Monday, August 4, 2025

TCRA YAWAFUNDA BLOGA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2025

 

Na Mwandishi Wetu

Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, wameaswa kutotoa taarifa ambazo zitaleta taharuki na machafuko ndani ya nchi hasa katika kuelekea kipindi cha Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge  na Madiwani  utakao fanyika baadaye mwaka huu (2025).


Yamesemwa hayo jana tarehe 3, Agosti 2025 na Meneja Kitengo cha Huduma za Utangazaji,TCRA, Injinia Andrew Kisaka wakati  akiwasilisha makala (mada) katika mkutano ulioandaliwa na  wa  Tume Huru ya Uchaguzi nchini (INEC) kwa  watoa maudhui mtandaoni, amesema kuwa wakati wa uchaguzi kuna mazingira ya migawanyiko, mivutano ya kijamii, na upotoshaji wa hali ya juu hivyo ni muhimu  Mabloga waepuke  kuepuka kusambaza uvumi, kuripoti kwa umakini, kutopendelea upande wowote  na kukemea lugha za chuki.


Kisaka amewataka  bloga nchini kote  kuimarisha maadili yao na kuchukua jukumu muhimu katika kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani kwa kupandisha maudhui yenye tija na kama unaona maudhui yataleta taharuki  ni bora kuachana nayo.


Aidha Kisaka ametoa mfano wa  Historia ya machafuko ya uchaguzi yaliyotea katika nchi Kenya  Nigeria (2007) na Kenya (2011), amesema kuwa, katika machafuko hayo zaidi ya watu 800 walipoteza uhai nchini Nigeria mwaka 2011 wakati nchini Kenya zaidi ya watu 1,000 walipoteza uhai na wengine 600,000 kupoteza makazi.


Aidha amesema kuwa  katika mazingira magumu yenye shinikizo la juu la uchaguzi, vyombo vya habari vinaweza kujikuta vikichangia machafuko kwa kueneza uvumi au kuchochea upendeleo wa kisiasa.


Amesema ili kukabiliana na maafa wakati wa uchaguzi na baada kuna miongozo ya kuripoti ambayo inatatua changamoto hizo.


"Uvumi ndiyo chanzo kikuu cha vurugu hivyo  Vyombo vya habari vinapaswa kuchunguza kwa kina uvumi na kutoa taarifa sahihi haraka iwezekanavyo ili kuzuia mzunguko wa vurugu za kulipiza kisasi." amesema Mhandisi Kisaka.


Pia amehimiza Mabloga  kukataa lugha na vichwa vya Habari vya Kichochezi.


"Msiripoti kila kauli ya uchochezi kutoka kwa wanasiasa ,hata kama kauli hizo zinaonekana kuwa habari kwenu na zenye kuvutia msomaji acha kabisa ni muhimu kutokuzirudia kwenye vichwa vya habari, " amesema Mhandisi Kisaka na kuongeza kuwa lugha inayodhalilisha inaweza kuchochea wananchi kutenda vitendo vya kikatili.


Aidha amesema kuwa  katika kipindi hiki cha uchaguzi, ni  vyema Bloga kuchukua tahadhari binafsi  kutoa  matangazo ya moja kwa moja 'live'   ya mikutano ya kampeni za wagombea kwa sababu yanaweza leta  machafuko.


"Matangazo ya moja kwa moja 'live'  ya machafuko ya uchaguzi yanatakiwa kufanywa na Waandishi Waandamizi na  wenye  uzoefu na siyo 'One Man Show' kama ilivyo kwa Bloga .
Wanaohamasisha chuki na vurugu hawapaswi kupewa nafasi hewani," amesema Mhandisi Kisaka.

Aidha amesema kuwa  vyombo vya habari vinapaswa kuzuia kuonesha picha zinazochochea vurugu  na ikiwa  ni lazima, kusimamisha matangazo ya moja kwa moja ili kuzuia hali kuwa mbaya zaidi.


Maafa na miongozo ya kuripoti
katika hali ambapo uchaguzi unafanyika wakati wa maafa, ni sehemu ya elimu zinazotolewa kwa   Mabloga katika kuhakikisha taifa linavuka salama katika uchaguzi wa mwaka 2025 kama ilivyokuwa katika chaguzi nyingine.


WAZALISHAJI WA MAUDHUI MTANDAONI WAHIMIZWA KUHAMASISHA WANANCHI KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2025

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutanio wa Tume na Wazalishaji Maudhui Mtandaoni kuhusu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Kikao hicho cha siku moja kilifanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 03 , 2025.

 

Baadhi ya wawakilishi wa serikali waliohudhuria mkutano huo.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg.Kailima Ramadhani akitoa mada wakati wa ufunguzim wa mkutanio wa Tume na Wazalishaji Maudhui Mtandaoni kuhusu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Kikao hicho cha siku moja kilifanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 03 , 2025.

Picha ya pamoja ya washiriki 


NA WAANDISHI WETU, DAR ES SALAAM.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa Jacobs Mwambegele, amewahimiza wazalishaji wa maudhui mtandaoni kutumia majukwaa yao ya kidijitali kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.


Akizungumza leo tarehe 03 Agosti, 2025, jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa kati ya Tume na Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, Mhe. Mwambegele amewapongeza wazalishaji hao kwa ushirikiano walioutoa kwa Tume katika hatua mbalimbali za maandalizi ya uchaguzi.


Mhe. Mwambegele amewasihi wazalishaji hao wa maudhui kuendelea kuwa daraja muhimu kati ya Tume na wananchi kwa kutoa taarifa sahihi na kwa wakati.


“Tuna imani kuwa tutazidi kushirikiana nanyi kwa karibu zaidi, na mtatumia nafasi zenu kuwapatia wananchi taarifa sahihi kuhusu maendeleo ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 na kuwahamasisha kushiriki kikamilifu kwa kupiga kura,” amesema Mhe. Mwambegele.


Amebainisha kuwa Tume inatambua mchango wa wazalishaji wa maudhui mtandaoni katika njia mbili kuu. Kwanza, kama daraja la mawasiliano kati ya Tume na wadau, na pili, kama wadau wa moja kwa moja wa mchakato wa uchaguzi.


“Tume inathamini kazi yenu ya kuandaa, kuchapisha na kusambaza taarifa kupitia majukwaa mbalimbali ya kidijitali kama mitandao ya kijamii, blogu, tovuti na majukwaa ya video kama YouTube,” ameongeza.


Akizungumzia nafasi ya vijana katika uchaguzi, Mhe. Mwambegele amesisitiza umuhimu wa mawasiliano ya kidijitali kwa kundi hilo, akiwahimiza wazalishaji hao wa maudhui kutumia ubunifu wao kwa kutumia michoro, video na ujumbe wenye mvuto ili kuwafikia wapiga kura kwa njia rahisi na ya kuvutia.


Amesema lengo kuu la mkutano huo ni kujadili hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya uchaguzi, kubadilishana mawazo, na kusikiliza changamoto zinazowakabili wazalishaji wa maudhui mtandaoni ili kutafuta suluhisho kwa wakati.


“Mkutano huu si wa upande mmoja; ni jukwaa la mawasiliano ya pande mbili ambalo linawapa fursa ya kueleza changamoto zenu na kusaidia kuboresha utekelezaji wa shughuli za uchaguzi,” ameeleza Mhe. Mwambegele.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani, amehimiza waandaaji wa maudhui mtandaoni kutumia majukwaa yao kutoa habari sahihi, na zilizothibitishwa na kufanyiwa utafiti.


Ameongeza kuwa majukwaa hayo ya kidijitali yanasaidia kurahisisha upokeaji wa taarifa za Tume na kuwafikia wananchi kwa haraka.


Aidha, Bw. Kailima amewahimiza wazalishaji wa maudhui mtandaoni kutoa taarifa za mara kwa mara kuhusu mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa 2025, ikiwa ni pamoja na kuitumia kauli mbiu ya uchaguzi “Kura Yako Haki Yako, Jitokeze Kupiga Kura” ili kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi tarehe 29 Oktoba, 2025.


Mkutano kati ya Tume na Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni ni mfululizo wa mikutano ya Tume na wadau wa uchaguzi ambayo ilianza tarehe 27 Julai, 2025. Mikutano hiyo inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 04 Agosti, 2025 kwa wahariri na waandishi wa vyombo vya habari kupatiwa mafunzo.







Picha mbalimbali za washiriki wa Mkutano huo.