Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka akifungua
Semina ya mafunzo kwa wadau wa usafirishaji (hawapo pichani), kuhusu Sheria ya
Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za
mwaka 2018 inayofanyika katika ukumbi wa Hazina mkoani Dodoma.
............................................
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka
ameutaka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kuongeza wigo wa utoaji elimu
juu ya Sheria ya Afrika Mashariki ya udhibiti uzito wa magari ya mwaka 2016 na
kanuni zake za mwaka 2018.
Ameyasema hayo wakati akifungua
semina ya mafunzo ya sheria hiyo kwa wadau wa usafirishaji yaliyoandaliwa na
Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS),
yanayofanyika kwa siku moja mkoani Dodoma katika ukumbi wa Hazina
“Toeni elimu ya kutosha kwa wadau wa
usafirishaji nchini, tumieni vyombo vya habari kwa kuandaa vipindi maalum vya
redio na televisheni ili kuweza kuwafikia wadau wengi zaidi na hivyo
kufanikisha azma ya Serikali ya kuhakikisha kuwa barabara hizi zinalindwa
ipasavyo”, amesema Mtaka.
Ameongeza kuwa changamoto
zinazowakumba watendaji wa mizani kutoka kwa wadau wa usafirishaji, zinatokana
na baadhi ya wadau hao kukosa uelewa wa kutosha juu ya sheria ya Afrika
Mashariki ya udhibiti wa uzito wa magari ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka
2018.
Naye Meneja wa TANROADS Mkoa wa
Dodoma, Mhandisi Leonard Chimagu, amesema kuwa mafunzo hayo ni muendelezo wa
elimu inayotolewa kwa wadau wa usafirishaji kuhusu sheria hiyo iliyoanza
kutumika nchini Machi mosi mwaka 2019.
Mhandisi Chimagu amesema kuwa awali
Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS),
ilifanya mafunzo hayo nchi nzima mwezi Oktoba mwaka 2020 na kwamba mafunzo hayo
ni jukwaa muhimu la wadau wa sekta ya usafirishaji, kufanya majadiliano kuhusu
sheria hiyo, kushauri au kutoa maoni yatakayostawisha utekelezwaji wake.
Aidha mmoja kati ya wadau wa
usafirishaji Juma Mussa, anayeshiriki mafunzo hayo amewaambia waandishi wa
habari kuwa uelewa juu ya sheria hiyo utawasaidia kudhibiti uzito wa magari yao
na hivyo kuepukana na makosa wanayoyafanya kwa kukosa uelewa, hali
itakayopelekea mtandao wa barabara nchini kudumu kwa muda mrefu bila kuhitaji
matengenezo ya mara kwa mara.
Mafunzo ya Sheria ya Afrika Mashariki
ya Udhibiti Uzito wa Magari ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018
yamepangwa kufanyika katika Mikoa 13 ikiwemo Dar es Salaam, Mtwara, Morogoro,
Dodoma, Njombe, Mbeya, Rukwa, Ruvuma, Kigoma, Geita, Tabora, Mwanza, Arusha na
Tanga, ambapo hadi kufikia sasa tayari, wadau wa usafirishaji katika mikoa ya
Dar es Salaam, Mtwara na Morogoro tayari wamenufaika na mafunzo hayo.
Imetolewa na Kitengo cha
Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania
(TANROADS), Mhandisi Leonard Chimagu akimkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Anthony Mtaka (hayupo pichani), kufungua Semina ya mafunzo kwa wadau wa
usafirishaji (hawapo pichani), kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya
Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika katika
ukumbi wa Hazina mkoani Dodoma.


Baadhi ya washiriki wa semina ya mafunzo ya
Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni
zake za mwaka 2018 wakimsikiliza mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony
Mtaka (hayupo pichani), wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo yanayofanyika kwa
siku moja katika ukumbi wa Hazina mkoani Dodoma.

Watoa Mada wa semina ya mafunzo kwa wadau wa
usafirishaji kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya mwaka 2016 na kanuni
zake za mwaka 2018 inayofanyika katika ukumbi wa Hazina mkoni Dodoma, wakiwa
kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka.

Baadhi ya washiriki wa semina ya
mafunzo kwa wadau wa usafirishaji kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya
Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika katika
ukumbi wa Hazina mkoani Dodoma, wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka.
Picha na WUU