  ujenzi pamoja na kiwanda  ambacho kinajengwa katika  eneo la  kata ya Pangani Wilayani Kibaha na kuwaasa watendaji na mamlaka zinazohusika kuwapa ushirikiano wa kutosha wawekezaji hao bila ya ubaguzi na ubinafsi  wowote.

Ndikilo alisema kwamba serikali ya awamu ya tano lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana na wawekezaji mbali mbali wa ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Jojn Pombe Magufuli, hivyo wafanyakazi wanatakiwa kupewa haki zao stahiki bila ya kuonewa hasa katika suala la vitendea kazi pindi wanapokuwa katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

“Katika Mkoa wa Pwani kwanza nashukuru kwa sasa tunaendelea kushirikiana na wawekezaji wazawa ambao wamekuwa na nia ya kuendelea kuwekeza katika sekta ya viwanda katika maeneo mbali mbali.

"Lakini kila siku Rai yangu kubwa ni kuwapa haki zao zote waafanyakazi kwani wao ndio wapo mstari wa mbele katika kuzalisha bidhaa, kwa hivyo katika hili naomba sana kwa wawekezaji kuliangalia kwa jicho la tatu.” alisema Ndikilo.

Aidha Mkuu huyo aliipongeza Benki ya Azania kwa kuweza kuonyesha uzalendo kwa kushirikiana bega kwa bega na serikali ya awamu ya tano katika kutoa msaada wa kuwawezesha mikopo wawekezaji ikiwemo kiwanda hicho  kwa lengo la kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kwa wananchi kupitia sekta ya viwanda.


Kwa upande wake mmoja wa wawekezaji wazawa katika kiwanda hicho John Obach akisoma risala kwa mgeni rasmi kwa niaba viongozi wenzake amebainisha kuwa ujenzi wa mradi huo umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 6.6 na kwamba wanatarajia kutoa ajira zaidi ya 300 ambazo zitaweza kuwasaidia wananchi kujikwamua kiuchumi na kuondokana na wimbi la umasikini.

Naye  Mkurugenzi wa Azania Benki Charles   Itembe ambao ndio wamewezesha kwa kiasi kikubwa  ujenzi wa mradi huo wa kiwanda  amesema kwamba lengo lao kubwa ni kuunga mkono  sera ya Rais wa awamu ya tano Dkt. John Pombe Magufuli ya kuwa na uchumi wa viwanda na kuahidi kuendelea kushirikiana na wawekezaji wengine katika kuinua sekta ya viwanda.


“Sisi kama  taasisi ya kifedha Azania Benki nia na madhubmuni yetu makubwa ni kuhakikisha tunaaunga sera ya Rais wetu wa awamu ya tano Dkt. John Pombe Magufuli katika kuwa na Tanzania ya viwanda, kwa hivyo ndio maana tumeamua kuwawezesha wenzetu wa kiwanda hiki cha kutengenezea vifungashio ili kuleta mapinduzi ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Aliongeza kwa kusema kuwa, kwa sasa wataendelea kutoa misaada kwa wadau wa maendeleo pamoja na serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa mbali mbali za ajira kupitia miradi ya ujenzi ywa viwanda ambavyo vinajengwa katika maeneo tofauti lengo ikiwa ni kuondokana na wimbi la umasikini na kujikwamua kiuchumi.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani  Mhandisi Evarist Ndikilo wa kulia akipeana mkono na Mwenyekiti wa makampuni ya Global Packaging na Wande Printing Joseph Wasonga  mara baada ya kumalizika kwa zoezi la uwekaji wa jiwe la msingi katika kiwanda cha kutengenezea vifungashio kilichojengwa Wilayani Kibaha.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akikagua moja ya bidhaa ambazo zinazalishwa katika kiwanda cha Wande Printing ambacho kinatengeneza vifungashio wakati alipofanya ziara yake ya kikazi kwa ajili ya uwekaji wa jiwe la msingi katika kuwanda hicho. 
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarit Ndikilo  akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbali mbali wa serikali, viongozi wa kiwanda hicho pamoja na wadau mbali mbali wa maendeleo ikiwemo Mkurugenzi wa benki ya Azania kulia kwake Charles Itembe.