Sunday, August 31, 2025

MLIPUKO WAUA WAWILI BAGAMOYO

 


Watu wawili wamefariki dunia na mmoja kujeruhiwa baada ya kutokea mlipuko ambao bado haujafahamika ni wa kitu gani.


Akitoa Taarifa kwa vyombo vya habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Salim Morcase, amesema tukio hilo limetokea leo tarehe 31 Agosti 2025 Mtaa wa kichemchem kata ya Nianjema wilayani Bagamoyo majira ya saa moja na dakika ishirini asubui.


Amesema chanzo cha vifo hivyo ni mlipuko wa chuma ambacho Doto Mrisho (Marehemu) alikuwa anakikata kwenye karakana yake ya kuchomelea mageti.


Waliofariki katika tukio hilo ni Doto Mrisho mwenye umri wa miaka 24 fundi wa kuchomelea mageti mkazi wa kichemchem kata ya Nianjema na Saidi Ramadhani mwenye umri wa miaka 53 mkazi wa Sanzale Bagamoyo, na aliyejeruhuwa katika tukio hilo ni  Hassan Omari, mkazi wa Sanzale Bagamoyo.


Kamanda Morcase amesema uchunguzi wa tukio hilo unaendelea kufanyika na jeshi la polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama ili kubaini chanzo cha mlipuko huo na ni wa kitu gani.



Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linatoa wito kwa baadhi ya wananchi wenye tabia ya kuokota vyuma ambavyo hawavijui na pia waache tabia ya kukata vyuma ambavyo ni aina ya mitungi ya gesi, au chochote chenye duara au mfano wa kibuyu kidogo kilichozibwa ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza.

Thursday, August 14, 2025

MARIAN SCHOOLS MARATHON NI KESHO

 



Na Albert Thomas Kawogo.

TAASISI ya Marian Schools Bagamoyo imeandaa mbio za marathon MARIAN SCHOOLS MARATHON 2025 zitakazofanyika Bagamoyo Ijumaa ya tarehe 15  Agosti.


Msemaji wa Marian Schools, Ohsana Mnalunde amesema mbio hizo zitaanzia kwenye kijiji cha Zinga Samakisamaki na kumalizikia kwenye hoteli ya Stella Maris Bagamoyo mjini.


Mnalunde amesema tayari zaidi ya washiriki 5,000 wamethibitisha ushiriki wao huku idadi kubwa ya watu wa Bagamoyo ikionyesha nia ya kushirki mbio hizo.



Msemaji huyo amesema mgawanyo wa mbio hizo ni wa km 21, km 10 na km 5 ambapo idadi ya washiriki watarajiwa ni wanafunzi, wazazi,  wafanyakazi, walimu na wakuu wa mashrika ya serikali na binafsi pamoja na wafanyakazi wao.


Naye Meneja wa Taasisi za Marian Schools Padre Valentine Bayo amewataka watu wengi kujitokeza kujisajili ili waweze kushiriki kwani kukimbia ni afya na  kunasaidia kupunguza kasi ya magonjwa yasiyoambukiza (NCDs) kama shinikizo la damu sukari na moyo ambayo huchangia zaidi ya asilimia 30 ya vifo vyote hapa nchini.


Padre Bayo ambaye pia ni mwanzilishi wa shule za Marian amesema watu wanaingia gharama kubwa kutibu magonjwa yatokanayo na uzito wa kupindukia lakini kama wangejenga utamaduni wa kufanya mazoezi hasa kukimbia wangeepuka magonjwa hayo.


Mbio hizo ambazo kwa mwaka huu zinatimiza miaka mitatu sasa zimedhaminiwa na Benki ya KCB.

Tuesday, August 12, 2025

TBN YAKEMEA 'MANABII' WA MITANDAONI, KWA UTABIRI WAO UNAOLETA TAHARUKI KWA JAMII.

 

Mkuu wa Mawasiliano Serikalini, Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, (PDPC) Innocent Mungy, akizungumza katika mafunzo hayo.


Na Mwandishi wetu, Dar es salaam.


Mtandao wa Bloga Tanzania (TBN) umekemea vikali tabia inayoshamiri ya watu kujinadi kufanya utabiri kwa watu na taifa kupitia mitandao ya kijamii, ukisema vitendo hivyo vinakiuka Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi.


Kauli hiyo imetolewa kama azimio katika kikao kazi cha mafunzo ya mabloga kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.


Mabloga hao wameitaka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) kushirikiana kuwasaka na kuwachukulia hatua kali wale wote wanaohusika na vitendo hivyo.


Katika kikao hicho, mabloga walibainisha kuwa kumeibuka kundi la watu wanaodai kuwa ni manabii na kutoa kauli zinazokiuka sheria za nchi na kuleta taharuki kuelekea uchaguzi mkuu.


Wakitolea mfano wa kauli hizo ni kama vile kusema kutatokea kifo cha kiongozi mkubwa siku za hivi karibuni, au kutatokea machafuko fulani, na kusema kuwa kauli hizo ni za kuleta taharuki kwa wananchi na kukiuka sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi.


Walisisitiza kuwa baada ya kuchambua Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (Personal Data Protection Act), walibaini kwamba 'utabiri' wa namna hiyo unavuruga haki ya msingi ya faragha ya wahusika.


Akizungumza katika mafunzo hayo, Mkuu wa Mawasiliani Serikalini, Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, (PDPC) Innocent Mungy, amesema sheria  inakataza kutoa Taarifa za mtu binafsi bila ya ridhaa yake.


Aliongeza kwa kusema kuwa, katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wapo watu watatoa taarifa za Afya ya mtu kwa lengo la kumharibia ili asichaguliwe jambo ambalo ni kosa kisheria.


Mungy alisisitiza kuwa sheria hiyo ina adhabu kali na lazima ifuatwe na kila mtu, si tu mabloga na waandishi wa habari.


Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na TCRA, yalilenga kuwaandaa mabloga kuripoti habari za uchaguzi kwa weledi na uadilifu. 


Pamoja na mada ya ulinzi wa taarifa binafsi, mada nyingine muhimu zilizotolewa ni pamoja na Mwongozo wa Waandishi wa Habari katika Uchaguzi na Matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika uandishi wa habari.


Lengo kuu la mafunzo haya ni kuongeza uwezo wa mabloga kuhakikisha wanafuata sheria na maadili ya uandishi, jambo linalotazamiwa kuchangia mazingira ya uchaguzi yenye amani na utulivu.

Meneja wa Huduma za Utangazaji wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mhandisi Andrew Kisaka, akiwasilisha mada katika mafunzo maalumu kuelekea uchaguzi mkuu mahususi kwa bloga yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Agosti 11, 2025 Jijini Dar es Salaam








Monday, August 4, 2025

TCRA YAWAFUNDA BLOGA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2025

 

Na Mwandishi Wetu

Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, wameaswa kutotoa taarifa ambazo zitaleta taharuki na machafuko ndani ya nchi hasa katika kuelekea kipindi cha Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge  na Madiwani  utakao fanyika baadaye mwaka huu (2025).


Yamesemwa hayo jana tarehe 3, Agosti 2025 na Meneja Kitengo cha Huduma za Utangazaji,TCRA, Injinia Andrew Kisaka wakati  akiwasilisha makala (mada) katika mkutano ulioandaliwa na  wa  Tume Huru ya Uchaguzi nchini (INEC) kwa  watoa maudhui mtandaoni, amesema kuwa wakati wa uchaguzi kuna mazingira ya migawanyiko, mivutano ya kijamii, na upotoshaji wa hali ya juu hivyo ni muhimu  Mabloga waepuke  kuepuka kusambaza uvumi, kuripoti kwa umakini, kutopendelea upande wowote  na kukemea lugha za chuki.


Kisaka amewataka  bloga nchini kote  kuimarisha maadili yao na kuchukua jukumu muhimu katika kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani kwa kupandisha maudhui yenye tija na kama unaona maudhui yataleta taharuki  ni bora kuachana nayo.


Aidha Kisaka ametoa mfano wa  Historia ya machafuko ya uchaguzi yaliyotea katika nchi Kenya  Nigeria (2007) na Kenya (2011), amesema kuwa, katika machafuko hayo zaidi ya watu 800 walipoteza uhai nchini Nigeria mwaka 2011 wakati nchini Kenya zaidi ya watu 1,000 walipoteza uhai na wengine 600,000 kupoteza makazi.


Aidha amesema kuwa  katika mazingira magumu yenye shinikizo la juu la uchaguzi, vyombo vya habari vinaweza kujikuta vikichangia machafuko kwa kueneza uvumi au kuchochea upendeleo wa kisiasa.


Amesema ili kukabiliana na maafa wakati wa uchaguzi na baada kuna miongozo ya kuripoti ambayo inatatua changamoto hizo.


"Uvumi ndiyo chanzo kikuu cha vurugu hivyo  Vyombo vya habari vinapaswa kuchunguza kwa kina uvumi na kutoa taarifa sahihi haraka iwezekanavyo ili kuzuia mzunguko wa vurugu za kulipiza kisasi." amesema Mhandisi Kisaka.


Pia amehimiza Mabloga  kukataa lugha na vichwa vya Habari vya Kichochezi.


"Msiripoti kila kauli ya uchochezi kutoka kwa wanasiasa ,hata kama kauli hizo zinaonekana kuwa habari kwenu na zenye kuvutia msomaji acha kabisa ni muhimu kutokuzirudia kwenye vichwa vya habari, " amesema Mhandisi Kisaka na kuongeza kuwa lugha inayodhalilisha inaweza kuchochea wananchi kutenda vitendo vya kikatili.


Aidha amesema kuwa  katika kipindi hiki cha uchaguzi, ni  vyema Bloga kuchukua tahadhari binafsi  kutoa  matangazo ya moja kwa moja 'live'   ya mikutano ya kampeni za wagombea kwa sababu yanaweza leta  machafuko.


"Matangazo ya moja kwa moja 'live'  ya machafuko ya uchaguzi yanatakiwa kufanywa na Waandishi Waandamizi na  wenye  uzoefu na siyo 'One Man Show' kama ilivyo kwa Bloga .
Wanaohamasisha chuki na vurugu hawapaswi kupewa nafasi hewani," amesema Mhandisi Kisaka.

Aidha amesema kuwa  vyombo vya habari vinapaswa kuzuia kuonesha picha zinazochochea vurugu  na ikiwa  ni lazima, kusimamisha matangazo ya moja kwa moja ili kuzuia hali kuwa mbaya zaidi.


Maafa na miongozo ya kuripoti
katika hali ambapo uchaguzi unafanyika wakati wa maafa, ni sehemu ya elimu zinazotolewa kwa   Mabloga katika kuhakikisha taifa linavuka salama katika uchaguzi wa mwaka 2025 kama ilivyokuwa katika chaguzi nyingine.


WAZALISHAJI WA MAUDHUI MTANDAONI WAHIMIZWA KUHAMASISHA WANANCHI KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2025

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutanio wa Tume na Wazalishaji Maudhui Mtandaoni kuhusu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Kikao hicho cha siku moja kilifanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 03 , 2025.

 

Baadhi ya wawakilishi wa serikali waliohudhuria mkutano huo.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg.Kailima Ramadhani akitoa mada wakati wa ufunguzim wa mkutanio wa Tume na Wazalishaji Maudhui Mtandaoni kuhusu uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Kikao hicho cha siku moja kilifanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 03 , 2025.

Picha ya pamoja ya washiriki 


NA WAANDISHI WETU, DAR ES SALAAM.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa Jacobs Mwambegele, amewahimiza wazalishaji wa maudhui mtandaoni kutumia majukwaa yao ya kidijitali kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.


Akizungumza leo tarehe 03 Agosti, 2025, jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa kati ya Tume na Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, Mhe. Mwambegele amewapongeza wazalishaji hao kwa ushirikiano walioutoa kwa Tume katika hatua mbalimbali za maandalizi ya uchaguzi.


Mhe. Mwambegele amewasihi wazalishaji hao wa maudhui kuendelea kuwa daraja muhimu kati ya Tume na wananchi kwa kutoa taarifa sahihi na kwa wakati.


“Tuna imani kuwa tutazidi kushirikiana nanyi kwa karibu zaidi, na mtatumia nafasi zenu kuwapatia wananchi taarifa sahihi kuhusu maendeleo ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 na kuwahamasisha kushiriki kikamilifu kwa kupiga kura,” amesema Mhe. Mwambegele.


Amebainisha kuwa Tume inatambua mchango wa wazalishaji wa maudhui mtandaoni katika njia mbili kuu. Kwanza, kama daraja la mawasiliano kati ya Tume na wadau, na pili, kama wadau wa moja kwa moja wa mchakato wa uchaguzi.


“Tume inathamini kazi yenu ya kuandaa, kuchapisha na kusambaza taarifa kupitia majukwaa mbalimbali ya kidijitali kama mitandao ya kijamii, blogu, tovuti na majukwaa ya video kama YouTube,” ameongeza.


Akizungumzia nafasi ya vijana katika uchaguzi, Mhe. Mwambegele amesisitiza umuhimu wa mawasiliano ya kidijitali kwa kundi hilo, akiwahimiza wazalishaji hao wa maudhui kutumia ubunifu wao kwa kutumia michoro, video na ujumbe wenye mvuto ili kuwafikia wapiga kura kwa njia rahisi na ya kuvutia.


Amesema lengo kuu la mkutano huo ni kujadili hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya uchaguzi, kubadilishana mawazo, na kusikiliza changamoto zinazowakabili wazalishaji wa maudhui mtandaoni ili kutafuta suluhisho kwa wakati.


“Mkutano huu si wa upande mmoja; ni jukwaa la mawasiliano ya pande mbili ambalo linawapa fursa ya kueleza changamoto zenu na kusaidia kuboresha utekelezaji wa shughuli za uchaguzi,” ameeleza Mhe. Mwambegele.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani, amehimiza waandaaji wa maudhui mtandaoni kutumia majukwaa yao kutoa habari sahihi, na zilizothibitishwa na kufanyiwa utafiti.


Ameongeza kuwa majukwaa hayo ya kidijitali yanasaidia kurahisisha upokeaji wa taarifa za Tume na kuwafikia wananchi kwa haraka.


Aidha, Bw. Kailima amewahimiza wazalishaji wa maudhui mtandaoni kutoa taarifa za mara kwa mara kuhusu mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa 2025, ikiwa ni pamoja na kuitumia kauli mbiu ya uchaguzi “Kura Yako Haki Yako, Jitokeze Kupiga Kura” ili kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi tarehe 29 Oktoba, 2025.


Mkutano kati ya Tume na Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni ni mfululizo wa mikutano ya Tume na wadau wa uchaguzi ambayo ilianza tarehe 27 Julai, 2025. Mikutano hiyo inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 04 Agosti, 2025 kwa wahariri na waandishi wa vyombo vya habari kupatiwa mafunzo.







Picha mbalimbali za washiriki wa Mkutano huo.