Tuesday, September 19, 2017

DC. KIBAHA- WAMILIKI WA VIWANJA 943 KUFUTIWA HATI ZAO.

SAM_5568
Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama amesema Serikli wilayani Kibaha ,mkoani Pwani inatarajia kufuta umiliki wa viwanja vya watu binafsi pamoja na taasisi 943 baada ya kushindwa kutekeleza agizo la kwenda kujisalimisha ndani ya mwezi mmoja wilayani humo ili kueleza mpango kazi kwa kila mmiliki .

Aidha inawaomba wawekezaji kujitokeza kwenda kuwekeza wilayani hapo kwani bado kuna maeneo ya kutosha yaliyotengwa kwa ajili ya viwanda .

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha ,mkuu huyo wa Wilaya ya kibaha, alisema ,hatua inayofuata sasa ni kupeleka majina yao kwa waziri wa ardhi na maendeleo ya makazi kwa ajili ya kuwafutia umiliki.

Assumpter alisema kuwa tayari ameshaandaa orodha ya wamiliki hao , na wiki hii anaipeleka ili kufanyiwa kazi.

“Wapo baadhi yao wameshindwa kuendeleza kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitano na wengine miaka 15 wakati sheria inataka mmiliki kuendeleza eneo ndani ya miaka mitatu na endapo atashindwa kuendeleza unaweza kunyanganywa eneo husika,” alisema Assumpter .

Alieleza viwanja ambavyo havikuendelezwa kabla ya agizo hilo vilikuwa 1,000 ambapo waliojitokeza ni 246 kuelezea mipango yao .

Viwanja vya taasisi ni 189 ambavyo wahusika nao hawajajitokeza.
“Hatuwezi kuwavumilia,mji wetu wa Kibaha ndiyo makao makuu ya mkoa wa Pwani kwa kushindwa kuendeleza maeneo yao hawa tunawafutia umiliki ili wapewe watu wengine,” alisema .

Hata hivyo ,Mkuu huyo wa wilaya alisema kuwa wilaya hiyo imedhamiria kuendeleza mji huo hivyo hataki kuona vichaka ambavyo vimekuwa ni moja ya sehemu ambazo watu wanafanyiwa uhalifu.

“Watu wamekuwa wakifanyiwa vitendo mbalimbali ikiwemo wanawake kubakwa, madereva bodaboda kuporwa pikipiki na kuuwawa kutokana na mashamba na viwanja kushindwa kuendelezwa,” alifafanua Assumpter .

Akizungumzia kuhusiana na taasisi za serikali na umma ambazo zilipewa maeneo na kushindwa kuyaendeleza na kuwa hatarini kunyanganywa maeneo hayo alisema yote yamefika na kueleza jinsi gani watakavyoendeleza maeneo hayo.

Agost 10 mwaka huu ,Assumpter alitoa mwezi mmoja kwa kwa taasisi ,makampuni mbalimbali na wananchi waliokumbatia viwanja vyenye hati zaidi ya 1,000 pasipo kuviendeleza kuhakikisha wanafanya hivyo ndani ya muda huo

WAZIRI MKUU AUTAKA MKOA WA PWANI KUBORESHA MAENEO YA UWEKEZAJI

PMO_8540
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha sabuni cha KEDS wilayani Kibaha, Bw. Jack Feni (Kushoto  kwake) kuhushu  mitambo ya  kiwanda hicho   hicho  wakati alipokitembela September 19, 2017.  Kulia kwake ni. Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mahandisi Evarest Ndikilo na kulia ni Mbunge wa Kibaha Mjini, Silyvestry Koka.

Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu
........................................

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa mkoa wa Pwani waboreshe miundombinu ya maeneo waliyoyatenga kwa ajili ya ujenzi wa viwanda ili waweze kuwavutia wawekezaji wa nje na ndani.

Ametoa agizo hilo leo (Jumanne, Septemba 19, 2017) wakati akizungumza na kwa nyakati tofauti na wafanyakazi wa kiwanda cha kutengeneza sabuni ya unga cha Keds kilichopo Kibaha na kiwanda cha kutengeneza vigae cha Twyford kilichopo Chalinze.

Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na kasi ya maendeleo ya ujenzi wa viwanda mkoani Pwani na amewaagiza viongozi wahakikishe maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji yanakuwa na miundombinu muhimu kama maji, umeme na barabara.

“Nimefarijika kuona miradi hii mikubwa ya ujenzi wa viwanda ikiwa katika hatua za mwisho kukamilika, nawashukuru kwa kuunga mkono mkakati wa Rais Dkt. John Magufuli wa kukuza uchumi kupitia sekta ya viwanda.”

Amesema mbali na viwanda hivyo kutoa ajira nyingi kwa Watanzania, pia vitakapoanza uzalishaji vitawawezesha wananchi kupata bidhaa mbalimbali kama vigae kwa bei nafuu kwa kuwa vitakuwa vinazalishwa nchini.

Pia Waziri Mkuu amewataka wananchi wanaofanyakazi kwenye viwanda hivyo wawe mabalozi wazuri wa Taifa kwa kufanya kazi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa ili kuwathibitishia wawekezaji kwamba wao wanauwezo mkubwa wa kufanya kazi na hakuna haja ya kutafuta wafanyakazi kutoka nje ya nchi.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa viwanda hivyo Bw. Jack Feng amesema ujenzi wa huo umekamilika kwa asilimia 90 na sasa wako katika hatua za mwisho ikiwa ni pamoja na ufungaji wa mitambo na vinatarajiwa kuanza uzalishaji Oktoba mwaka huu.

Amesema vigae watavyovizalisha wanatarajia kuviuza kwa gharama nafuu kwa sababu asilimia 95 ya malighafi inapatikana ndani ya nchi. Pia ameahidi kutoa ajira nyingi kwa wananchi waishio kwenye maeneo yanayozunguka viwanda hivyo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarest Ndikilo amemuomba Waziri Mkuu awasaidie upatikanaji wa nishati ya umeme ya kutosha kuweza kuendesha viwanda katika mkoa huo.

Mhandisi Ndikilo amesema mahitaji waliyonayo ya nishati ya umeme ni megawati 92, ambapo kwa sasa wanasambaziwa megawati 40, hivyo ameomba suala hilo lipatiwe ufumbuzi wa haraka ili lisije kuathiri uzalishaji.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
JUMANNE, SEPTEMBA 19, 2017.

DC BAGAMOYO AKIWA SHAMBANI KWAKE AHIMIZA KILIMO CHA UBUNIFU.



Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, Majid Mwanga, amewahimiza wananchi wa wilaya  hiyo, kulima kilimo cha ubunifu ili kujiongezea kipato.

Mkuu huyo wa Wilaya ya Bagamoyo, aliyasema hayo hivi karibuni baada ya bagamoyokwanza blog kutembelea shambani kwake lililopo kata ya Kiromo wilayani humo.

Alisema, kilimo bora kitakachomuongezea kipato mtu ni kile kinachoendana na soko la zao husika.

Aliongeza kwa kusema kuwa, katika Wilaya ya Bagamoyo kuna viwanda kadhaa vya kusindika matunda, mbogamboga na viungo mbalimbali ambavyo vyote ni mazao yanayotokana na kilimo.

Majid alisema sio mwananchi ataweza kuajiriwa katika viwanda hivyo, bali kila mwananchi atafaidika kwa namna yake ikiwemo wale watakaoshughulika na kilimo cha mazao yanayohitajika kwenye viwanda hivyo.

Akitolea mfano wa Kiwanda cha viungo cha VEGETA kilichopo kata ya Kisutu wilayani Bagamoyo, mkuu huyo wa wilaya alisema kiwanda cha VEGETA kinatumia mazao ya kilimo ikiwemo, Pilipili, Nyanya NK. hivyo ni vyema wakulima wa Bagamoyo wakafanya utafiti kuhusu mazao yanayohitajika kwenye viwanda vilivypo ili walime mazao ambayo yakivunwa yanaenda sokoni moja kwa moja.

Mbali na kiwanda cha VEGETA Mkuu huyo wa wilaya amekitaja Kiwanda kingine cha Elvin kilichopo Kata ya Mapinga katika Halmashauri ya Bagamoyo, ambacho ni maalum kwa kukausha matunda ambayo yatasafirishwa nje ya nchi.

Alisema kuwa, kiwanda hicho cha Elvin ni kiwanda pia kitakachohitaji matunda ya aina mbalimbali kwa wingi ili kuweza kuzalisha bidhaa za matunda yaliyokaushwa na hivyo ni fursa kwa wakulima kutumia ubunifu wa kulima mazao ambayo tayari masoko yake yapo.

Aidha, alisema, mbali na hivyo kipo kiwanda cha Sayona Kata ya Msoga Halmashauri ya Chalinze ndani ya Wilaya ya Bagamoyo ambacho hicho ni kwaajili ya kutengeneza juisi za matunda na kwamba katika kiwanda hicho soko kubwa la matunda litapatikana hivyo ni vyema wananchi wa wilaya ya Bagamoyo wakachangamkia fursa hizo kilimo cha ubunifu kulingana na soko la zao husika ili kujiongezea kipato.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, Majid Mwanga, pamoja na majukumu yake aliyonayo ya kuingoza wilaya, hutmia muda wake wa ziada shambani, ikiwa ni sehemu ya kuonesha mfano wa kile anachokisema ambapo ameweza kupanda Migomba, Mipapai Pilipili, Ufugaji wa Samaki na Kuku wa Kienyeji.

Harakati hizi za shamba za mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, licha ya kuwa anaweza kujiongezea kipato kutokana na mazao yaliyopo shambani kwake, lakini pia ameweza kutoa ajira kwa vijana wanaofanya kazi za kuhudumia mazao hayo hapo shambani.

Ni Mfano wa Kuigwa kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, majid Hemed Mwanga, mimi na wewe tufuate njia.

    Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, majid mwanga akionesha zao la pilipili ambazo amepanda shambani kwake eneo la Kiromo.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, majid mwanga akiwa kwenye shamba lake la Migomba Kiromo wilayani humo.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, majid mwanga akionesha aina ya Mpapai ambao huzaa kwa muda mfupi katika shamba lake huko Kiromo ndani ya Wilaya yake.
Mkurugenzi wa bagamoyokwanza blog. Brother, Athumani Shomari (kulia) alipotembele shambani kwa Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, (kushoto) Alhaj Majid mwanga.