Sunday, October 29, 2023

MAGAZETI YA LEO TAREHE 30 OKTOBA 2023.

 


































TaSUBa KITOVU CHA MAFUNZO TASNIA ZA SANAA NA UTAMADINI NCHINI-DKT. BITEKO

 

Amefunga tamasha la 42 la Kimataifa la Utamaduni Bagamoyo.


Aipongeza Wizara kwa kutangaza utamaduni wa nchi.


Sanaa iwe nyenzo kuunganisha wananchi


Imeelezwa kuwa, Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) ni kitovu cha mafunzo katika tasnia za Sanaa na Utamaduni nchini na Serikali imeendelea kuiboresha taasisi hiyo kwa kutoa fedha za kuboresha miundombinu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia. 


Hayo yameelezwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko alipomwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na TaSUBa mkoani Pwani Oktoba 28, 2023.


"Niwapongeze Wizara kwa kuitangaza nchi yetu kwa kupitia kazi mbalimbali za utamaduni, sanaa na michezo. Aidha nakupongeza Waziri na wafanyakazi wa Wizara yako kwa kazi kubwa mnayoifanya kila mwaka katika kuliandaa na kuliendesha Tamasha hili kwa kipindi cha miaka 42 sasa," amesema Dkt. Biteko.


Ameongeza kuwa, tamasha hilo lina hadhi kitaifa na kimataifa kwani limehusisha ushiriki wa vikundi vingi vya sanaa vya hapa nchini na vya kutoka nje ya nchi zikiwemo Zambia, Kenya, Burundi, Uganda, Botswana, Afrika Kusini, Canada na nyinginezo.


Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameipongeza taasisi hiyo kwa kukuza utalii wa kiutamaduni (cultural tourism) hapa nchini jambo linalofanya kuendelea kuvutia utalii wa ndani na nje ya nchi.


 "Nawakaribisha na kuwahimiza vijana wote wa kitanzania wenye vipaji vya sanaa kuchangamkia fursa hii kwani sanaa sasa ni ajira hivyo tuitumie vyema kupitia taasisi hii," amesisitiza Dkt. Biteko.


Vile vile, Dkt. Biteko ameitaka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuwa na Mipango mikakati ya kuwasaidia wasanii nchini ili kupitia sanaa hiyo waweze kunufaika kiuchumi na kuitangaza nchi. Amesisitiza wapewe ushirikiano ili Sekta hiyo iwe na mchango mkubwa katika Pato la Taifa.


Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amesema kuwa, tamasha hilo limekua na mafanikio makubwa kwa Bagamoyo na mkoa wa Pwani. Amesema wadau wamejitokeza kwa wingi na kulifanya liwe tamasha bora nchini.


Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa amesema kuwa, tamasha hilo ni fursa ya kutangaza utalii uliopo nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya nchi. Amesisitiza kuwa mwaka 2024 tamasha litakuwa kubwa kwa kuwaleta wadau wengi zaidi nchini.


Wengine walioshiriki kilele cha tamasha hilo ni Mkuu wa Chuo TaSUBa, Dkt.Herbert Makoye, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Halima Okash na Watendaji wa Taasisi za Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wadau wa Sanaa na Utamaduni. Maonyesho hayo ambayo hufanyika kila mwaka yalianza rasmi tarehe 26 mwezi huu na kilele chake ilikuwa Oktoba 28, 2023. 






MAGAZETI YA TANZANIA LEO TAREHE 29 OKTOBA 2023.

 








Saturday, October 28, 2023

ZAIDI YA BILIONI 4 KUTUMIKA UPANUZI WA BARABARA BUKOBA.

 

Na Alodia Babara


Bukoba. 


zaidi ya Shilingi bilioni 4.4 zitatumika katika upanuzi wa barabara ya lami ya njia nne yenye urefu wa kilomita moja katika manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.


Barabara hiyo ambayo tayari imeanza kutengenezwa itasaidia kuondoa kona kali na kupunguza mlima katika eneo la Nyangoye ambalo lilikuwa linasababisha ajali kwa wingi.


Kaimu meneja Wakala wa barabaraTanroads mkoa wa Kagera Mhandisi Ntuli Mwaikokesya akizungumza mbele ya waziri wa ujenzi Innocenti Bashungwa leo Oktoba 28, 2023 amesema, barabara hiyo inajengwa kilomita moja awamu ya kwanza kuanzia mzunguuko wa barabara ya Rwamisenyi hadi mtaa wa Mitagi.


Mhandisi Mwaikokesya amesema kuwa, mradi huo ulishaanza tangu Oktoba mosi, mwaka huu utatekelezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi Oktoba mosi, mwaka 2024 na mkandarasi atakayetekeleza mradi huo ni Abemlo Contractors Ltd.


“Kwa sasa shughuli tunazofanya ni kuhamisha miundombinu ya maji, umeme na simu na wananchi  wameondoa kwa hiyari nyumba zao na mkandarasi anaendelea na shughuli za kusawazisha eneo la mradi” amesema mhandisi Mwaikokesya.


Ameongeza kuwa, barabara hiyo itajengwa awamu nne awamu ya kwanza imeanza, ya pili ni kutoka mtaa wa Mitaga hadi stend kuu ya Bukoba mita 600, ya tatu ni mita 650 ambapo mita 400 kutoka mzunguko wa barabara ya Rwamishenye kwenda Muleba na mita 250 kutoka mzunguko wa barabara ya Rwamishenyi kuelekea barabara iendayo wilaya ya Misenyi na awamu ya nne ni kutoka stend kuu hadi Bandari ya Bukoba.


Aidha Waziri wa ujenzi Innocent Bashungwa amesema kuwa, kipande cha mita 600 kutoka mtaa wa Mitaga hadi stend kuu ya Bukoba ambacho kitatengenezwa awamu wa pili ataenda kumuomba Rais ili serikali iongeze fedha za kipande hicho kitengenezwa kwa awamu moja ambayo tayari imeishaanza.


“Kwa jitihada nzuri za serikali katika ujenzi wa stend kuu ya Bukoba ngoja nikatoe mrejesho kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwamba ule utamu wa barabara ya njia nne wa kilomita moja kuanzia Rwamishenyi usiishie Mitaga basi uje moja kwa moja ili awamu ya kwanza iishie stend kuu” amesema Bashungwa.


Jawil Mahamud ni mkazi wa manispaa ya Bukoba ambaye amesema kuwa, hata kama waliumia nyumba zao kubomolewa, lakini anapongeza kutengenezwa kwa barabara hiyo na kusema kuwa wanahitaji maendeleo na barabara hiyo ilishachukua maisha ya watoto na ndugu zao wengi, wanafurahi kupanuliwa kwake kwani itaepusha ajali zilizokuwa zinatokea eneo hilo.


Aresius Ntwara mkazi wa Hamugembe manispaa ya Bukoba alisema, barabara hiyo ilikuwa finyo hivyo serikali kuipanua kutoka njia mbili kwenda njia nne pamoja na kuondoa changamoto ya ajali pia itasaidia hata mji wa Bukoba kukua kimaendeleo