KURASA ZA MBELE
Saturday, October 28, 2023
Friday, October 27, 2023
DKT. TULIA ACKSON ACHAGULIWA KUWA RAIS WA MABUNGE DUNIANI.
Spika wa Bunge la Jamahuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Tulia Ackson amechaguliwa kuwa Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) katika uchaguzi uliofanyika leo Oktoba 27, jijini Luanda nchini Angola.
Dkt. Ackson amechaguliwa kwa kupata kura 172 kati ya kura 303 zilizopigwa na anarithi mikoba ya rais aliyemaliza muda wake, Duarte Pacheco kutoka Ureno aliyekuwa rais wa IPU kwa mihula mitatu.
Tulia alipata ubunge nchini Tanzania mwaka 2015, na baadae kuchaguliwa kuwa Naibu Spika na hatimae Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akizungumza mara baada ya uchaguzi huo, Dk Tulia Ackson amesema, “Asanteni kwa kuniamini kwa kunichagua, naipokea nafasi hii kwa unyenyekevu huku nikitambua majukumu yote yanayoambatana na nafasi hii, napenda kuwathibitishi tena kuwa, jitihada zangu za kufanya kazi mkono kwa mkono na wote ili kuifanya IPU iwe na ufanisi zaidi, yenye kuwajibika na uwazi.”
Wabunge wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) walipiga kura ya siri, huku kukiwa na wagombea wanne, ambapo rais mpya Dkt. Tulia Ackson, alipata kura 172 sawa na asilimia 57 ya kura zote zilizopigwa, huku wagombea wengine ni Catherine Gotani Hara kutoka Malawi, aliyepata kura 61, Adji Diarra Mergane Kanouté, kutoka Senegal, aliyepata kura 59, na Marwa Abdibashir Hagi kutoka Somalia aliyeambulia kura 11. Wote wakiweka historia ya kuwa wabunge wanawake kutoka Afrika, waliogombea nafasi hiyo.
Dkt. Tulia Ackson anakuwa Rais wa 31 wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) na anakuwa mwanamke wa tatu kushika nafasi hiyo baada ya Najma Heptulla kutoka India (1999–2002) na Gabriela Cuevas kutoka Mexico (2017–2020), pia Dkt. Dulia Ackson anakuwa mwanamke wa kwanza kutoka Afrika kushika nafasi hiyo.
MSIGWA AZINDUA RASMI TAMASHA LA SANAA BAGAMOYO.
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa amefungua rasmi Tamasha la 42 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo lililohudhuriwa na wananchi na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi ambapo alisema kuwa Utamaduni na Sanaa ni Sekta zenye umuhimu mkubwa katika kuleta maendeleo na kukuza ajira hapa nchini.
Katibu Mkuu Bw. Msigwa amesema hayo usiku wa Oktoba 26, 2023 wakati akifungua rasmi tamasha hilo linaloendelea katika viwanja vya Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa).
"Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua kwamba eneo la Sanaa katika nchi yetu ni la kimkakati, ni lazima tulitumie kimkakati, naomba sana vijana wenye vipaji wasizuiliwe kufanya Sanaa, huku nako kuna ajira" amesisitiza Katibu Mkuu Bw. Msigwa.
Hafla ya ufunguzi wa Tamasha hilo ambalo linafanyika kwa siku tatu kuanzia Oktoba 26 - 28, 2023 katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBA) limehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Bodi ya taasisi hiyo Bw. George Yambesi, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa Dkt. Emmanuel Ishengoma, viongozi na wakazi wa Wilaya ya Bagamoyo.
Wednesday, October 25, 2023
WAJASIRIAMALI WAHIMIZWA KURASIMISHA BIASHARA BRELA
Tuesday, October 24, 2023
BODI MPYA YA USHAURI YA WIZARA YA AFYA (MAB) KWA TMDA YAZINDULIWA
Na. WAF - Dodoma
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu Oktoba 23, 2023 amezindua rasmi bodi mpya ya ushauri ya Wizara ya Afya (MAB) kwa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ambayo inawajumbe Saba.
Waziri Ummy wakati akizindua bodi hiyo mpya amewataka wajumbe hao kuimarisha usimamizi wa TMDA katika upande wa dawa, vifaa na vifaa tiba ili kusiwepo na upotevu wa aina yoyote wa vifaa tiba hivyo.
“Kazi kubwa mnayotakiwa kufanya ni ufuatiliaji wa mara kwa mara wa bidhaa duni na bandia zinazoingia kwenye soko ili zisiwafikie wananchi wakazitumia”. Amesema Waziri Ummy
Lakini pia wakati akifungua bodi hiyo Waziri Ummy amewataka wajumbe hao kuharakisha utoaji wa vibali na leseni mbalimbali ili kutokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara wa dawa, Vifaa na Vifaa Tiba.
“Kwakweli niwapongeze kwa hili bodi iliyomaliza muda wake, sikusikia malalamiko ya mtu kucheleweshewa leseni au kibali cha kufanya biashara hivyo bodi hii mpya mkaliendeleze hili”. Amesema Waziri Ummy
Aidha, Waziri Ummy amepongeza bodi iliyopita kwa kufanya kazi zake kwa weledi ambalo TMDA imepiga hatua kubwa kwenye masuala mbalimbali ndani na nje ya chi na mafanikio ambayo Wizara pia inajivunia kuyafikia na kuitaka bodi mpya kuendeleza mazuri hayo.
“Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana kwa bodi iliyopita ni pamoja na kuboresha mifumo ya utoaji huduma kwa wananchi ikiwemo mifumo ya TEHAMA kwenye kutoa vibali vya uingizaji bidhaa nchini ambapo sasa vibali vinatolewa ndani ya masaa 24”. Amesema Waziri Ummy
Bodi hiyo iliyoundwa na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu ina wajumbe Saba ambayo inaongozwa na Mwenyekiti aliyeongezewa muda kwa kipindi kingine Bw. Erick Shitindi, Prof. Appolinary Kamuhabwa (Mjumbe) ambae ni Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS).
Pia, Bi. Mariam Mwanilwa (Mkurugenzi wa Mishahara na Maslahi ya Watumishi wa Umma-Ofisi ya Rais Utumishi), CPA Chiku Thabit Yusuf (Mkuu wa Kitengo cha Uhasibu Shirika la Hifadhi ya Jami (NSSF), Wakili Patricia Maganga (Mwanasheria Mbobezi).
Vile vile yupo Bw. Daudi Msasi (Mfamasia Mkuu wa Serikali) na Bw. Adam M. Fimbo ambae ni Katibu lakini pia ni Mkurugenzi Mkuu wa TMDA.
Monday, October 23, 2023
ULEGA, PROF. KITILA WAKUTANA KUJADILI MAENDELEO SEKTA YA MIFUGO NA UVUVI
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amekutana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo na kufanya mazungumzo yaliyolenga kufahamu vipaumbele muhimu vya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambavyo vitajumuishwa katika mapendekezo yatakayosaidia kuandaliwa kwa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa mwaka 2024/2025.
Katika kikao hicho ambacho kimefanyika Oktoba 23, 2023 katika Ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi, jijini Dodoma, Prof. Kitila aliongeza kuwa, kikao hicho kimelenga kuleta ushirikishwaji wa sekta katika maandalizi ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2024/2025.
Kwa upande wake, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ameahidi kufanya kazi kwa karibu na Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji ili sekta za mifugo na uvuvi ziweze kutekeleza majukumu yake sambamba na Mpango wa Maendeleo wa Taifa.
Aidha, Mhe. Ulega ameomba masuala yanayohusu uanzishwaji wa Mamlaka inayosimamia Uvuvi, Chanjo ya Mifugo , Bandari ya Uvuvi ya Bagamoyo na Uchumi wa buluu na Programu ya Jenga Kesho Iliyobora (BBT-LIFE) kujumuishwa katika mapendekezo hayo.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Dkt. Tausi Kida ametoa rai kwa Wizara hiyo kuzingatia uzalishaji wenye tija na upatikanaji wa masoko wa bidhaa zinazozalishwa huku akigusia matumizi ya teknolojia katika uzalishaji akitolea mfano ufugaji wa Samaki.



































































