Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho
upande wa Bara, Magdalena Sakaya,ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Kaliua Mkoani
Tabora.
..........................................................................................................................................
TAARIFA RASMI
Awali ya
yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na uzima
wa afya na tukaweza kukutana hapa asubuhi hii ya leo. Tunamshukuru Mwenyezi
Mungu pia kwa kuijaalia nchi yetu kuendelea kubaki katika hali ya amani na
utulivu licha ya matatizo mengi yanayotukabili.
Pili,
nichukue fursa hii kukushukuruni nyinyi waandishi wa habari kwa kuitikia wito
wetu na kuja kutusikiliza. Ni imani yangu kuwa kama ambavyo mmekuwa mkitupa
mashirikiano mazuri katika kuwafikishia wananchi yale ambayo chama chetu
kupitia kwenu kimekuwa kikiyatolea taarifa, kwa uzito wa kipekee taarifa hii
nayo mtawafikishia Watanzania wote kupitia vyombo vyenu vya habari.
Ndugu
Waandishi wa habari,
Tumewaita
leo hii kuwaeleza juu ya maazimio ya kikao cha Baraza Kuu la Uongozi la Taifa
katika kikao chake cha dharua kilichofanyika jana, Jumapili ya tarehe
28/08/2016 Katika ukumbi wa Makao Makuu ya Chama, ofisi za Vuga. Kikao hicho
kilichoongozwa na Mwenyekiti wa muda Mhe, Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Jimbo
la Mchinga kilihudhuriwa wa Wajumbe 46 katika ya Wajumbe 60.
Ndugu
Wandishi wa Habari,
Kama
mnavyojua tarehe 21/08/2016 Chama Cha Wananchi – CUF kilikuwa na Mkutano Mkuu
Maalum wa Taifa uliofanyika katika ukumbi wa Blue Pearl, Ubungo Plaza, Dar es
Salaam. Mkutano huo ulikuwa na agenda mbili kuu, ambazo ni:-
1.
Kupokea barua ya Profesa Ibrahim Haruna Lipumba ya kujiuzulu nafasi yake ya
uenyekiti ya tarehe 05/08/2015; na
2.
Kufanya Uchaguzi wa kujaza nafasi zilizo wazi - Mwenyekiti Taifa, Makamu
Mwenyekiti na Wajumbe wanne wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.
Kufuatia
hujuma za makusudi zilizoandaliwa kwa mashirikiano ya maadui wa ndani na nje ya
chama, aliyekuwa Mwenyekiti wa muda wa Mkutano Mkuu Maalum, Mhe Julius Mtatiro
alilazimika kuakhirisha Mkutano ule mara baada ya kumalizika kwa ajenda ya
kwanza ambapo Mkutano Mkuu uliridhia kujiuzulu kwa Profesa Ibrahimu Haruna
Lipumba kwa azimio lililoungwa mkono na wajumbe 476 dhidi ya wajumbe 14
waliokataa.
Hivyo basi agenda namba 2 haikuwahi kukamilishwa, na kwa hivyo
haikufanyiwa maamuzi.
Kikao cha
Baraza Kuu la Uongozi, kilichokaa jana kimejadili kwa kina juu ya hujuma za
kuvuruga Mkutano Mkuu Maalum wa tarehe 21/08/2016. Baraza kuu limesikitishwa
sana na kitendo kile ambacho mbali ya kukisababishia chama hasara ya zaidi ya
Shillingi milioni 600, pia kimepelekea kuharibu taswira ya chama ndani na nje
ya nchi.
Baraza Kuu
lilipata nafasi ya kupokea maelezo ya kina kutoka kwa wajumbe mbali mbali hasa
wale wanaotokea Tanzania Bara walioeleza kwamba hujuma zilizofanywa kuvuruga
Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa tarehe 21 Agosti, 2016 hazikuwa za bahati mbaya
au za kushtukiza bali ni matokeo ya njama na mbinu ovu na chafu ambazo zimekuwa
zikipangwa na kutekelezwa chini kwa chini kwa muda mrefu.
Wajumbe wa Baraza Kuu
la Uongozi la Taifa walieleza kwa ushahidi jinsi baadhi ya viongozi wa Chama
walioaminiwa na kupewa nyadhifa za juu walivyogeuka na kuanza kutumiwa na
maadui wa nje ya Chama kukihujumu Chama.
Baraza Kuu
limezingatia kuwa CUF ni chama cha kistaarabu, ni Chama cha Kidemokrasia na ni
Chama chenye kutoa matumini ya mabadiliko ya kweli kwa Watanzania walio wengi.
Vurugu zilizojitokeza ni aibu na fedheha kwa chama chetu mbele ya macho ya
Watanzania na wapenda demokrasia.
Baraza Kuu
la Uongozi la Taifa limeridhika kwamba watu hao waliokuwa vinara wa vurugu na
njama hizo ovu walipewa nafasi mara kadhaa kujirekebisha dhidi ya mwendo wao
huo dhidi ya Chama lakini waliendelea na vurugu na hujuma zao hizo. Kwa hatua
iliyofikia, Baraza Kuu limeona halina njia nyengine ya kukinusuru Chama
isipokuwa kuchukua hatua kali na madhubuti kukilinda Chama ambao ni wajibu wake
kikatiba.
Kwa msingi
huu basi, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa kauli moja (unanimously) limeamua
kuchukua hatua za kinidhamu kwa viongozi na wanachama mbali mbali waliohusika
kwa njia moja au nyengine katika kuchochea vurugu zile. Baraza kuu limechukua
hatua mbili kubwa ambazo ni kutoa karipio kali, kusimamisha na kufukuza
uanachama wahusika wote walioshiriki kuchochea vurugu hizo.
Viongozi
waliopewa karipio kali kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(b) ambao
ni wajumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa ni:
1.
Rukiya Kassim Ahmed na
2.
Athumani Henku
Viongozi
waliosimamishwa uanachama kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(c),
hadi hapo watakapopata fursa ya kujieleza mbele ya Baraza Kuu ni;
1.
Prof Ibrahim Haruna Lipumba
2.
Magdalena Sakaya
3.
Abdul Kambaya
4. Ashura
Mustafa
5.
Omar Mhina Masoud
6.
Thomas Malima
7.
Kapasha M. Kapasha
8.
Maftaha Nachumu
9.Mohamed
Habib Mnyaa
10.
Haroub Shamis
na
11.
Mussa Haji Kombo
Mwanachama
aliyefukuzwa chama ambaye alipata fursa ya kujieleza mbele ya Baraza Kuu na
kikao kuamua kumfukuza chama kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(c)
ni aliyekuwa Kaimu Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wazee wa CUF (JUWACUF), Shashu
Lugeye.
Kufuatia
maamuzi hayo, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limewateua viongozi mbali mbali
kukaimu nafasi mbali mbali zilizoachwa wazi.
Kwa
kuzingatia kwamba kutokamilika kwa Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa tarehe 21
Agosti, 2016 kulipelekea kushindwa kufanyika kwa uchaguzi wa Mwenyekiti na
Makamu Mwenyekiti wa Chama, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limetumia uwezo
liliopewa na Katiba ya Chama, Ibara ya 101 na 118, kuunda Kamati ya Uongozi
ambayo itakuwa ikifanya kazi za Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti hadi hapo
uchaguzi wa kujaza nafasi hizo utakapofanyika. Baraza Kuu la Uongozi limewateua
wafuatao kuwa wajumbe wa Kamati hiyo ya Uongozi:
1.
Mhe. Julius Mtatiro – Mwenyekiti;
2.
Mhe. Katani Ahmed Katani – Mjumbe; na
3.
Mhe. Severina Mwijage – Mjumbe.
Aidha Baraza
Kuu la Uongozi la Taifa, kwa kufuata Ibara ya 105 (1) na (3) ya Katiba ya
Chama, limemteua Mhe. Joran Bashange kuwa Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Chama kwa
upande wa Tanzania Bara na Mhe. Mbarala Maharagande kuwa Kaimu Naibu Mkurugenzi
wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma hadi hapo nafasi hizo zitakapojazwa
rasmi kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Chama.
Mwisho,
Baraza Kuu la Uongozi la Taifa linawahakikishia wanachama na wapenzi wake na
Watanzania wote kwa ujumla kuwa Chama Cha Wananchi – CUF kipo imara na makini na
katu hakitoyumbishwa kwa hila na njama ovu na chafu zinazofanywa na maadui wa
chama hichi. Tangu kuasisiwa kwake, CUF imeandamwa na maadui wa kila aina, na
imepitia katika misuko suko mingi. Tunaamini hila na njama hizo ovu zimekuwa
zikielekezwa CUF kwa kutambua kwamba Chama hichi ndicho kinachobeba dhamira ya
dhati ya kuleta mabadiliko ya kweli hapa nchini.
Kutokana na
umadhubuti, umakini na uimara wa Katiba ya Chama na safu ya viongozi wake, CUF
imeweza kuvuka salama kila ilipoingia katika misuko suko hiyo na kwa hivyo,
hata wimbi hili lililoonekana kukitikisa Chama limekabiliwa ipasavyo na sasa
kazi iliyopo mbele yetu ni kuendeleza harakati za kisiasa za kuwaletea
Watanzania wa Bara na Zanzibar mabadiliko wanayoyataka.
HAKI SAWA KWA WOTE
Nassor Ahmed
Mazrui- +255 777 426 975
NAIBU KATIBU
MKUU CUF
Mawasiliano:
Mkurugenzi Habari - Salim Biman 077414112
K/Naibu
Mkurugenzi : Mbarala Maharagande- 0784 001408