Wednesday, October 27, 2021

RC MKIRIKITI: NATAKA FEDHA ZA MIRADI ZISICHEZEWE HOVYO

 No description available.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti (kulia) akisikiliza taarifa kuhusu mradi wa ujenzi wa shule ya sekondarri ya wasichana Matai toka kwa Mkurugenzi Mtendaji  Halmashauri ya Kalambo  Shafii Mpenda (kushoto)  alipokagua mradi huo ambapo hajaridhishwa na matumizi ya fedha. Katikati  ni Mkuu wa Wilaya ya Kalambo Tano Mwera.

.........................................

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti  ameonya watendaji wa serikali Mkoani humo kutotumia vibaya fedha za miradi ya maendeleo zinazotolewa na serikali.

 

Akiwa kwenye ziara ya ukaguzi wa miradi wilayani Kalambo Tarehe 26 oktoba 2021, Mkirikiti hakuridhishwa na namna fedha kiasi cha shilingi milioni 60 zilivyotumika katika ujenzi wa madarasa matatu katika sekondari ya  Wasichana Matai  .

 

"Nataka kuona fedha za umma zinazotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan zinatumika kwenye miradi mipya iliyopangwa na wala si kwa miradi viporo kwenye halmashauri yenu ya Kalambo. Sijafurahi kuona mradi huu wa majengo matatu ya darasa shule ya sekondari ya wasichana Matai kutokamilika licha fedha zote milioni 60 kuisha" alisema Mkirikiti 

 

Mkirikiti  alibainisha kuwa hataki kuona fedha zilizotolewa na serikali kwa ajili ya utekelezaji  mpango wa maendeleo na mapambano dhidi ya UVIKO-19 zitumike kwenye miradi ya zamani bali halmashauri  ikamilishe miradi viporo kwa kutumia fedha za mapato ya ndani.

 

"Kuweka tiles (marumaru) kwenye darasa siyo mbadala wa kutoweka madawati na meza. Tafuteni fedha shule hii ikamilike" aliagiza Mkirikiti.

 

Kufuatia hali hiyo Mkuu huyo wa Mkoa aliagiza viongozi wa wilaya hiyo kuongeza umakini kwenye usimamizi wa miradi pamoja na kuzingatia vigezo vilivyomo ndani ya (BOQ) ili miradi iwe bora na kuendana na thamani ya fedha.

 

Akizungumza kwenye eneo la mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo Shafii Mpenda alisema shule hiyo ya wasichana Matai inatarajiwa kuanza mwezi Januari 2022 kutokana na kutokamilika kwa vigezo vilivyotolewa na Mkaguzi Mkuu wa Elimu Kanda.

 

Mpenda amemthibitishia Mkuu wa Mkoa kuwa amejipanga kushirikiana na watendaji  wenzake kusimamia matumizi ya fedha kwenye miradi na kuepusha ubadhilifu unaoweza kusababisha miradi kutokamilika kwa wakati.

 

Mkuu huyo wa Mkoa amenza ziara ya kikazi ya siku mbili wilayani Kalambo ambapo atakagua miradi ya maendeleo, kuhamasisha wananchi kushiriki shughuli  za kukuza uchumi na kuelimisha juu ya kujiandaa na zoezi la sensa ya watu na makazi litakalofanyika mwakani.

No description available.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti akisalimiana na wajumbe wa Kamati ya Usalama Wilaya ya Kalambo leo alipoanza ziara ya kikazi ya siku mbili wilayani humo. Nyuma yake ni Mkuu wa Wilaya ya Kalambo Tano Mwera (aliyevaa shati jeupe).


No description available.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti akikagua mlango uliotumika kwenye ujenzi wa madarasa  mawili shule ya sekondari  Matai wasichana ambapo amebaini kukiukwa kwa vigezo vilivyoaninishwa kwenye  (BOQ) kutokana vifaa kuonekana kuwa na ubora hafifu.

No description available.

Watumishi wa Halamshauri ya Wilaya ya Kalambo wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti leo wakati alipoanza ziara ya kikazi wilayani humo.

(Habari na Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa)

TAMASHA LA AINA YAKE BAGAMOYO 2021.

 No description available. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbas, akizungumza katika ukumbi wa TaSUBa wakati wa kutoa Taarifa ya Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka 2021 ambalo litaanza Tarehe 28oktoba hadi tarehe 30 oktoba 2021.

...........................................

Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbas amesema Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni la mwaka huu wa 2021 litakuwa la aina yake kwa kuwepo kwake Burudani, Matembezi ya kitalii na vyakula vya asili ambavyo vitapatikana katika siku zote tatu za Tamasha hilo.

 

Dkt. Abbas ameyasema hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa Habari katika ukumbi wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni (TaSUBa) mjini Bagamoyo kuhusu Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni ambalo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi Tarehe 28 Oktoba 2021 na kufungwa Tarehe 30 Oktoba 2021.

 

Alisema katika Tamasha hilo la siku tatu kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali ambao watatoa burudani za aina yake katika viwanja vya TaSUBa vilivyopo ufukweni mwa Bahari ya hindi, na kuongeza kuwa siku hizo tatu zitakuwa ni siku za kuondoa mawazo kwa wale wote watakaohudhuria.

 

Aidha, alisema kuwa, siku ya tarehe 30 oktoba 2021 itakuwa ni siku ya kutemebelea mbuga ya wanayama ya Saadan safari ambayo itawajumuisha wageni waalikwa, wageni maalum, wasanii na wananchi watakaopata fursa ili wageni watakaotoka nje ya nchi waweze kujionea vivutio vilivyopo Tanzania na hatimae wakaaitangaze Tanzania kwa katika uso wa dunia.

 

Akizungumzia aina za sanaa zitakazokuwepo katika Tamasha hilo, Dkt. Abbas alisema, kutakuwa na maonyesho mbalimbali ya sanaa yakiwemo ya Sarakasi, Maigizo, Uchongaji, na Uchoraji sambamba na burudani kutoka wasanii mashuhuri wakizazi kipya na ngoma za asili.

 

Alisema zaidi wasanii 60 kutoka Tanzania wamethibitisha kushiriki Tamasha hilo huku nchi zaidi ya tano zimethibisha kuleta wasanii wake katika Tamasha hilo la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka huu 2021.

 

Aliongeza kuwa, lengo la wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Serikali ya awamu ya sita kwa ujumla ni kuendeleza, kuzikuza na kuzifanya sekta za sanaa na utamaduni ziwe na mchango mkubwa katika Taifa la Tanzania kwa kukuza kazi za wasanii na kutengeneza ajira kwa vijana kupitia sanaa na utamaduni.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama (KUU) Mkoa wa Pwani, ambae pia ni Mkuu wa Mkoa huo, Abubakar Kunenge amesama hali ya usalama katika mkoa huo ipo vizuri na kwamba amewahakikishia usalama wageni wote watakaokuja kwenye Tamasha na kwamba wanapaswa kushiriki kwa furaha bila hofu ya aina yoyote ile.

 

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa wa Pwani, ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuionyesha dunia kuwa wilaya ya Bagamoyo ambayo ipo Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa wilaya zenye vivutio vikubwa vya utalii katika Tanzania.

 

Alisema kitendo cha Rais Samia kufika Bagamoyo katika maandalizi na utengenezaji wa filamu ya ‘’Royal Tour’’ ni kielelezo tosha kuwa Bagamoyo ni kitovu cha utalii na kwamba Tamasha hilo la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni ni muendelezo katika dhamira ya Rais Samia ya kuitangaza Bagamoyo na Tanzania kwa ujumla.

 

Abubakari Kunenge ameongeza kuwa, wageni wote watakaofika kwenye Tamasha hilo watapata nafasi ya kutembelea maeneo yote ya vivutio vya utalii ambayo Mh. Rais Samia Suluhu Hassan alipita wakati wa kutayarisha filamu ya Royal Tour katika mji huo wa kihistoria Bagamoyo.

 

Nae Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainab Abdallaah amesema anawakaribisha wageni wote kufika katika Tamasha hilo la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kuanzia tarehe 28 Oktoba 2021 katika viwanja vya TaSUBa mjini Bagamoyo.

 

Alisema kutokana na ukubwa wa Tamasha hilo ambalo linatarajiwa kukusanya wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi, tayari kama wilaya wamefanya mazungumzo na wamiliki wa Hoteli zilizopo Bagamoyo ili kuwe na punguzo la bei kwa siku hizo tatu.

 

Tamasha la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni hufanyika kila mwaka katika viwanja vya Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) lengo  likiwa ni kuonyesha kazi na mafanikio ya wasanii, kuwaunganisha wasanii wa ndani na nje ya nchi ambapo Tamasha la Mwaka huu 2021 ni Tamasha la 40 na Kauli mbiu ya Mwaka huu ni Sanaa ni Ajira.

No description available. 

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge akizungumza katika ukumbi wa TaSUBa wakati wa kutoa Taarifa ya Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka 2021 ambalo litaanza Tarehe 28oktoba hadi tarehe 30 oktoba 2021.

No description available.No description available.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainab Abdallaah akizungumza katika ukumbi wa TaSUBa wakati wa kutoa Taarifa ya Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka 2021 ambalo litaanza Tarehe 28oktoba hadi tarehe 30 oktoba 2021.

No description available. 

Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, Dkt. Herbert Francis Makoye, (aliyesimama kushoto) akiwatambulisha wasanii watakaoshiriki Tamasha katika ukumbi wa TaSUBa wakati wa kutoa Taarifa ya Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka 2021 ambalo litaanza Tarehe 28oktoba hadi tarehe 30 oktoba 2021.

No description available. 

Meza kuu waliokaa, kutoka kulia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, Dkt. Herbert Francis Makoye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbas, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainab Abdallaah, Katibu Tawala wa wilaya ya Bagamoyo (DAS) Kasilda Mgeni. Walipokuwa katika ukumbi wa TaSUBa wakati wa kutoa Taarifa ya Tamasha la 40 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni kwa mwaka 2021 ambalo litaanza Tarehe 28oktoba hadi tarehe 30 oktoba 2021. Waliokaa nyuma yao ni wasanii mbalimbali watakaoshiriki Tamasha hilo.
No description available. 

Pichani ni wasanii mbalimbali watakaoshiriki Tamasha hilo.